Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, January 21, 2013

Uchungu wa mwana Aujuaye ni Mzazi-50




‘Hodi hapa, ….hodi hodi kwa bibi harusi, ….chereko cherako.....’sauti ya kilevi ikasikika kwa nje, na mama Maua akachungulia kupitia kitundu kidogo kilichopo hapo mlangoni. Alijua kuwa ni mumewe, lakini likuwa kahisi kuwa hayupo peke yake, atakuwa na huyo rafiki yake mpya ambaye  eti ndiye mshenga kwa ajili ya kuozeshwa binti yake.

Aliwaona kweli mumewe na huyo mshenga, lakini pia walikuwepo watu wengine wawili, ambao hakuweza kuwatmbua kwani kitundu kile hakikuweza kuwaona vyema. Akajifunga khanga yake vizuri, akijua kunaweza kukatokea mtafaruku, kwahiyo inabidi ajifunge kibwebwe, akafungua mlango.

‘Weewe mwanamke kwanini nagonga mlango muda wote huo hutaki kufungua…?’ huyo mwanaume akatoa sauti ya kilevi huku akiyumba, na rafiki yake akijitahidi kumshikilia ili asianguke.

‘Usinishike..unafikiri mimi nimelewa sana siwezi kusimama kwa miguu yangu mwenyewe….mimi ni ngangari, nimeanza kunywa pombe nikiwa na miaka miwili…sitetereki na hivi vijipombe….kwanza….ehe, nikutambulishe mke wangu…’akasema huku akimsogelea mkewe pale aliposimama, na alipomkaribia akteelza na kuanguka.

Wenzake walijitahidi kujizua kuchake na mmojawapo ambaye mama Maua alishamtambua kuwa ndiye huyo anayetaka kumuoa binti yake, akamsogelea huyo mwanaume kutaka kumsaidia..

‘Oooh, pole sana mzee…’akasema huyo jamaa, akionyesha adabu.

‘Mimi sio mzee bwana, wewe kuanzia sasa niite baba mkwe…..au sio..hahaha…wewe kweli unaweza kuishi na watu kama sisi,…huyu binti wangu ni kimataifa watu wengi wananisifia kuwa nina binti mrembo..kama mama yake, japokuwa mama yake kachooooka, kajichokea, …kila siku kuumwa. Yaani haoa mimi ni docta,…fulu, kuuguza mwanamke..’akawa anainuka kwa kushikilia ukuta.

‘Mzee naona tukae , maana muda unakwenda, na sisi hatuna muda mrefu kama nilivyokuelezea kuwa nina mazigo wangu nataka kuufuatilia huko Dar, bandarini..’akasema huyo muoaji.

‘Hilo nalo neno..kweli nisamehe mwanangu..maana wewe sasa nakuita mwanangu japokuwa huenda kiumri tumelingana..hahaha, huwezi kuona ndani hapa, mimi nina miaka karibu hamsini na nne,…sasa wewe san asana una miaka thelathini….na tano, sita, ukizidi sana arubaini’akasem huku akichezesha vidole.

‘Arubaini mzee…’akasema huyo mtu.

‘Aaah, unaona, halau unaoa msichana mbichi, hata kumi nanane bado,m utafungwa wewe….lakini usijali, kasichana kangu hako kameshavunja ungo..na kanafaa, kazuri…na huo mwili, kama wale warimwende kwenye runinga’akawa anageuza uso kumwangalia mama Maua.
Mama Maua alikuwa kasimama huku akiwa kaangalia pembeni, akijua kuwa leo inawezekana kukawa hakukaliki, ….

‘Jamani wageni karibuni ndani, …maana mkimuendekeza huyu mtu mtasimama hapo mpaka mtachoka..’akasema mama Maua huku akifungua mlango kwa mapana, na wote wakaingia ndani.

‘Mke wangu….ooh, nisamehe, inabidi nikuite hivyo kama watu wanavyotaka iwe hivyo, japokuwa mimi na wewe ni kama miti miwili iliyopo kwenye shamba moja, haigusani, lakini ni …kama mtu na ….na…’akacheka.

‘Msinione nacheka, inauma, hebu fikiria, huyu mwanamke nimekaa naye toka lini….tangu akiwa ananyonyesha hadi leo,..lakini ..mmh, kila siku kuumwa, ..hasa usiku, basi mimi kwa vile nina mpenzi wangu mahabubu, sijali, nikashampata huyo, sina shida, nikirudi mimi na mpenzi wangu, kitandani, kuamuka ni majogoo….shauri lake,..aumwe weeee, akifa tutazika’akasema huku akijiegemeza vyema kwenye kochi.

