Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, March 7, 2013

Uchungu wa Mwana Aujuaye ni Mzazi-68



 Maua akiwa ameduwaa akiwa mwingi wa mawazo, hasa pale alipomuwaza mama yake, akijua sasa mama yake keshaondoka, akahisi upweke fulani, na akiwa hivyo, mara akaingia mtu , mwanzoni alijua ni mama yake aliyekuwa akifunga mlango vyema, lakini akahisi kuwa mlango upo wazo, hakutaka kugeuka mara moja, ….baada ya sekunde kadhaa, akageuza kichwa chake na kuangalia huko mlangoni.

Alipogeuza kichwa chake akiwa anajua kuwa huenda ni mama yake ambaye huenda aliamua kurudi, lakini kumbe siyo mama yake, aliyekuwa kasimama pale mlangoni, huku akiwa kaushikilia mlango, na huku akiwa katizama nje, huko alikotoka, huyu alikuwa sio mwingine, alikuwa ni Tajiri. Maua alibakia akishangaa, mbona huyo mtu badala ya kuingia ndani, amesimama pale mlangoni, halafu anaonekana akishughulishwa na jambo jingine……..

‘Labda amefika na maaskari, …..’akasema Maua, huku akijiweka sawa, akageuza kichwa mara moja na kumwangalia yule mzee ambaye kwa muda huo alikuwa kajiliza kwenye sofa lake, na alionekana kuchoka,…na ingelikuwa vyema, kama angepata nafasi ya kupumzika. Maua akataka kwenda kumwambia Tajiri kuwa mzee hatakiwi kusmbuliwa tena….lakini…

Kabla hajamwambia lolote, yule jamaa akatoka pale mlangoni, na kurudi huko alipotoka, na mlango ukabakiwa wazi, kwani huo mlango ukiushikilia kwa muda, na weneywe hukaa hivhi hivyo kwa muda, na baadaye hujifunga,….Na Maua alipouona upo wazi,  alikwenda hadi pale mlangoni, akaufunga ule mlango, na mara akasikia sauti ya mzee, ikisema.

‘Maua ufunge huo mlango kabisa kwa fungua,….. maana nataka tuongee, nimeota ndoto, na mimi ndoto hunielekeza jambo,…..nisingelipenda mtu kuja kutusumbua kabla sijasema hilo ninalotaka kukuambia,….na hata hivyo, naona muda wa kutumia dawa zangu umefika, kwahiyo kwanza,….sijui tuanze lipi?’ akawa kama anauliza.

‘Dawa zako ni muhimu Mzee…..kwanza jail afya yako….’akasema Maua.

‘Ndio maana nakupenda, na nahisi wewe ndiye chagua halisi la moyo wangu, kwanza nipate hiyo dawa au sio….lakini nikianza na hiyo dawa, itanilewesha na nitashindwa kukuambia hilo ninalotaka kukuambia,…unaona, sasa tuanze lipi?’ akawa kama anauliza.

‘Mimi naona unywe dawa zako, na kwa vile mimi bado nipo, utaniambia tu, hakuna shida mzee wangu…..’akasema Maua. Yule mzee, ambaye alikuwa kavaa fulana nyepesi, na nguo za kulalia…akachukua shuka, akajifunga kiunoni, …..na kuvua ile suruali ya kulalia, huku akisema

‘Samahani sana Maua najua wewe ni dawa yangu, lakini siwezi kupuuza masharti ya dakitari wangu, kweli ni muhimu sana ninywe  hiyo dawa yangu, na pia nahitajika kupumzika…lakini kabla ya hayo yote, nahitajia msaada wako, …..’akasema Huyu mzee, na Maua akamwangalia kwa mashaka.

‘Msaada gani mzee wangu, ….?’ Akauliza Maua huku anamwangalia huyo mzee, akiwa kafunga shuka kiuononi….mzee, huyu alionekana kupungua, kwa muda mfupi, mwili wake, ulikuwa umepungua sana, sio kama alivyoonekana awali.

