La mgambo limelia,
kila mwenye sikio na asikie, na amfahamishe yule ambaye hajasikia, kuwa leo ni
siku muhimu sana, siku ambayo ilikuwa ikisburiwa kwa hamu, siku ambayo haki
inarejea, haki inarejea kwa mwana wa ukoo wetu, haki iliyokuwa imechukuliwa na kwenda kusipostahili inarejea kwake….’ilikuwa ni mbiu ya mgambo, iliyokuwa
ikipigwa na mshereheshaji mashuhuri wa jamii ya Mzee Hasimu.
Kila mmoja alitega sikio kusikia ni nini anachotaka
kukielezea, na kwa vile minong’ono ilishapita , minong’ono iliyojaa propaganda potofu,
ambayo huwa inasikilizwa zaidi kuiko ukweli. Kutokana na propaganda hiyo, wengi
walitaka kujua kuwa kuna ukweli gani kwenye hilo waliloliskia, na waliposikia
hiyo mbiu ya mgambo, na kinachoelezewa, wakazidi kuingiwa na hamasa ya kuliona
tukio zima.
Ama kwa hakika lilikuwa tukio kubwa ambalo kila mmoja
alilisubiria, kwani kama ilivyobashiriwa, siku hiyo ndiyo iliyotakiwa mfalme,
kupewa kiti chake, na malikia kumiki wana wa jamii zote bila ubaguzi, lakini
ili aweze kulifanya hilo ni lazima apate mume bora, mume shupavu, jemedari, na kiongozi
muadilifu.
Kipindi chote cha mwaka, walikuwa wakimsubiria kiongozi ,
ambaye ndiye atakayeweza kulifikisha taifa hilo kule walipoahidiwa baada ya
miaka ya nyuma ya vita na kumwaga damu. Walikuwa wakimsubiria malikia mtarajiwa, malikia mama wa wanajamii
wote, kwani hata pale walipompata malikia malikia mwenyewe, bado, kiumri
alikuwa hajafikia hatua ya kuingia kwenye sehemu takatatifu, , wakawa
wanaisubiri hiyo siku ili waweze, kutawadhwa na kukabidhiwa majukumu ya kijami.
Muda uliokuwa ukisubiriwa ndio umefika, na majira yaliyokuwa
yakisubiriwa ndio hayo yamefika, tatizo likabakia ni nani mfalme, maana huyo
waliyetarajia kuwa ndiye mfalme, wamesikia kuwa kaliwa na mamba, jambo ambalo
liliashiriwa kuwa huenda sio yeye aliyestahili kuwa mfalme.
Majira hayo yalikuwa ni ya mavuno, na majira hayo ya mavuno,
kila mwanajamii hupeleka zawadi kwenye jumba, au sehemu wanayoitambua kama
sehemu takatifu, zawadi hizo, wanaamini kuwa ni sadaka, kwa ajili ya baraka za
familia zao, na zawadi hizo ndizo zinazotumika kwenye sherehe za kijamii, na mojawapo
ya sherehe hizo ni ya kumsimika mfalme na malikia na mambo mengi ya imani zao.na
pia kwa ajili ya kuweka akiba kwa siku zijazo.
‘Tumesikia kijana wa mzee mteule, kaliwa na mamba, hivi ni
kweli hii, na kama ni kweli, ina maana kweli hakustahili kumuoa malikia
mtarajiwa, sasa ni nani atakaye muoa?’ akauliza mama mmoja.
‘Unauliza jibu, eti ni nani wa kumuoa malikia, humuoni kijana
wa mzee Hasimu,…hilo limeshapitishwa na baraza la wazee, nani atapinga hilo’akasema
mama mwingine, huku akijiangalia alivyovalia, tayari kwa shughuli, kila mmoja
alijioana kavaliwa zaidi ya mwingine, mavazi rasmi ya shughuli ya kimila.
‘Na kama ni hivyo, ni nini hatima ya ukoo wa mzee mteule,
kwasababu kama uongozi wote utakwenda kwa hasimu wake, sizani kuwa ukoo huo
utaruhusiwa tena kuwepo kwenye jumba takatifu….nawaonea sana huruma, ….maana
wao wamejitahidi sana kuonyesha uongozi bora’akasema mama mwingine huku nay eye
akijiangalia alivyovalia.