‘Ina maana rafiki yangu huyu mwanamke sio mkeo?’ akauliza yule mshenga.

‘Nani kasema sio mke wangu, halafu huyo mtoto nilimpataje, wee, funga domo lako, usinikoseshe mahari…’akainua kichwa na kuwaangalia wale wanaume wawili, yaani anayetka kuoa na mwenzake.

‘Kwanza nakudai bei gani, maana maharii tulikubaliana ni milioni hizi…’akawa anaonyesha kwa kidole, vidole viwili,…

‘Mzee hayo tumeshaongea, tatizo lako,….hapo ulipo sijui kama unajua nini unachoongea,..akini yupo mshenga, tusiandikiane na mate, mshanga hebu weka mambo hadharani’akasema muoaji, huku akitoa mabulungutu ya pesa, na yule mzee mlevi akainuka kidogi kuteke kusogelea huku akijialamba lamba.

‘Mama mkwe, hizi hapa ni za kwako, ….maana mumeo kila nikimpa pesa,a ainsihai kulewa, sasa ni zamu yako kupokea sehemu ya mhari, kama tulivyoongea siku ile, kuwa mimi sina lengo baya, nia na lengo langu ni kuhakikisha naishi na binti yenu kama mke na mume, nataka nitulia, niishi kwa raha na mke wangu….’akasema huku akiinuka kumkabidhi huyo mama pesa.

Mama Maua aliziangalia zile pesa, bila kupokea, na mumewe alipoona hivyo, akainuka kutaka kuzichukua, lakini yule mtu akaondoa mkono, na kwa haraka akazishkisha kwenye mkono wa mama Maua.

‘Hebu acha uroho,….hizi nilishakuambi ni kwa ajili ya mama mkwe, ili ainue mtaji wake..yeye anahangaika na vitumbua, kwanini sifungue genge kubwa, mkaweza kujiendeleza, hivi utaendelea kuishi maiaha kama hayo hadi lini..utakopa, mpaka utakopwa na wewe….’akasema mshenga wake.

‘Wewe umeanza unataka kuingilia maisha yangu, hivi unafikiri mimi sina pesa, uliza mitaa ile ya akribu na msitu, watu wananitambua mimi, kama fza lao, pedeshee, wa kinywaji, tena sio kinywaji kama hiho mlichokunywa….’akaangalia nje kama vile anaogopa.

‘Ngoja wenyewe wasikie kama hutaenda kunyea kopo’akasema yule jamaa mwingine ambaye muda mwingi alikuwa kimiya.

‘Nani anyee kopo, unafikiri mimi nimezaliwa leo..acha utani wako wewe, nilijua kuwa wewe ni mtu wa busara, kumbe ni sawa na huyu kidowezi hapa, eti anajiita mshenga,…’akasema huku akimkonyesha huyo rafiki yake.

‘Kama mimi sio mshenga ni nani basi, …..mwenzako kanituma kwako kuwa kaona ndege mrembo akiambaa hewani na mara akamuona akitua hapa, akataka kujua kuwa kiota chake kipo hapa….akagundua kuwa kipo hapa, akaona aah, kwanini nisimchukue huyo ndege nikaishi naye kwenye mali yangu, tule mali sote….’akatulia.

‘Acha hiyo, hata ushenga huujui, ....ina maana sisi tunaishi kwenye kiota, hiyo ni zarau, na zarau kama hiyo inahitajika kutoa kafara,..bila elifu ishirini, sijakubali….’akageuka kususa.

Yule muaji akatoa elifu ishirini na kuziweka mbele ya meza karibu na yule mzee, na yule mzee alipoziona kwa haraka akazichukua, na kusema;

‘Hapo sasa tuongee, …..kwanza huyo binti yupo wapi, bado anajiremba tu?’ akageuka kumwangali mkewe.

‘Katoka…..’akasema mama Maua.

‘Katoka, kaenda wapi, nilikuambia nini wakati naondoka asubuhi?’ akasimama. Na yule anayeitwa mshenga alipoona hivyo, akasimama na kumshika huyo mwanaume na kumkalisha chini.

‘Hebu tulia, umeambiwa katoka, sasa hasira za nini, mbona nyie watu hamjui kuishi na wanawake,….’akasema huyo mshenga.

‘Mama sisi kama inavyotuona tumekuja na kwa lengo moja, ..na lengo limeshajieleza, japokuwa sio kwa utaratibu mzuri…maana kuna taratibu zake, lakini mwenzetu huyu kama unavyomjua, akiwa hivi kila kitu kwake sawa….sisi tumekunywa, lakini unatuona, hatuonyeshi kabisa kuwa tumelewa,….ila mwenzetu kazidi..’akasema mshenga.