Yule mzee, alisogea hadi kwenye meza kubwa, akavuta droo zake na kutoa kichupa kidogo, akakifungua na kukinusa, akakitikisa, halafu, akamwangalia Maua.

‘Nahitaji unichue na maji ya uvuguvugu….kama hutojali, ukishamaliza unanipaka haya mafuta…yananisaidia sana…na kwa vile wewe ni dawa ya moyo wangu, najua leo mwili wangu utakuwa na afya tele…usiniogope, ukiwa na mimi uwe huru, na nakuhakikishia kuwa siwezi kufanya jambo lolote baya dhidi yako,….ukiwa hutaki wewe niambie hutaki, au huwezi…siwezi kukushurutisha….’akasema na huku akijiandaa, akavua kile kifulana chepesi, na kubakiwa kifua wazi, ….alionekana kutokujali.

Maua kwanza alisita kuifanya ile kazi, lakini baadaye akaona ni kazi rahisi tu, basi akaenda akachukua maji ya uvuguvugu, akayachanganya na mafuta aliyoelekezwa, akaanza kumchua yule mzee, akiwa amelala kifudufudi, alifanya hivyo, kwenye mikono, mgongoni na miguuni akitumia kitambaa laini ambacho alielekezwa na huyo mzee.

‘Oh, ….kweli wewe unafahamu hii kazi, nahisi mwili wote ukiwa na nguvu,…..nakuhitajia sana Maua katika maisha yangu,…nakuomba sana, unikubalie ombi langu la mwanzo, kuwa wewe uwe mke wangu, usijali umri….japokuwa ndoto….kuna njozi, ilinijia ….sijui ina maana gani, lakini usijali….’akasema huku akijituliza kwenye sofa lake, ilionyesha dhahiri kuwa dawa zimeshaanza kufanya kazi yake na macho yake yalikuwa yakiishiwa nguvu, kama mtu analiyeweshwa madawa ya kulevya.

‘Mzee wangu achana na mawazo hayo…mimi ni sawa na mjukuu wako, hata hivyo kuna mengi ya kuongea, ambayo ni muhimu sana kwangu, lakini kwa sasa nakuomba wewe upumzike, ukiamuka najua tutaongea kwa marefeu na mapana……’kabla hajamaliza mlango ukagongwa.

‘Nani huyo tena, …?’ akauliza huyo mzee kwa sauti, na alipoona kupo kimiya akamgeukia Maua na kusema;

‘Hakikisha kwa yoyote atakayekuja, hanisumbui, ….wengi wanajua nimeshakufa, waambie hivyo hivyo, kuwa mzee keshakufa,…au hajazindukana, na huenda hayupo hai’akasema huyo mzee.

‘Eti nini….kwanini niwaambie umeshakufa wakati bado upo hai?’ akauliza Maua.

‘Kama nilivyokuambia…waambie nimeshakua, ni bora kwao…..’Yule mzee akawa anaongea kama anaweweseka, kuonyesha yupo usingizini…Maua alitulia kwa muda, ….na alipoona huyo mzee, katulia, kuonyesha kuwa keshalala, …..akatafuta shuka kubwa jeupe, kwenye kabati, akaja akamfunika vyema, akiacha sehemu ndogo tu ya usoni ya kutolea hewa,…ili kumfanya yoyote atakeyekuja asimuone vyema,

‘Hapo anaonekana kama kafa kweli….’akasema Maua huku akitabasamu

*******
Tajiri aliharakisha ili amfikie yule mwanamke , lakini alishachelewa, kwani yule mwanamke alipotoka nje, aliingia kwenye boda boda, na ile boda boda ikaondoka, nay eye akabakia na kitendawili kichwani, ambacho hakuweza kukutegua.

