Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, March 20, 2013

Uchungu wa Mwana Aujuaye ni Mzazi-74



 ‘Mume wangu najua nimekuwa mbaya kwako, na huenda yote niliyowahi kukufanyia hayana maana tena kwako…tenda wema uende zako. Lakini hata kama hujali wema wangu, sio sababu ya kutaka kuoa mjukuu wako, hii ni fedheha kwa familia yako, na sijui unataka watoto wako wajisikieje….’Maua akasikia sauti ya mwanamama ikiongea, …mlango ulikuwa haujafungwa vyema, kwahiyo watu wakiongea ndani unawasikia.

Maua akasimama ghafla, na kutulia, na wenzake waliokuwa wamesimama kwa mbali wakisubiria kukaribishwa kwanza, wakawa wanamwangalia Maua. Na mama Mdogo alipoona Maua kaduwaa pale mlangoni, akasema;

‘Kwanini tusiingie ndani, hamuona mlango upo wazi..’akasema mama mdogo huku akitembea kuelekea pale aliposimama Maua akitaka kuingia ndani, lakini Maua akamzuia.

‘Hebu  subirini kidogo, kuna kitu nasikiliza….’akasema Maua na mama yake akasogea karibu na aliposimama binti yake, na kumfanya mama mdogo arudi nyuma, akisonya kwa hasira. Maua akawa katega sikio kusikiliza kinachoongelewa huko ndani.

‘Mimi sioni ubaya wa mzee kama mimi kumuoa binti sawa na mjukuu wangu, na hata kama wewe umempata kijana uliyependezewa naye, ninakupa ruhusa nenda ukaolewe..’akasema Mzee na yule mama alimwangalia yule mzee kwa jicho baya, akasema;

‘Mimi sina laana hiyo….siwezi kujishushia hadhi yangu, kwa kujizalilisha kwa watoto…kwanza ili iweje, nitapata nini kwa huyo kijana, kama sio kujivunjia heshima’akasema yule mwanamama.

‘Kwasababu gani,….ngoja nikuambie kwa nini mtu kama mimi nifanya hivyo, ni kwa kuwa huyo binti ameweza kuyafanya yale ambayo mke wangu…wewe uliyekuwa mke wangu, hakuweza kunifanyia, kwanini nisimchukue binti hata kama ana umri mdogo,…..’wakasikia Mzee akisema.

‘Hahaha….unanichekesha kweli, yepi aliyokufanyia ambayo mimi nilishindwa kukufanyia, tatizo lako ni kuwa tamaa zimekuzidi, hakuna lolote na pia wewe ulitaka niwe kama mtumwa wako, kila utakalo mimi nikubali tu, nikae ndani kama mfungwa, hivi dunia ya leo ni ya kumweka ndani mke kama kitanda, ili ukija unakilalia tu….hiyo ni aibu kwako, wewe na uzee huo unamezea mate vibinti vidogo huna hata haya, hamuoni kuwa ni kujizalilisha, ….’wakasikia sauti ya mwanamke ikiongea.

‘Kwangu mimi sioni kuwa najizalilisha,….kwasabbu sijafanya ubaya, nimeamua kufuata taratibu zote, na sijawahi kusikia popote wakisema mzee, hawezi kumuoa kijana-binti mdogo, au kijana, binti mdogo hawezi kuolewa na mzee, hizo ni hisia zenu…..na sio kwamba mtu anapenda kufanya hivyo bila sababu, hali halisi inamsukuma mtu afanye hivyo….’akasema Mzee.

‘Kwahiyo kama hiyo hali halisi ikiondolewa, hutakuwa na haja ya kumuoa huyo binti?’ sauti ikauliza, ilikuwa ni sauti ya mmoja wa binti.

‘Sio rahisi kama unavyosema wewe,…. moyo ukipenda, au ukikinai jambo, kuurejesha kwenye hali nyingine inakuwa vigumu, sana sana ukilazimisha mtokeo yake ni kujiumiza…mimi hali iliyofikia kama ningeendelea kuwa na mama yenu mngekuwa mumeshanisahau,…..’akasema huku akimwangalia yule mwanamke, aliyekuwa kaangalia pembeni akiwa kama hataki kuangaliana na huyo mwanaume.