‘Ongea, maliza kila kitu…’akasema huyo mwanaume huku kajishika kama kujikumbatia kifuani.

‘Mama nia yetu ni njema, ..huyo hapo ndiye anayetaka kumhukua binti yenu, kijumla…na kwa makubaliano, leo,…..leo hii, kama tulivyokubaliana na….’akageuka kumwangalia huyo mwanaume akiwa kageukia dirishani.

‘Tunatakiwa kuondoka na huyo binti, na harudi, itafanyika wiki ijayo…lakini kwa vile mwenzeti ni mtu wa masafari, anahitaji huyo binti akakae kwake, ili kulinda mali,..kwasababu hakuna cha zaidi , kama ni mahari keshalipa zaidi na zaidi….’akasema mshenga.

Mama akawa kakunja uso, akaziangalia zile pesa pale mkononi, akainuka na taratibu akaenda pale alipokaa yule ambaye anataka kumuoa binti yake, na akasema;

‘Ndugu ….nasita hata kukuita mwanangu, maana kiumri umenizidi….lakini kwa ajili ya haya yote, inabidi nikuite hivyo..mwanangu….kama hii pesa ni kwa ajili ya hicho mnachokiita mahari, naomba uichukue, na pili, hayo makubaliani ya kumchukua binti yangu yametoka wapi….’akaziweka zile pesa kwenye mapaja ya yule mwanaume…

‘Mama usifanye hivyo, hizi ni kwa jaili yako, wewe ni mama yangu, kuanzia siku ile, nilipokuja hapa,….hizi chukua tu, sio sehemu ya mahari…’akasimama na kwenda kuziweka mikononi mwa yule mama. Mama Maua akawa kazishika nusu,, huku zikitaka kumdondoka….

‘Kama hazitaki nipeni mimi…..’akasema huyu mwanaume, akitaka kusimama kwenda kuzichukua na mama Maua alipoona hivyo, akazishika vyema zile pesa na kuangalia chini.

‘Mwanangu sio bizaa, ya kunadiwa,  kwa pesa….na sijawahi kukaa na nyie tukakubaliana hilo, kuwa mwanangu anatakiwa kuolewa, ba baya zaidi hili la kusema kuwa eti mumekubaliana kumchukuliwa…sikubaliani nalo, na kama ni pesa zenu, mimi sizitaki niacheni nife na umasikini wangu, muacheni mwanangu, hamjuii mateso gani niliyoyapata hadi akapatikana, uchungu wa mwana aujuaye ni mzazi…’akasema na kuinuka.

Watu mle nadni wakabakia kimiya na yule mshenga akamshika yule mwanaume mlevi kweny bega, na kumtikisa, kwani alikuwa kama kalala;

‘Vipi mwenzetu, kumbe haya mambo ulikuwa ukiyafanya kitemi,….hukumshirikisha mkeo, sasa tuambie kulikoni….maana sisi tuekuja kuchukue chetu, mara hili linazuka, …na huyo binti yupo wapi, ili tuwe na uhakika …..’akasema mshenga na yule muoaji akatikisa kukubaliana na hiyo hoja.

‘We….mwanamke, Maua yupo wapi?’ akauliza, wakati huo mama Maua keshaondoka, yupo nje.

‘Nimekuambieni kaondoka, na sijui wapi alipokwenda…’akasema.

‘Eti nini…hujui wapi walipokwenda,….ohoooo, naona unatikisa pombe zangu,…umeshanisahau, unajua, mimi sipendii ugomvi, lakini….lak---ini, watu wananitafuta, hebu niambieni, kwa mtaji huu mnataka nifanye nini,…..nikae kimiya,…hebu niambieni, nataka muone vumbi langu…’akainuka na kutaka kutoka nje.

Yule mshenga akamuwahi na kumshikilia, lakini hakukubali , ikaw apurukushani, hado wote wakaanguka chini. Wale jamaa wawili walikuwa wamekaa wametulia kimiya, hawakusimama kusaidia. Baadaye yule muoaji, akasema kwa sauti chini chini;

‘Hebu tuambie, …huyo Maua uliwahi kuongea naye akakubali, au na yeye umetumia ubabe kama huu, maana uliniambia kuwa mumekubaliana, hakuna shida, au ulifanya hivyo ili upate pesa zangu, …naona hapa hatutaelewana kwa hilo, kama lengo lako lilikuwa kunichuna, sasa mimi nitakuonyesha kuwa sitanii, nitakuhuna ngozi yako kiukweli…..’akasema yule jamaa huku akitabasamu, kama vile anatania.