‘Huyu mwanamke ni nani..hii sura kama naifahamu, sio yeye huyu kweli, lakini sio yeye….hapana, labda awe ni mama yake, ….haiwezekani awe amechakaaa  kiasi hiki..haiwezekani,….’akawa anaongea peke yake akiwa anasindikiza ile boda boda kwa macho ambayo ilikuwa inakwenda kwa kasi.

Alipoona hana la kufanya, akarudi ndani, na kuelekea kwenye mlango wa chumba ambacho mjomba wake yupo, hakujua ni nani mwingine yupo humo ndani, kwani alipofika mara ile ya kwanza, hakuchungulia ndani, ila alihisi kama kuna mtu ndani..

‘Huyo anaweza akawa ni dakitari….’akajisemea moyoni, huku akifungua kitasa cha mlango, na akakuta mlango umefungwa.

‘Ni nani tena kaufunga huu mlango…?’ akauliza na akageuka huku na kule kuwaangalia wafanyakazi wa humo ndani, lakini wafanyakazi  hawakuwepo hapo karibu, walikuwa nje, …akatoka nje, na huko akakutana na mama mdogo.

‘Heee,..mama kumbe upo hapa,…. nilijua mpo hotelini kwenu….upo na Maua?’ akauliza.

‘Hujamuona huko ndani,…Heheheee, Maua, anamuenzi mzee, maana mzee keshazimia kwa dogo dogo, nakuambia ukweli, bosi sasa ukizubaa, mzee anachukua ngoma ,…na hata mimi naona iwe hivyo, kwa hivi sasa hatutajali kuwa ana mimba yako’akasema huyo mama.

‘Acha utani wako, mzee yupi anachukua ngoma?’ akauliza.

‘Kuna wazee wangapi humo ndani, …?’ Mama mdogo akauliza swali huku akimwangalia Tajiri kwa makini, na Tajiri, akawa kama hamsikilizi, ….yeye akageuka kurudi ndani, akijua kuwa huenda aliyekuwepo huko ndani ni huyo mzee anayemuongela mama mdogo, na yupo na Maua, kwani asingelikuwa na ujasiri kwa ukaa na maiti, au huenda mwili wa mjomba wake umeshachukuliwa, ….

‘Kwahiyo una maana Maua yupo huko ndani….na ….huyo mzee?’ Akauliza Tajiri.

‘Ndio maana yake, …..nakuambia mzee haambiwi kitu ….na Maua naye ..oh, tatizo lake bado mdogo, ningelikuwa mimi…ooho…nisingeliipoteza hiyo bahati…’akasema huku akitabasamu, na alipomwangalia Tajiri, akainama chini na kusema;

‘Ndio Maua yupo huko ndani, anamuenzi mzee, siunajua tena mapenzi ya wazee, wazee wanajua jinsi ya kulea watoto wadogo,….wewe zubaa tu, ..nikuambie kitu bosi wangu, ukitaka niweke mambo sawa, ongeza dau,…nipe mshiko wa nguvu,..la sivyo,…mzee anamchkua binti kilaini’akasema mama mdogo.

‘Wewe mama wewe, acha tamaa, ina maana pesa zote ninazokupa hujarizika,….hivi wewe una akili kweli..hayo unayoongea yanatoka akilini mwako, au ni tamaa ya pesa ndio inakutuma iwe hivyo…..ngoja nikaonane na huyo mzee wako…’ akasema Tajiri huku akiwa anatembea kuelekea huko ndani.

‘Nikuambia ukweli ….bosiiii, mwenye kisu kikali ndiye atakayekula nyama….haheee’akasema huyo mama mdogo huku akicheka utafikiri yupo nyumbani kwake.

Tajiri moyoni alishaanza kuhisi kitu kama wivu, lakini hakuwa akimuamini sana huyo mama, lakini moyoni mwake, alitaka kumuona huyo anayeitwa `mzee’ ni nani, au ni yule dakitari,… ni mzee gani huyo anayetaka kumchukua Maua, hapo akahisi kuna jambo, na ili apate ufumbuzi wake, ni lazima aingie ndani kwa haraka.