‘Angalieni, binti wa watu nimekaa naye siku mbili tu…., na sio siku mbili, maana amekuwa akija kwa muda tu, na kuondoka, angalieni mabadiliko niliyoyapata….hamuyafurahii haya mabadiliko?’akatulia.

‘Mabadiliko gani, mimi sioni ulichobadilika nacho….ni uzee tu,….hakuna jingine,  na zaidi ni ufinyu wa kufikiria kwani ukizeeka sana na akili zinasinyaa…, jiheshimu mzee, hiyo unayotaka kufanya ni aibu,..na huoni kuwa unamnyima haki huyo binti, kwani alihitajika kuolewa na kijana mwenzake, wewe umemkatili….hiyo ni dhuluma…’akasema huyo mama.

‘Unauliza mabadiliko gani,…wewe ulipoondoka uliniacha wapi,….si uliniacha nikiwa kitandani, sijiwezi,….hebu ulizia yaliyotokea hapa, walishafikia hatua wananisubiria ili wakanizike,…lakini akaja huyo binti,…ooh, jamani, …kwanini hamunielewi’akasema huyo mzee.

‘Nilikuacha kitandani kwa vile ulinifukuza, kama usingelinifukuza ningeliendelea kuwa nawe, na kukuhudumia,…..kama kufa siku zikifika utakufa tu, hata akiwepo dakitari, …..sioni kwanini umtukuze huyo binti, na nakuapia ole wake….’akatulia.

‘Mama usiseme hivyo, tulishakuomba, na ukakubali kuwa utaongea kwa amani na busara, sasa…hayo ya kuapiza yanatoka wapi tena..mama sisi tungelifurahia kama ungekuja na kuishi na baba tena, kwanini usimuonyeshe kuwa upo tayari….’akasema mmoja wa binti.

‘Inabidi nimuambie ukweli huyu baba yenu, maana itaniuma sana, kuona mzee kama huyu anaoa kibinti, na wakati nyie ni watoto wangu, eti mnaishi na binti ambaye huenda kawazidi umri, ,mnafikiria nini kitatokea, nyie hamuyajui hayo, msifikirie huku ni ulaya…’akasema na kutulia kidogo, na baadaye akasema;

‘Akiolewa huyo,….hamtaweza kumuheshimu kwa vile ni mdogo, na yeye ataona mumemzarau, ataanza kuwachongea kwa huyo mzee, na kwa vile mzee keshapenda, …unafikiri nini kitatokea…atamasikiliza yeye, na nyie mnaweza hata kutimuliwa kwenye nyumba yenu…kwa mtaji huo mimi sikubali, katu sitakubalina na hilo,…kama hanitaki mimi atakaaa hivyo hivyo, hadi atakapokufa…na nyie make hapa mlinde mali zenu’akasema huyo mama.

‘Wewe mwanamke,….hukubali nini, unahusika na nini hapa ndani,…kwanza hayo maswala na kunitisha tisha, sitai kuyasikia , maana mimi sitishiki….ndio nakujua tabia zako,na hizo ndizo zinanifanya nisiwe na amani na wewe…una imani za kishirikina , hapo ulipo unafikiria kumloga binti wa watu…nakuambia ukweli, uchawi wako hauwezi kumzuru yoyote…ni ibilisi tu,…’yule mzee akawa anasema kwa sauti.

‘Mimi nimeshasema, wewe utaamua mwenyewe, lakini sitaweza kuona watoto wangu wanaishi na huyo binti, eti ni mama yao, hilo halitakubalika  na nitalipiga vita kwa nguvu zangu zote…’akasema huyo mwanamke.

