Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, May 13, 2013

Majuto ni mjukuu huja baada ya kitendo



Mtoto mmoja  wa tajiri alijikuta akiokolewa kufa baada ya kunywa sumu, ili apendwe zaidi na wazazi wake akiwa marehemu: Je ilikuwaje,…

Wazazi tuna mtihani mkubwa wa kulea watoto wetu. Unaweza ukalea ukijua unapenda, kumbe unamponda mtoto wako mwenyewe. Tuwe makini sana.

Mzazi mwenzetu huyu, baada ya kuhangaika miaka mingi, baadaye akabahatika kupata mtoto, na furaha iliyoje kwenye familia, wewe fikiria watu walihangaika miaka saba, ili wapate mtoto, ikafikia sehemu wakakata tamaa kabisa. Mungu akasikia kilio chao, na kuwajalia mtoto binti, mrembo kweli kweli.

Hebu fikiria furaha iliyokuwa ndani ya ya hiyo familia, furaha hiyo  ilizidi ile furaha ya mgumba kupata mtoto, au kibogoyo kuota meno…. Wazazi hawa wakawa wanamlea mtoto wao kama malikia. Huduma zote muhimu akawa anapatiwa, hadi akakua akiwa na afya njema furaha na kujiamini kuwa ninapendwa zaidi ya kitu kingine , kwani Kila atakacho anakipata.

Mungu mkubwa, akawajali mtoto mwingine wa kiume. Sasa yule wa kwanza keshakua kidogo, …..ana miaka  minne, kwahiyo mapenzi yakawa sasa yanaeleka kidogo kwa mdogo wake. Hali hii ikawa inamuuma sana dada mtu, yaani kifungua mimba, kwahiyo akawa anajaribu kufanya kile anachoona mdogo wake anakifanya ili na yeye aendelee kupendwa zaidi.

*******

Siku moja mdogo wake alijikata kidole kwa bahati mbaya, wazazi wakawa na pikila pilika za kumsaidia huyo mtoto. Ilimradi mtoto asiendelee kulia, akapakwa dawa, na kununuliwa hiki na kile. Dada mtu akaona hayo matendo, kwani kwa muda huo hakuna aliyekuwa akimjali, hata pake alipoomba kitu, aliona kama wazazi wake hawamsikilizi, wao na mdogo wake tu…kuona hivyo, akaingia ndani kwake, anapolala, akachukua wembe, akajikata mkono.

Tatizo hakujali wapi ajikate, yeye alipochukua wembe kwa hasira akajikata kwenye mkono sehemu ile, yenye mshipa mkubwa, kwahiyo damu ikawa inamtoka kwa wingi sana, na wakati anafanya hilo tukio alikuwa chumbani kwake, na wazazi  wake walikuwa barazani wakihangaika na mdogo wake. Hakuna aliyekuwa na mawazo naye kwa muda huo.

Ilikuja kubainika baadaye kuwa binti hayupo, na walipohangaika kumtafuta ndio wakamkuta yupo chumbani keshapoteza fahamu kutokana na  kupoteza damu nyingi, akakimbizwa hospitalini.
Ilikuwa huzuni kweli siku hiyo kwenye familia hiyo, maana ajali mbili kwa wakati mmoja, na alipoulizwa binti ilikuwaje, yeye akajibu bila aibu kuwa alijaribu kuangalai jinsi mdogo wake alivyojkata ili na yeye asikie maumivu kama mdogo wake, kwa kumuonea huruma, na ili pia nay eye apendwe kama mdogo wake.

‘Hivi huoni ulikuwa unajiua,….?’akaambiwa.

‘Mbona mdogo wangu hakufa, na badala yake mlimpenda kuliko mimi….’akasema.

‘Wewe mjinga kweli kweli…usifanye hivyo tena…..’kauli hiyo aliiweka kichwani, kumbe yeye sasa ni mjinga, hajui, ina maana hapendwi tena….