Akafika pale kwenye chumba na alipofungua kitasa , mlango ukawa haufunguki, ina maana umefungwa kwa ndani, Tajiri, akahisi joto likiogezeka, wivu ukazidi kumpanda, ….akagonga, kimiya….akatoka hadi sehemu wanapoweka fungua za akiba. Huwa kuna sehemu wanaweka ufunguo za akiba, ili kama kuna dharura, huenda mzee kazidiwa ndani, wanazitumia hizo funguo.

Aliporudi, na kufungua mlango, ukafunguka bila hata kutumia ufungu, akaingia ndani moja kwa moja, na akahisi maji yakimwagika huko bafuni,  akajua kuna mtu anakoga, akasogea kidogo pale alaipolala mzee wake…..’ na simu yake ya mkononi ikaita.

Ilikuwa ni simu kutoka kituo cha polisi, na aliambiwa kuwa Malikia anataka kuongea na yeye, na ni muhimu sana, ikabidi asogee pembeni na kuanza kumsikiliza Malikia;

‘Haya sema…’akaongea akiwa hana shauku ya kumsikiliza.

‘Sikiliza wewe mwanaume, ….usipofanya mpango wa kunitoa humu ndani, nitahakikisha kuwa na wewe unaingia humu, na ujue ninajua mambo yako mengi….ukumbuke tulikuwa pamoja katika mpango wa kumuua huyo mzee, na mambo mengine mengi nilikuwa nikishirikiana na wewe…na mzee…kwahiyo fanya ufanyalo kesho nitoke humu ndani….kwani nisipotoka , kila mtu kwenye familia ya mzee atajua hilo, kuwa mimi na wewe tulikuwa na mango mmoja wa kumuua huyo mzee….’akasema Malikia.

‘Nitajitahidi, lakini polisi wamesema haitawezekana’akasema Tajiri huku akikunja uso kwa hasira

‘Kwanini haiwezekani,…hakuna kisichowezekana kukiwa na pesa, tumia pesa, usiwe bahili, nenda na mshiko wa nguvu, kaonane na mkuu wakituo,….kwani pesa zako, tumia pesa za mzee….kwanza yule mkuu wa kituo  ni mtu wangu….mnoko ni huyo jamaa aliyekuja ambaye nasikia atakuwa ndiye mkuu wa kituo….’akasema Malikia kwa haraka haraka.

‘Hata hivyo…..muda kama huu….’akaanza kulalamika Tajiri

‘Nakuambia ukweli….nenda kaonane na huyo mkuu sasa hivi….unanisikia lakini….ukumbuke, nina mambo yako mengi, mabaya yako mengi…, ambayo familia ya huyo mzee, wakiyaona, watahakikisha unakwenda jela, au unakufa, na hutaweza kurithi chochote kwenye hiyo familia,….nilitaka kumuonyesha mzee wako siku mbili zilizopita baada ya kusikia kuwa unataka kunisaliti, lakini, nikaona haina haja,…muda wake utafika tu, na….kama usiponitoa hapa,…hilo litafanyika…..’akasema Malikia.

‘Malikia sio kwamba sitaki kufanya hilo unalosema, ….nimeshafanya, nimekwenda kuonana na mkuu wa kituo, nilipotoka hapo tu, nikamfuata….lakini ndiye huyo huyo aliyesema kuwa dhamana , haiwezekani….lakini nitajaribu kwenda kumuona tena’akasema huku akiwa na wasiwasi, kwani anavyomjau Malikia, …ni lazima anaweza kufanya lolote kama akiona hana njia nyingine, …..na anajua kuwa malikia ana mambo yake mengi ya siri na akiyaweka hadharani …ataumbuka, na asingelipenda kurudia ule umasikini……

‘Nispofanya jitihada za kumtoa huyu mwanamke…ataniumbua,…..na nitakosa kila kitu, …haiwezekani,…ni lazima nimtoe humo ndani kwa njia yoyote ile…..’akawa anawaza akilini.