‘Tutaona, ….’akasema Mzee, na kukatishwa na simu, binti yake akaipokea na kusikiliza na baadaye akasema, akiongea na huyo aliyepiga simu;

‘Lakini iweje mtu atoreke kwenye kituo chenu, hamuoni kuwa kuna udhaifu…..’akatulia na kusikiliza na baadaye akaweka simu na kuwageukia wenzake akasema;

‘Wanasema wakili naye katoroka, na kuna wenzao wengine wameuwawa, wakati wanatoroka, …..’akasema huyo binti.

‘Mnaona, …..ndivyo itakavyokuwa hivyo, watakimbia watauwana, lakini hawatakuwa na amani,….hawawezi kuingilia anga zangu….haki yangu itawaangamiza mmoja baada ya mwingine…’akasema yule mwanamke.

Kukatulia kidogo, na baadaye, yule mzee, akasema;

‘Mbona hawa watu hawaonekani, hebu jaribu kuwapigia simu…..’akasema Mzee, na akina Maua walivyosikia hivyo, wakasogea mbali na mlango, wakawa kama wanatoka nje, na mama yake Maua akasema;

‘Kuna haja kweli ya kuingia humo ndani,…binti yangu, tuondoke hapa kabisa, hii ni familia ya watu,  utajiingiza kwenye matatizo yasiyo na maana kwako,….huyo mwanamke nimeshamfahamu, ukoo wao unaogopewa sana kule kijijini, ..tuondokeni zetu’akasema mama Mua.

Maua akainama kidogo., halafu kweli akaanza kuondoka, mama mdogo akamuwahi na kumshika mkono, akasema;

‘Haondoki mtu hapa mpaka kieleweke, kwanini nyie mnaogopa nini, …mtoto wa majini halogeki, wanaologwa ni wale wanaoamini mambo hayo….mimi siyaamini,..japokuwa nayasikia,….hatuondoki hapa hivi hivi….’akasema.

‘Wewe kama unataka nenda, kaongee nao, sisi tunaondoka…’akasema Maua na wakaondoka na mama yake. Mama mdogo, alisita kidogo na baadaye akawafuata huko nje, huku akilaani, kwa kitendo hicho.

‘Haiwezekani, ina maana ndoto zangu zote zipotee hivi hivi,….hapana, lazima nitafanya jambo,..’akasema na kutoka nje, na huko nje aliwaona wenzake wakielekea getini, kuondoka kabisa kwenye eneo hilo, akawakimbilia na kuwauliza;

‘Sasa mnataka twende wapi?’ akauliza huku wakiwa wameshaingia mitaani , kwenye watu wengi.

‘Tunaenda kumtafuta dakitari aliyekuwa akimtibia huyo mzee’akasema Maua.

‘Wa nini,ni nani anaumwa hapa…na kama ni maswala ya Maua, haumwi, ni mambo ya uja uzito hayo,….au kuna nini kwa huyo dakitari, madakitari mara nyingi hawana pesa..’akasema mama mdogo huku akiwafuatia kwa nyuma.

‘Hatuendi kwake kwa ajili ya kutafuta pesa,…tunahitajia kujua ukweli, je huu uja uzito ni wa nani?’ akasema mama Maua, na kumfanya mama mdogo, awaangalie kwa mashaka na kusema;

‘Hivi nyie, ….manataka kuthibitisha nini…mimba hiyo inajulikana ni ya nani,…na kama alimpa hiyo mimba keshakufa, basi wa kubeba huo mzigo ni mjomba mtu, tunatakiwa tucheze karata vyema, tukizubaa hatutapata kitu hapa…..mimi nawashangaa mnataka kumuona dakitari ili iweje?’ akauliza.

‘Hayo utakuja kuyajua baadaye….maana mdomo wake hauwezi kufungwa,..ni bora uelewe hivyo hivyo…’akasema Maua akawa kama anatabasamu, lakini myoni, alikuwa akiumia kuona binti yake anaishi ya huyo ndugu yake.