Watu walianza kujiandaa, kila mmoja akitafuta nguo yake
maalumu, nguo ya kutokea, tayari kuwepo kwenye sherehe kubwa, na hakuna
aliyekubali tukio hilo limpite, hata wazee vikongwe, wagonjwa, kila mmoja
aliomba asaidiwe afike hapo kiwanjani, kwani wengi waliamini kuwepo kwao,
kunaweza kuwasaidia katika maradhi yao,
na matatizo yao, na wazee wataweza kujaliwa nguvu za kuweza kuishi
zaidi.
Katika imani zao , kiongozi, sio tu kuwa kiongozi, lakini
kiongozi anatakiwa kuwa na karama, ya kuweza kuwaombea wagonjwa na wenye shida
wapone. Kiongozi, anatakiwa mtu ambaye akiletewa tatizo anajua jinsi gani ya
kulitatua, na kiongozi alitambulikana kama mzazi wa kila mtu, …kwahiyo kila mtu
aliona ni muhimu kufika hapo kwa mzazi, na kwa mtoto kutokufika kwa mzazi ni kuvunja
heshima na adabu.,
La mgambo lilipolia, kila mmoja akajua siku imefika, na asiye
na mwana aeleke jiwe, na asiye na ngo ya maana akaazime kwa jirani, kila mmoja
alikuwa na upendo uliopitiliza, na hakuna aliyeombwa kitu siku hiyo akakataa
kama anacho. Na siku hiyo kila mwenye tatizo, hulibeba tatizo lake, na
kulifiksha huko, kwa ajili ya maombezi, wakijua ndio mwisho wa matatizo. Siku
maalumu iliyotabiriwa.
********
Malikia mtarajiwa alikuwa ndani kwake, akiwa kashika shavu,
hakukubali moyoni kuwa kweli mumewe ndio basi tena, kila mara alikuwa akiinua
kichwa kuangalia mlangoni, akitarajia kuwa ataingia mumewe, mumewe aliiyempenda
kwa moyo wake wote, mume ambaye kwake yeye alijua kiwa karibu yake, hata kazi
hiyo ya umalikia angeliiweza kuifanya kwa ufanisi zaidi.
Lakini kila alipoinua kichwa kumwangalia aliyeingia,
alijikuta akiangaliana na wapembe waliotumwa na kutoka kwa wahasimu wao.
Ingawaje kwa muda huo, hakutakiwa kuwaona kama mahasimu wake, kwani kama ni
kweli mumewe keshakufa huenda wakawa sio wahasimu wake, tena, ni wapenzi
wake.Hilo aliliomba listokee, lakini je dua yake ingekubaliwa, wakati mumewe
hajatokea.
Alikumbuka babu yake alipokuja asubuhi, na wazee wenzake,
ujio wao ulikuwa kama wa kumuaga, na ingawaje walisema bado hawajakata tamaa,
lakini ilionyesha dhahiri kuwa kuja kwao ilikuwa ni sehemu ya kumpa baraka kuwa
anaruhusiwa kuondoka hapo na kwenda huko kwenye jumba takatifu tayari kwa mume
mwingine mpya ambaye anatarajiwa kutoka upande wa mhasimu wao.
‘Binti yetu, kama tulivyokuambia, siku ya leo ndio siku
iliyotarajiwa, siku ambayo tuna uhakika kuwa mfalme alitabiriwa , ambaye anatakiwa
amuoe malikia mtarajiwa atatawazwa, …hii ni kusema kuwa kila mmoja, hana
mamlaka tena ya kulipinga hilo litakalotokea leo, ….tunatarajia, au tulitajia kijana
wetu atafika, lakini hadi sasa kama unavyoona hakuna dalili yoyote….’akatulia
huyo mzee, na malikia alikuwa kama kamwangiwa maji ya baridi kusikia kauli hiyo
Usiku kucha alikuwa akiombea kuwa wazee hawo wakifika
watafika na kauli yenye matumaini, na alikuwa tayari kusikia kuwa watazua tukio
hilo lisifanyie siku hiyo hadi kweli ijulikane kuwa mumewe hayupo tena dunia,
na uchunguzi ufanyike ili kubainisha ni nini kilichomsibu mumewe, kwani huenda
kuna hujuma ilifanyika, lakini kauli ikawa kinyume chake.