‘Na sikiliza, najua sasa hivi upo na huyo Malaya…nakuambia ukweli, kama unataka kuumbuka, endelea kuwa naye…sikiliza wewe mwanaume, achana na huyo mshamba, malaya wa mitaani, unataak nini kwake, ….kama utaendelea kuwa naye ujue huyo huyo ndiyee atayakutia hatiani, ….hujiulizi kwanini haya yataokee hivi sasa alipoonakena huyo kinyamkera wako,….hakikisha wanaondoka hapa Arusha haraka iwezekanavyo, hawo ni mashushu…wametumwa toka Dar, kuja kukuchunguza’akasema Malikia.

‘Hawo usiwajali..hawana shida,….na wala sio mashushu kama unavyofikiria wewe, hawo wamekuja na mambo yao mengine,….ambayo hayakuhusu…’akasema Tajiri

‘Hawana shida eeh ndivyo unavyojidanganya, ngoja nitoke humu…na nikitoka tu, nitahakikisha narudi humu, nikiwa najua hakuna kiumbe ambacho kitafungua mdomo mahakamani, nakuhakikishia nitatoka humu bila hata msaada wako,…..hilo naapa, kama una mapenzi na huyo Malaya wako, na wengineo, hakikisha wanauhama huu mji…kabla sijatoka’akasema Malikia na simu ikakatika.


Tajiri,…. alipogeuka, akamkuta Maua keshatoka bafuni, na alikuwa akifuta maji kichwani huku akionyesha kuwa alikuwa akisikiliza hicho walichokuwa wakiongea na Malikia…., akamwangalia kwa makini, na Maua akawa anaendelea kufuta maji kichwani huku anatabasamu, Tajiri akageuza kichwa kuangalia kule alipolala mzee wake, halafu akageuka kumwangalia Maua.

`Maua ulikuwa na nani humu ndani?’ akauliza Tajiri kwa hasira

‘Nailikuwa na nani humu ndani….mbona sikuelewi, walikuwepo wengi kabla hujafika, na…alikuwepo docta, alikuwepo mama….una maana gani kuuliza hivyo?’ akauliza Maua huku akionyesha uso wa kushangaa.

‘Oh, hamna shida, lakini mmmh, Maua ..una ujasiri gani wa kukaa humu ndani,…na huyo docta yupo wapi, mbona, hajauchukua huu mwili….na nimesikia kuna mzee anataka kukuchukua,…ndio huyo docta au ni mzee gani huyo?’ akauliza Tajiri, akihisi wivu ukimtinga akilini.

‘Mwili gani huo, mbona sikuelewi,….na unasema kuna mzee anataka kunichukua, kunipeleka wapi….mbona uanongea mambo mengi nisiyoyaelewa, upo sawa kweli?’ akauliza Maua.

‘Mwili gani,…..!’ akasema kwa mshangao, huku akigeuka kuangalia kule alipolala yule mzee, hakupenda kumwangalia sana, maana akilini mwake, alikuwa kama anajuta, anahisi kama anahusika katika kumwangamiza mjomba wake, akasema

‘Si huu mwili wa mzee, ukiendelea kubakia hapa huoni kama utaharibika, sitaki mzee wangu afanyiwe hivi, ana stahili haki zote, na mimi ndiye mtoto wake niliyekaribu naye,….’akasema huku akiangalia kule alipolala mzee wake kwa muda, halafu akageuka kumwangalia Maua.

‘Tajiri, ina maana na wewe ulikuwa katika mpango, wa kuhakikisha kuwa mzee wako, mjomba wako anayekujali anakufa, na …huna hata haya…ya kusema hayo unayoyasema…una uhakika gani na hilo unalolisema…!’akawa anataka kuongea, lakinia akasita.