‘Tatizo lenu hamuoni mbali, na kwa mtaji huo, mtaendelea kuwa masikini,…na naona nifanye mpango wa kupata pesa nirejee bongo,…’akasema huku akichukua simu yake, na kuanza kupiga namba, na wenzake hawakumsubiri wakaondoka.

*******

‘Dakitari yupo Dar,…kafungua ofisi yake huko, na anakuja kwa dharura tu, je mlikuwa na shida gani nay eye,…?’ akauliza mmoja wa wahaudumu wa hiyo hospitali, ambayo anaimiliki huyo dakitari waliemfuata.

‘Tuna shida kubwa na yeye, ….kama yupo Dar, tutamfuata huko huko,….umesema hiyoo hospitali yake kaifungua sehemu gani?’ akauliza.

‘Maeneo ya Sinza….ukifika hpo ukiuliza jina lake, wanamfahamu sana, kwani ni dakitari bingwa…’akasema huyo mhudumu …

‘Sawa tunashukuru….’akasema Maua na wakaondoka na mama yake, hadi kwenye hoteli wanayoishi.

‘Mwanangu mimi naonatuondoke, twende tukaishi pamoja kijijini..’akasema mama Maua.

‘Mama mimi mpaka nimjua baba wa huyu mtoto, kama Tajiri, alisema yeye sio aliyenipa hii mimba, basi yupo mtu mwingine…..ni lazima nimfahamu’akasema mama Maua.

‘Halafu itasaidia nini…na kama ni mmoja wa walinzi wa Tajiri, maana kama alizidiwa na ulevi, na wewe kutokana na hayo madawa ulikuwa hujitambui, basi lolote liliweza kufanyika….katika wasadizi wake yupo mmoja alifanya hivyo….’akasema mama Maua.

‘Ni lazima nimfahamu……na nitafanya kila aina ya uchunguzi mpaka nimfahamu….swali kubwa, ni kwanini Tajiri akasema tumuone dakitari, je yeye anahusika nini na huu uja uzito….’akajiuliza Maua.

‘Au labda yeye ndiye aliyekupa huo ujauzito..’akasema Mama yake.

‘Haiji akilini, maana siku ile kwa kumbukumbu zangu, sikuweza kumuona, ina maana alikuja baadaye, au ni mmoja wa kundi lao….?’ Akawa anajiuliza.

‘Ingelikuwa mimi ni wewe…nisingelisumbuka kabisa, na kwa vile hata aliyekupa mimba hajulikani, basi, mtoto utamwambia baba yake alikufa,…yamekwisha,…..nani atakuuliza, maana kweli humjui, tatizo na pale unapomfahamu…hutaweza kumficha mtoto…’akasema mama yake.

‘Mbona mimi umenificha, wakati unafahamu fika kuwa baba yangu ni nani?’ akauliza Maua, na hapo akamfanya mama yake atulie, na kujikuta akitingwa na mawazo, akasimama na kutembea hadi kwenye dirisha, akawa anaangalia nje, na kumbukumbu zikaanza kumrejea, siku ile alipoamua kwenda hospitali mwenyewe.

*********

‘Oh,…naona kuna kitu, …..nimeota…..mungu nisamehe, ..ooh, eti nini, hapana..haiwezekani, ina maana ni damu yangu, haiwezekani,..oh, Maua ina maana wewe ni ni….oh, oh, oh, kamuone docta atakuelezea,  ….’ Maneno haya yalimrejea mama Maua, na siku ile ile aliamua kurejea hospitalini, na alipofika akaambiwa kuwa huo mwili ulishahifadhiwa.

‘Docta samhani sana,….nina mashaka kuwa huyo mtu ni ndugu yangu, alipotea kijijini muda mrefu uliopita, naomba niutambue…’akasema.

‘Mbona ndugu zake wameshafika ….’akasema docta kwa mashaka.

‘Waliofika nawafahamu, na watoto wa mjomba wake, …..mimi nilikuwepo wakati anakata roho, akatuagiza jambo, na kauli aliyoiongea inaashiria kuwa ni mmoja wa ndugu zangu…nahitaji nimuone, na kuna alama nikiiona nitajua ni yeye, ….’akasema.