Yule rafiki yake ambaye anamjulia, akamshika begani, na halafu akasimama, na kutoka nje, ….huko nje akakutana na yule mama akiwa kaka chini huku kainama,na kushikilia kichwa,….akasimama karibu yake bila kusema neno kwa muda,…halafu akakohoa

‘Nimewaambia kuwa mwanangu sio kitu cha kuuza, hamunielewi,…jamani hivi kuwa masikini ndio kuwa huna maana, unaweza ukandaiwa kama chombo tu,….hata hiyo haiwezekani,najua sisi hatuna thamani mbele ya nyie mliojaliwa, na mnaweza kufanya lolote muwezalo, sio shida, fanyeni mnalotaka, lakini …mungu yupo’akasema yule mama na kuinua mikono juu.

‘Mama sikiliza, sisi hatkuja kwa nia mbaya, mumeo alituambai kuwa mumeshakubaliana, hakuna tatizo, na hili la kutuambia kuwa mwanao sio chombo, tunashangaa….mumeo kachukua pesa nyingi sana za huyo jamaa, na kila siku anaongea kuwa binti yake hana shida,…na wewe umeshakubaliana na hilo….’akatulia.

‘Mimi sijakubaliana naye kamwe, alinielezea hilo kuwa huyo mwanaume akataka kumuoa binti yangu, nikamwambi kwanza binti mwenyewe bado mdogo…hinahitajika muda wa kumfunda, ili aelekee kuwa mke, huwezi ukamchukua kama alivyo, akaenda kuishi na mume…pili, je huyo binti aliwahi kukutana na huyo mwanaume wakaongea japo kidogo, akakubali…..’mama Maua akainua kichwa kumwangalia huyo mtu.

‘Sisi tuliomba hivyo, kuwa jamaa yangu aje aongee na huyo binti, lakini kila tulipotoa hiyo hoja , huyo mwanaume wako, akawa anapinga, akisema yote tumuachie yeye…..sasa haya tunyoyaona hapa ni mageni, na niwaambie ukweli, huyu jamaa, hadhulumiki kirahisi….ni hatari, anaongea huku anacheka, lakini yaliyopo moyoni mwake….’akatulia kidogo.

‘Mimi namfahamu sana, hapo alipofikishwa lolote linaweza kutoka,….huwa anakuchoma kisu moyoni huku anatabsamu, kama vile hakuna kitu kimetokea,….na hatari, kuliko sumu ya nyoka,… lakini ni mpole kwa wanahitaji upole wake, …..’akawa anatikisa kichwa huku na kule.

‘Mimi hayo sijui, awe hatari, awe vipi sijui, kwasababu sikushirikishwa, mumekutana na huyo mlevi, mkadanganyana, bil ridhaa ya mimi na binti yangu….’

‘Kwani wewe mama unataka shilling ngapi?’ akuliza yule jamaa huku akitoa mfukoni, pochi yake iliyotuna kwa manoti ya pesa. Yule mama akainua kichwa kumwangalia huyo jamaa, akitoa pesa kwenye hiyo pochi.

‘Tatizo lenu, mnafikiria kuwa kila kitu kinanunuliwa kwa pesa….mnafikiri pesa , utajiri ndio kila kitu, mnasahau ubinadamu….ndio mimi ni masikini, lakini umasikini wangu sio wa kuuza utu wangu,…siwezi kamwe, kumuuza binti yangu….’kabla hajamaliza pesa nyingi zikawekwa kwenye miguu yake, nyingine zikidondoka chini….

Na mara yule mwanaume mlevi, na yule muoaji, wakatoka, na kuwasogelea , yule mama alikuwa kainama chini, hakujali kuwaaangalia, na mara yule mwanume mlevi akamsogelea mkewe, na alipoona zile pesa akainama kuziokota, huku akisema;

‘Mke wangu kipenzi…ooh, mungu akupe nini, mpenzi, ….neema ndio hii, ngoja nikusaidie kuokota, nitakuwekea mke wangu, au sio….’akawa anamshika begani huku akiziweka sawa zile pesa mkononi, na huku akijalambalamba…

Mara yule mshenga akafika, na kusimama kati kati, …huku wakiwa wamesimama yule muoaji na rafiki yake, na huku wakiwa wapo mama Maua na mwanaume wake;

‘Jamani kumetokea wazo jipya naona hilo linawezekana, maaan watu wazima ni dawa, na mapenzi ya kikubwa ni mazuri, kwa wale wanayoyajulia. Mwenzetu amesema kwa vile lengo lake ni kuoa, basi anaweza kubadili kibao, ….amuoe mama mtu, na kumuacha binti,….kwa vile huyo mlevi kasema hana ndoa na huyu mama,..sijui wazo hilo wewe mama unalionaje..