‘Mimi sikuwa kufikiria hivyo,….hata siku moja, eti nimue mzee, mjomba wangu, halo halipo kwangu, na sikuwepo katika mpango huo, na sitaweza kufanya hivyo kamwe, japokuwa yule mwanamke, alikuwa akinishawishi nifanye hivyo….’akasema huku akionyeshea mkono kwa kupinga hilo, akawa anatembea huku na kule, kama aliyechanganyikiwa.

‘Usipige kelele….’akasema Maua, alipoona huyo jamaa anaongea kwa jaziba huku akiwa kazifunga nwele zake kwa juu.

‘Nakuambia ukweli, huyo mwanamke….atakona cha mtemwa kuni….unaona sasa, sasa hivi anakiona cha mtema kuni….hata hivyo, inabidi nitajihiidi huyo mwanamke apate dhamana, maana, hata kama mzee angelikuwepo angelifanya hivyo, kwani alikuwa mtu wake wa karibu….na kashikilia mpini’ Akasema Tajiri.

‘Hivi wewe bado unamwamini huyo mwanamke wako, mtu aliyetaka kumuua mjomba wako…hebu fikiria hayo aliyomfanyia mzee wako, …huoni ilivyotokea, kwani kwanini mzee alifikia kuwa katika hiyo hali mbaya…si ulikuwepo kipindi ambacho mjomba wako, alifikia hatua hiyo mbaya..nakuuliza si ulikuwepo?’ akauliza na kabla Tajiri hajasema kitu,Maua  akasema kwa sauti ndogo, akiogopa kumsumbua huyo mzee

‘Na…ni nani aliyesababisha yote hayo…..? Na ni nani aliyeweka sumu…., ili mjomba wako afe..na bado upo nyuma ya huyo mtu, kwa namna hiyo, kila mtu atakushuku, kuwa na wewe unashirikiana na huko mwanamke…!’akasema Maua.

‘Usiseme hivyo Maua,..hujui mambo haya yalivyo, adui yako, …anaweza akawa msaada mkubwa katika kufanikisha mambo haya ya kibishara, na …pia huyo mwanamke ana siri kubwa sana za mzee,…..na mimi, tusiposhirikiana naye…ooh, siwezi kukuambia zaidi maana mambo mengine ni ya siri’akasema Tajiri.

‘Mambo gani hayo ya siri, ya kuuana..wewe umeshajua kuwa huyo ni adui wa mzee wako, na lengo lake ni kuhakikisha huo mzee, anakufa nay eye, aanrithi mali yake,  au sio?’ akauliza Maua.

‘Hayo maswali ya polisi,…..au na wewe ni shushu wao nini, maana unavyouliza, nakuona kama polisi,…’akasema Tajiri.

‘Kwani hata nikiwa polisi wewe una wasiwasi gani, kama huhusiki, ….au unahusika ndio maana una kuwa na wasiwasi?’ akauliza Maua.

‘Sikiliza, hata kama wewe ni shushu, mimi sihusiki, unasikia….na kumbuka safari yetu ya kuja huku, ….na kama unaingiza mambo mengine, ni bora mrudi huko Dar, nitakuja huko tutayamaliza huko huko…’akasema Tajiri.

‘Mimi siondoki hapa hadi hapo, nitakapojua ni nini majaliwa yangu, umeshaniharibia maisha yangu, ….na sijui mama yangu atakuwa katika hali gani kwa sasa….nahitaji kujua majaliwa yangu haraka iwezekanavyo’akasema Maua, na alipotaja neno mama ndipo Tajiri akakumbuka…

‘Umenikumbusha kitu, …wakati naingia humu, alitoka mama mmoja, …..akiwa na haraka, ni nani huyo?’ akauliza huku moyoni akiwa anamwangalia Maua, ambaye kwa muda huo, alikuwa bado kafungwa nguo alilotoka nalo bafuni, ....akawa anaumia kimoyo moyo, .....