*********

Hali ile ikaisha, na tabia ile ya kuona mdogo wake anapendwa zaidi ikawa inaendelea kumnyong’onyesha sana. Na siku moja wakati wanapita mitaa ya jirani wakitoka shule ya chekechea, wakakutana na msiba. Pale kwenye msiba, waliwaona wazazi wa mtoto aliyefariki wakilia kwa huzuni kubwa, na yeye akauliza;

‘Kwanini wanalia vile?’ akauliza

‘Kwasababu kipenzi cha hawa wazazi kimefariki, …ndio maana wazazi wa huyo mtoto wanalia hivyo.  Yeye akilini mwake ikamwiingia sana, kumbe mtu akifa anapendwa kiasi hicho, watu wanakuja kwa wingi, wanamlilia, na wazazi wanaonyesha upendo wa hali ya juu.

‘Itabidi na mimi nifanye kitu, ili nife, …lakini nikifa itakuwaje?’ akajiuliza. Hapo akafanya utafiti wa haraka, akaambiwa ukifa unakwenda kuzikwa, na unawekwa  kwenye jeneza nzuri la kifahari….

‘Oh, kumbe….basi nimelewa. ..’akasema na jioni ile akatafuta sumu ya kuulia panya, akaikoroga na kuiweka kabatini.

Muda ukafika, na akijua sasa wazazi wake wote wapo nyumbani, wakiwa na mdogo wake, yeye alikaa pembani, akiwaza alichopanga kichwani, baadaye akaingia chumbani kwake, na kuinywa  ile sumu ….Tumbo likaanza kuuma, maumivi aliyoyasikia hapo, alijuta kwanini alikunywa hivyo…na wazazi wakasikia hilo yowe na kukimblia chumbani kwake.

Yule mtoto alikimbizwa hospitalini, baada ya kupewa maziwa, …aliponea chupuchupu,..na toka siku hiyo hakutaka tena kujidekeza, akajua kuwa kumbe kila jambo lina wakati wake, faida na hasara zake. Na sasa hivi tunaposimulia hiki kisa ni muheshimiwa fulani, akiwa na majukumu ya kulea.

Wanajamii, yaliyotokea kwa watoto hawa, huenda hata sisi tunaojiona ni wazima wazima tunayo kasumba hiyo, kuwa kila wanalofanyiwa wengine , hasa likifanyika huko majuu tunaliona ni bora zaidi, huenda na sisi tukilifanya tunaweza kuwa maarufu na kupendwa na watu. Sio kweli kuwa kila lilofanywa na wengine lina maana kwetu, mengine ni sumu, tunaweza tukajikuta tunajiua wenyewe, na tuombe mungu, itokee bahati, wawepo watu wa karibuni wa kutuokoa.

Tuweni makini sana na maisha yetu, maisha ni kitu chenye thamani kubwa sana, tukichezea maisha yetu, hatari yake ni mara mbili ya hivyo tunavyofikiria, kwani hali zetu ni ngumu, maisha ni magumu, sasa uongezee na hayo matatizo, kweli tutaweza kuji,mudu.

Tujiulize ni nini tunachotaka katika uhai huu mfupi, kumbuka ni  kama jana tu walikuwepo watu mashuhuri, sasa hivi tumeshaanza kuwasahahu, wameshaondoka, na ni nini walichoondoka nacho, hakuna ….sasa tujiulize huo umashuhiri tunaoutaka kwa wanadamu wenzetu , utaweza kutuweka milele,..jibu lake ni kuwa haiwezekani kuishi milele.

Tufanyeni mambo kwa utaratibu wake, tukiwa na malengo chanya, tuache kuiga vitu tusivyokuwa na uhakika navyo, hasa kwenye afya zetu, madawa ya kulevya, kulewa, kuvuta bangi na umalaya, haya yote ni sumu katika maisha yetu. Pia tusikimbilie kuiga mambo ya kisiasa ambayo sio hulika yetu, tuwe makini na ukoloni mambo leo, ni hatari sana kwenye usalama wa nchi zetu, ili mwisho wa siku tuwe na kitu cha kujivunia, sio cha kujijutia.  

Tukumbuke kuwa majuto ni mjukuu huja baada ya kitendo....

NB: Badi nipo kwenye changamoto za hapa na pale, na hili linanipa wakati mgumu kukiendeleza kisa chetu, lakini nitajitahidi tu, tuombeane heri.


Ni mimi: emu-three

No comments :