‘Hatujakata tamaa, kwanii saa ya mwisho ni saa ya jioni, …wenzetu
wao wameshajihakikishia kuwa kijana wetu hayupo tena, ndio maana wamejiandaa
kwa kila kitu…na ndio maana wametuma wapambe wao kuja kukuweka sawa…sisi
hatuwezi kuwazuia, na wewe usikatae kwa lolote lile…ila bado tunasubiri hadi
saa ya mwisho…’akasema mzee
‘Dalili kuwa kijana wetu bado yupo hai, zinajionyesha….na
mimi nina uhakika atajitokeza …lakini je imani hiyo ipo kwa wote,…kwahivi sasa
hakuna mwenye imani hiyo tena, kila mmoja keshaamini kuwa kijana wetu hayupo
hai tena. Mawazo ya kila mmoja ni kuangali ni nini atakipata siku kama ya leo, ….hakuna
anayejali uhalali, hakuna nayejali, kuulizia ni kweli kijana yetu aliliwa na
mamba, au kuna hujuma ilifanyika.
Siku ya leo, kila mmoja ni kama watu wenye njaa walioona
chakula mezani, unafikiri nini kitafuata, kama sio kila mmoja kufikiria jinsi
gani atashibisha tumbo lake, hata kama wengine watakosa, ….hakuna mwenye
kumjali mwenzake, zaidi ya tumboo lake….
Hata hivyo, tukubali ukweli kuwa siku ya leo nii siku
tukufu, ni siku ya matarajio, sisi kama wenzetu, siku ya leo ni siku ya matajio,
ya kumsimika kijana mpya ambaye ndiye atakayekuwa mfalme…..sisi kama wazee,
tumekuwa tukijiuliza kama hivi ndivyo ilivyo, je ni kweli huyo kijana wao
anastahili kuwa mfalme,mfalme yule tuliyemtarajia…’akawa kama anauliza huyo
mzee.
‘Kwahiyo binti yangu, hapo ndipo tunaingiwa na wasiwasi,
lakini hata hivyo hatuwezi kufanya lolote, siku kama ya leo haitakiwi kumwaga
damu, siku kama ya leo, inaongozwa na baraka, zilizoasisiwa na wazee wetu
waliotangulia, na lolote litakalofanyika leo, ni matarajio, na limebarikiwa, ya
kesho yatajileta yenyewe,….
Kama itatokea kama ilivyo, keshao itasema, nakuhakikishia
kuwa kama sio kweli, kama hafai, na wametumia ujanja, ulaghai na nguvu, lazima
kutatokea kipingamizi…kwa upande wetu hatuwezi kufanya lolote hadi siku hii
ipite…’akasema huyo mzee.
‘Tunakuomba uvute subira, na ukubali kwa lolote lile, hadi
hatua ya mwisho…sisi kama wazee tunaojua haya mambo, hatuna wasiwasi, …ndio
kama binadamu tuna wasiwasi kuwa huenda kijana wetu kazuiliwa sehemu, na ndio
maana kashindwa kutokea…lakini tutafanyeje kwa hali kama hii….’akasema huyo
mzee.
‘Jeshi tunalo na limejiandaa kwa lolote lile, linasubiri
amri..lakini sio siku kama ya leo…hatuwezi kutumia nguvu,…usije ukaona kuwa
tumekutelekeza, hapana, …siku kama ya leo ni siku muhimu sana hapa kwetu, na inayoaminika
kuwa ni siku tukufu, sote tunatakiwa tutulize shughuli zetu, tuombe, tushukuru,
…’akasema huyo mzee huku akinua mikono juu, na wenzake wakafuatilia hivyo
hivyo.
‘Na wewe malikia mtarajiwa, huna kipingamizi, wote
wamekukubali, kwahiyo baraka zako
zinahitajika kwa wanao wote, uwakubali wote kuwa wewe ni mama yao, bila kujali
kuwa anatokea huku au kule, bila kujali kuwa ni ukoo gani, ni hali gani,…hiyo
ndiyo hulka ya mama , malikia mtarajiwa…tuliza kichwa chako na elekeza maombi
yako kwa mwenye nguvu wa kila jambo, najua tutafanikiwa…’akasema huyo mzee na
kuinamisha kichwa
Hapo malikia hakutakiwa kusema lolote au kuongea lolote,
anachotakiwa na kuinua kiganja chake cha mkono na kuwashika wazee wale kichwani
mmoja mmjoa,, na baadaye wote wakaondoka, akabakia peke yake, na hapo hakuweza
kuyazuia machozi tena, akashindwa kuvumilia machozi yakamtoka , akajitahidi
kuziia kwikwi,…akijua kuwa yeye ni mama wa wote, na anhitajika kukubali yote
kuwa ni mapnzi ya mwenye nguvu zaidi ya wote…..