‘Mama mmoja, una maana mama yangu?’ akauliza Maua.

‘Hapana sio mama yako, …kuna mwanamke, alitoka humu,….mimi siongelei mama yako, mama yako namfahamu sana,…..huyo mpenda pesa,…achana naye, maana kila mara ukikutana naye, anadai pesa, pesa zitamuua…na mara anadai upo na mzee, kama ningelimkuta humu ndani….ungelianiambia vyema….ole wake’akasema huku akiangalia huku na kule..

‘Mimi simjui huyo mwanamke mwingine unayemzungumiza…na hata kama ungelimkuta huyo mzee unayemzungumzia, sijui mzee gani, ungenifanya nini, kwani tuna makubaliano gani mimi na wewe….makubaliano yetu ni hayahusiani na lolote ….zaidi ya kuwajibika basi….’akasema Maua huku akijiandaa kuondoka.

‘Sasa unataka kwenda wapi?’ akauliza Tajiri.

‘Kwani hapa ni kwangu hadi nikae humu, nakwenda huko tulipopanga,….na kesho tunahitajia kujua maswala yetu haya …na nataka tuyaongee mbele ya mzee wako, maana naona hapa mnataka kunichnaganya kic’ahwa changu, nyote akili zenu ni sawa…’akasema huku akiangalia kule alipolala huyo mzee.

‘Hayo mengine tuliyotoka nayo Dar, kwa sasa yasitisheni,…..mpaka haya matatizo yaliyotokea hapa yaishe, ….itakuwa jambo la ajabu, kama nitakimbilia maswala hayo …..wakati kuna msiba’akasema.

‘Msiba wa nani tena, hivi wewe unaongea nini, mboan sikuelewi?’ akauliza Maua kwa mshangao.
Tajiri akageuka kuangalia pale alipolala mzee wake, na akahisi kitu tofauti, kwani alipofika anakumbuka kuwa yule mzee, alikuwa kalala kaangalia juu, lakini sasa hivi anaona ajabu yule mzee kalala upande upande….

‘Haiwezakani….ni nani kamgeuza mzee?’ akauliza.

‘Wewe mbona hueleweki?’ akauliza Maua akiwa kwenye mshangao.

Tajiri, hakutaka kuongea zaidi, akaenda hadi pale alipolala mzee wake, akamchungulia na baadaye akainamisha kichwa na kumsikilizia,…..akainuka haraka, kama vile mtu anaruka, kama vile mtu aliyeshitulia na kitu cha kuogofya….

‘Ina maana mzee….’akasema kwa mshangao, na akasikia sauti ikisema.

‘Hebu toka nje, nahitajika kupumzika….na ole wako utoe dhamana kwa huyo hawara wako…na nakuonya kama wewe una husika kwa lolote lile na huyo mwanamke wako, ….nitahakikisha huna haki yoyote kwangu….utamfuata huyo mwanamke wako jela…..’ilikuwa sauti ya mzee, iliyomfanya Tajiri ashikwe na bumbuwazi, akabakia ameduwaa, aliogopa hata kuangalia wapi sauti ilipotokea, akasimama kwa muda bila kusema kitu, …..

NB Mvua imeleta mengi…shida za usafiri, mtandao shida….ooh, lakini hicho kidogo kwa leo kinatosha.

WAZO LA LEO: Tusipende kuombeana mabaya, tusipende kujenga husuda na chuki, hasa pale tunapoona mtu fulani kafanikiwa, …cha muhimu ni kujitahidi, kufanya kazi kwa bidii, huku tukimuomba mungu, kuwa na wewe uwe kama yeye, upate kama yeye, kihali….tukumbuke kuwa aliyempa yeye, ndio huyo huyo anayeweza kukupa hata wewe.


Ni mimi: emu-three

No comments :