‘Lakini sio utaratibu,….’akasema docta, na hakutaka kubishana na huyo mama akamchukua huyo mama hadi pale ulipohiofadhiwa huo mwili, na kumwangalia huyo mama.

‘Mwili wenyewe ndio huo, ….nikuachie, au unahitaji msaada wangu?’ akauliza.

‘Nomba msaada wako, ..alama hiyo ipo shingoni,…kwenye shingo yake, kuna sehemu aliumia akashonwa…kulibakia kitu kama mstari,  …..’akasema na kabla hajamaliza, yule dakiatari akawa keshamfunua yule maiti.

Mama akamsogelea na kumwangalia vyema usoni…na hisia za kumbukumbu zikaanza kumrejea, japokuwa 
sura ilikuwa imebadilika…lakini akawa anahisi kama ndio huyo mtu anatemfahamu…

‘Hii alama ndio hapa?’ akauliza docta

Mama akasogea na kuiona,…alama ilikuwepo, lakini ilikuwa ndogo sana, sio kama ile aliyokuwa akiifahamu,…hata hivyo alishangaa kujishia mwili ukiishiwa na nguvu, …kitu ambacho kilimjia ghafla,akajikaza na kuinama kuichunguza vyema ile alama, lakini labda kwasababu ya unene, alama ile ilikuwa imefifia..hata hivyo, alijikuta machozi yakianza kumjia machoni, akasema;

‘Oh, inawezekana sio yeye……’akasema huku moyoni akiomba asio ndio yeye, kwani itamuumiza sana, na ni kama mkosi,….

‘Nitashukuru sana akiwa sio yeye, maana ni aibu,…je kama aliwahi kutembea na ….mungu naomba siwe ndio yeye….na kama angelikuwa ndio yeye, wakazaa na binti ….ya..yake..hapaan sio yeye…’akawa anasema kwa sauti ndogo ambayo huyo dakitari hakuwahi kumsikia, na yule dakitari akajua huenda huyo mama alikuwa akimuombea huyo marehemu, akawa anafanya shughuli zake nyingine, na Mama Maua akawa anaondoka, na yule dakitari akasema;

‘Kwani mama wewe ni mwenyeji wa wapi, inaonekana sura yako sio ngeni kwangu?’

‘Natokea Singida…’akasema huku akitamani atoke hapo ndani haraka.

‘Basi nimeshawahi kukuona hata kama sio huko, lakini nimeshawahi kukuona mahali….inaonekana kabisa ninakufahamu….Hata mimi natokea huko huko Singida, hata huyu marehemu namfahamu..’akasema.

‘Unamfahamu…..ooh, unamfahamu vipi?’ akauliza.

‘Marehemu anatokea huko huko kijijini, alikuja huku Mererani, na bahati nzuri, hali ikamnyookea,…na Tajiri akawa Tajiri kweli….na hata jina lake la asili, likasahaulika kabisa..’akasema.

‘Mimi wasiwasi wangu ni hilo jina,..Tajiri, ..mbona majina kama hayo hayopo kule kwetu Singida,….na hata huyo niliyekuambia kuwa ninammfahamu, hata nikamfananisha na huyu hakuwa na jina hilo la Tajiri, ndio maana naona sio yeye…..’akasema mama Maua.

‘Wengi wanabadili majina yao kwasababu zao binafsi….wengine eti wakitafuta nyota ya bahati,kwa ajili ya kupata madini ….’akasema huyo dakitari huku akicheka.

‘Hizo ni imani zao…’akasema Maua.

‘Ni imani tu,…...na hata huyu marehemu aliabadili jina, kwasababu namfahamu kwa jina lake la asili...na hutaamini wenyeji wengi wa hapa hawamfahamu kwa jina lake la asili,…’akasema huyo dakirai na kumfanya mama Maua ageuka na kumwangalia yule dakitari hata ile haraka ya kuondoka ikapungua.