‘Kabisa, mimi sina ndoa na huyu mama, anaishi kwangu kama …….kupata hifadhi, simjui ….kabisa kama mke, tupo, nyumba moja, …lakini tunaishi kama kaka na dada, nje watu wanajua kuwa ni mke na mume, lakini ndani…hakuna kitu kama hicho, hiyo ni siri yenu,..hatukutaka kuitangaza, mnasikia, msiseme kwa watu,….’akasema kama ananongona huku akijaribu kuziweka zile pesa mfukoni mwake.

‘Mzee hizo pesa ni kishika uchumba, ni za mtu anayetaka kuolewa, je wewe ndiye uanyetaka kuolewa?’ akauliza yule rafiki ya mwanaume anayetaka kuoa.

‘Jamani kwani ugomvi, mim namshikia tu, …nyie hamumjui huyu mama, pesa nyingi kama hizi, hajawahi kuzishika,..sasa bora mimi nimuwekee , haina shida, nitamkabidhi zote….’akasema huku akizidii kuzizamisha zile pesa mfukoni.

‘Tafadhali zitoe hizo pesa na mkabidhi mwenyewe….’akasema huyo jamaa akiwa katoa macho.

‘Kwani ugomvi….haya nimezitoa…’akawa anazitoa, na nyingine zikadondoka, akazikangaga kwa mguu kama kuzificha,…na yule jamaa akamsogelea na kumsukama pembeni, akamshika mkono na kuzichukua zile pesa, akahakikisha habakiwi na pesa yoyote, na kuzichukua zile pesa pale chini, akamsogelea mama Maua.

‘Kama ulivyosikia mama Maua , hizi pesa ni zako,……tulipanga toka huko tulipokuwa kuwa hizi pesa, ni sehemu ya pesa za kukuwezesha…..hatukuwa na wazo hilo kuwa tutamkosa binti yako,…sasa hatuwezi kuzichukua tena, na kwa vile kuna wazo hilo limekuja…wazo la baraka, basi, hakujaharibika neno,…hizi pesa ni mali yako, …na usimpe kabisa huyo mlevi…’akasema huyo mwanaume, huku akimwangalia yule mwanaume.

Mama Maua akainua uso kidogo na kuwaangalia, hakuziangalia zile pesa….machozi yakaanza kumtoka kama maji……Yule mwanaume mlevi alipoona mwanamke wake hainui mkono kuzipokea, akajiinua huku akilalamika, na kusema;

‘Yaani hata wewe..unanizalilisha kiasi hiki…niliwaambiaje, hata zipokea, kama mimi mumewe nipo hapa wa kuzipokea, toka lini mke akapokea mahari….mahari hupokewa na wanaume…anajua sheria na mila huyo….’akawa anaongea huku akiinuka na kujifuta mchanga.

‘Kwani Maua yupo wapi?’ akauliza yule mshenga huku akimwangalia yule mama, kwa huruma.

‘Kaondoka, na hata rudi leo au kesho…’akasema mama Maua huku akifuta machzo usoni mwake, na hakuahangaika kuzipokea zile pesa, na yule jamaa akaziweka miguuni mwake.

‘Sasa unasemaje kuhusiana na hilo wazo, upo tayari, maana huyu mwenzetu anataka kusafiri, na anahitaji mwanamke mwaminifu, …keshachoka kuishi bial mke, na kaona wewe unaweza ukaishi naye kwa amani, na utulivu…..alimpenda sana binti yako, lakini kwa vile mwenyewe hukubaliani, basi hakujaharibika neno….unasemaje kwa hilo?’ akasema mshenga.

Mama Maua akasimama na kuwaangalia mmoja mmoja, akazishika zile pesa mkononi, ……

NB: Muda …muda umekwisha,….

WAZO LA LEO: Pesa ina majaribu makubwa, ukiwa huna ni mtihani, …unaweza ukadhalilika, na kama unazo pia kuna mitihani yake,…kiburi, zarau, na.unajiona wewe una kila kitu, unaweza ukasahahu hata utu wa wengine. Hala hala mti na macho, fedha zisitufedheheshe.

Ni mimi: emu-three

1 comment :

Anonymous said...

If you arе goіng foг most excellent сοntents lіke myѕelf, just pay a vіѕit
this site everyday sinсe it gives feature contents, thanks
Also visit my homepage ; http://feettoinches.info/