Moyoni malikia alikumbuka ndoto yake, ndoto ambayo
iliashiria harusi, …harusi ambayo aliiona ni tofauti na harusi za hapo, akiwa ndani
ya hiyo ndoto, alijiona kavalia nguo za huko alipotokea, na wazazi wake wakiwa
pamoja naye, na muda huo walikuwa wakimsubiria mume mtarajiwa kutokea, lakini
alikuwa kachelewa, kiasi cha kuwakatisha tama watu…haikupita muda mara kwa
mbali wakasikia vigelegele, kuashiria kuwa mume keshafika.
Akiwa kwenye hiyo ndoto, alijiona yupo kasimama akimsubiri
huyo mume mtarajiwa afike ili wafungishwe ndoa, na muda ulikuwa ukienda, ….na
ndoa hiyo ilikuwa na muda maalumu, ukipita haiwezi kufungwa tena, na kila
akiangalia mishale ya saa, ilikuwa ikionyesha kuwa kumebakia dakika chache, …akawa
anageza kichwa kungalia huko mumewe anapotokea, mara kwa mara kwa matarajio,
lakini hakutokea na muda ulikuwa ukienda kwa kasi….
Na ikawa imebakai dakika moja..mume hajatokea….akawageukia
wazazi wake, na wao, walikuwa wakiangalia kule mlangoni ambapo mume anatakiwa
atokee..haonekani, nje ni vigelegele na shangwe, na hapo akataka amwambie mmoja
wa watu wake aende nje akamlete huyo mume kwani muda unapita, na alipogeuka
kuangalia saa akakuta imebakia dakika moja inakimbilia kwenye sekunde, na mara
mlango ukafunguliwa…
Kipindi hicho yeye alikuwa akiongea na mpambe wake, kwani
alitaka kumuelezea kuwa aende akawaharakishe huko nje, na mpambe wake alikuwa
kamziba, kwahiyo hakuweza kuone kule mlangoni, kitu ambacho hakutaka kiwepo,
kwani yeye alitaka kuona jinsi mume wake atakavyotokea pale kwa mara ya kwanza…..akawa
anataka kunyosha mkono, kumuondoa mpambe wake, kwani alichotaka kumwambia
hakina maana tena.
Kila mmoja pale ndani kwanza alipumua kwa shauku, na huku
wakishukuru, na nyuso zilizoanza kukata tama zikabadilika na kujaa furaha, kila
mmoja akijiandaa kuona huyo mume ametokelezeaje.
Mara mtu wa kwanza akatokea, ambaye ndiye alitakiwa kuwa
mumewe mtarajiwa, …mara nyuso za watu zikabadilika , kutoka kwenye nyuso za
tabasamu, na kuelekea kwenye nyuso za woga,..macho yakawatoka pima kwa woga,…
Vipi tena, …mara watu wakainuka kwenye viti vyao,.. hakuna
aliyesubiri…kwa sekunde chache tu, kila mmoja alitafuta sehemu ya kutokea, ……ikawa ni
purukushani….bibi harusi akajikuta yupo peke, yake, akawa sasa anageuza kichwa,
kwani muda huo alikuwa akiwaangalai watu wakikimbia, akashikwa na mshangao,
sasa akawa anageuza kichwa taratibu kuanglia kule mlangoni, kuona nini
kimetokea hadi watu wote wakimbie…mara akafumbua macho, …..kumekucha.
NB: Nimeona niitoe sehemu hii kama ilivyo, ...sina jinsi,
WAZO LA LEO: Sasa hivi ni hapendwi mtu, hasa kunapokuwepo na masilahi, na hata wengine husihia kusema `mjini hapa' ...lakini tukumbuke kuwa haki ya mtu haipotei bure, kula utakula, lakini ipo siku utaulizwa. Tafuta riziki yako kwa chumo halali ili upate baraka.
Ni mimi:
emu-three
1 comment :
Tupo pamoja..kazi nzuri sana....
Post a Comment