‘Huyu Marehemu alipofika hapa, akawa haonekani onekani…alikuwa mtu wa kujificha ficha, akipambana na polisi, maana alikuwa akishirikiana na binti mmoja matata, waliokuwa karibu naye walimkanya kuwa huyo binti, ni uzuri wa sura tu, lakini kiundani sio mwema, lakini hakusikia.

‘Kuna kipindi alitafutwa sana na polisi, ….na akawa kama kapotea kabisa,… na nalipoonekana tena,akawa kabadilika kabisa, kawa mnene, tofauti na umbo lake, la awali….alikuwa mwembamba sana huyo jamaa….na alikuja kwa jina hilo jipya la Tajiri….akawa anagawa pesa, na kuhakikisha kuwa kila mtu anamuita kwa jina hilo….la Tajiri., likajulikana na likawa ndio jina lake….’akasema huyo dakitari

‘Ina maana hilo sio jina lake hasa la asili…?’ akauliza mama Maua akiwa na moyo wa shauku, hadi akawa kama anajisikia kudondoka.

‘Hapana sio jina lake la asili,…mimi namfahamu sana…..japokuwa kiukweli amebadilika sana, kwa tunaomjua …..tunaweza kumkumbuka, lakini kwa mtu ambaye alionana naye mara moja, hawezi kusema huyu ndiye yule aliyetoka kijijini, akiwa hana mbele wala nyuma….’akasema huyo dakitari.

‘Kwahiyo jina lake la asili anaitwa nani?’ akauliza Mama Maua.

‘Marehemu  jina lake la asili anaitwa Adam….’akasema huyo docta, na mama Maua akaziba mdomo, safari hii hakuweza kuvumilia, akajikuta akilia kwa kwikwi, hadi yule dakitari akashangaa, akamsogelea yule mama na kumliwaza.

‘Pole sana…naona sasa umemfahamu vyema….’akasema

‘Ndio nimemfahamu vyema….’akasema huku akijikaza kutaka kuondoka, na hakuweza kumwangalia yule dakitari tena, akatoka kwa haraka haraka huku akijifuta machozi, hadi kule alipomuacha Maua kwenye hoteli waliyofikia.Na siku hiyo hakutaka kuongea, na hata Maua laipomuuliza mbona amebadilika hivyo, yeye alisema;

‘Mwanangu nina wasiwasi na maisha yako, hali hii inatia wasiwasi, ikizingatia kuwa mimi ndiye mama na baba yako, ……ukumbuke kuwa huna baba, …na kama alikuwepo, hayupo hai tena…’akasema mama Maua.

‘Mama umeshaanza maneno yako…nilishakuambia kuwa mimi simuhitaji huyo baba, ..baba wa nini kwangu, kama hakunitafuta wakati nikiwa mtoto hadi nimefikia umri huu, atanitafuta sasa ili iweje…na hata nikikutana naye, sitakuwa na haja naye tena, ….mungu amepanga iwe hivyo….achana na kumbukumbu hizo…’akasema Maua.

‘Hutaweza kukutana naye tena mwanangu....msahau kabisa….sahau kabisa ujue kuwa wewe hukuwa na baba….’akasema mama yake na Maua akamwangalia mama yake kwa mashaka, alitaka kumuuliza mengi zaidi lakini mama yake mdogo akafika na mazungumzo yao yakakatishwa, na hawakuweza kuliongelea hilo, hadi leo, wakati Maua aliposema;

‘Mbona mimi umenificha, wakati unafahamu fika kuwa baba yangu ni nani?’

‘Maua ni bora usimjue kabisa….huyo aliyeitwa baba yako, kwani ukimjua utaumia sana..naomba usiwe na shauku hiyo…’akasema Mama yake. Maua akahisi kuna jambo,….inaonekana mama yake kagundua kitu ambacho kinahusiana na baba yake, akaona ni lazima akifahamu.

‘Mama kama baba yupo, na unafahamu wapi alipo, naona kwa haya yaliyotokea ni bora nikaonana naye, ili nizitoe hasira zangu kwake, maana kama angelikuwepo, akatimiza wajibu wake kama mzazi huenda haya yaliyonikuta yasingelitokea tena….hata kama mlifukuzwa kijiji, lakini alikuwa akifahamu kakuacha na ujauzito, kwanini asihanganike kukutafuta, ili ajue kama umejifungua mtoto wake yupo wapi, …’akatulia kidogo, halafu kama vile kakumbuka jambo, akasema;

‘Halafu mama, ehee, nimekumbuka,….kama sikosei ulisema baba, au huyo mwanaume alikupa uja uzito wangu,….alikimbilia huku…au sio?’ akauliza na hakusubiri mama yake aseme kitu, akaendelea kusema.

‘Ulisema alikuja kuishi huku Arusha Mererani, ….na leo ulivyobadilika hivyo, nahisi kama umekutana naye, niambie mama ukweli maana hayo mabadilko uliyonionyesha leo, inaashiria kitu…naomba mama unieleze, kama umekutana naye, au kama yupo hapa, ni wapi anaishi, usijali, mimi sitakwenda kumsumbua kabisa….ila nataka tu kujua hilo…’akasema Maua.

‘Mwanangu,…baba yako hayupo hai….nilishakuambia hilo, je unahitaji ukaone kaburi lake?’ akauliza Mama Maua.

‘Kama hilo kaburi lipo, nitafurahia kuliona…na nikiliona moyo wangu utatulia,..na kwa hilo, inabidi niache mambo mengine yote, hadi nilione hilo kaburi, au nimuone huyo baba kama yupo hai,….angalau hata kwa mbali tu….’akasema Maua. Mama Maua alimwangalia binti yake kwa muda, na hakuweza kujizuia, akajikuta  machozi yakianza kumtoka.

*********

NB: Najaribu kukumbuka kitu gani tumesahau, maana ndio tunaishia kwenye kisa chetu hiki.

WAO LA LEO: Unapolima shamba, ukapanda mbegu, utarajie kuwa kuna mmea utaota, na mmea huo ili ukuwe vyema, unahitajia matunzo.

Siku hizi wimbi la watoto wa mitaani linaongezeka, na ajabu kabisa, kuna akina mama wenye mtindio wa ubongo, ….wengine ni wazima, lakini hali zao, kiafya, zimewafanya wawe kama wametengwa na jamii, kuna wasiojiweza kiviuongo, …wamepewa ujauzito, na hata kujifungua, lakini wanaume waliotenda hayo hawaonekani,….

Wewe mwanaume, uliyetenda hivyo, unatumai nini…kama kweli una ubinadamu nenda kamchukue mwanao, hiyo ni damu yako, na utahukumiwa kwa hilo,…nenda kamchukue mtoto wako umlee…kwani ulipopanda mbegu ulitarajia nini?



*********

NB: Najaribu kukumbuka kitu gani tumesahau, maana ndio tunaishia kwenye kisa chetu hiki.

WAO LA LEO: Unapolima shamba, ukapanda mbegu, unatarajia kuwa kuna mmea utaota, na mmea huo ili ukuwe vyema, unahitajia matunzo.
Siku hizi wimbi la watoto wa mitaani linaongezeka, na ajabu kabisa, kuna akina mama wenye mtindio wa ubongo, ….wengine ni wazima, lakini hali zao, kiafya, zimewafanya wawe kama wametengwa na jamii, kuna wasiojiweza kiviuongo, …wamepewa ujauzito, na hata kujifungua, lakini wanaume waliotenda hayo hawaonekani,….
Wewe mwanaume, uliyetenda hivyo, unatumai nini…kama kweli una ubinadamu nenda kamchukue mwanao, hiyo ni damu yako, na utahukumiwa kwa hilo,…nenda kamchukue mtoto wako umlee…kwani ulipopanda mbegu ulitajia nini?


Ni mimi: emu-three

No comments :