Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, October 1, 2012

Uchungu wa mwana, aujuaye ni mzazi



Katika maisha haya, unaweza ukakutwa na majanga na kufikia hata kukufuru, ukizania wewe tu ndiye unayeonewa, lakini ugumu na matatizo ya kimaisha yapo katika watu wengi, ila ni kwasababu tu hujawahi kusikia au kukutana na watu kama hao. Nalisema hili pale nilipokumbuka kisa cha huyu mwanadada ambaye nilimkuta akiwa kainama upembezoni mwa nyumba huku kashika shavu na michirizi miwili ya machozi ikiwa imeshajichora mashavuni.

Niliingiwa na huruma nilipoona ule ukaaji aliokuwa kaka huyo binti, hasa kwa binti mkubwa kama yule, na ile nguo nyepesi aliyovaa asubuhi kama ile licha ya baridi kali.  Pembeni yake kulikuwa na ndoo ya maji, iliyo tupu. Niliingiwa na moyo wa huruma nikamsogelea kwa tahadhari, kwani dunia hii haina wema, unaweza ukajitia una huruma, na huruma hiyo ikakutokea puani.

Wakati namsogelea kwa tahadhari,nilikumbuka kisa cha jamaa yetu mmoja, ambaye alienda kusota jela, baada ya kujifanya msamarai mwema, kwa kumoenea huruma binti kama huyu. Yeye alimkuta huyo binti  njiani, akiwa analia, na hali aliyomkuta nayo, ilikuwa ya kusikitisha, kwani kama alivyodai, ana siku mbili , kula hali, anachoambulia ni makombo. Yule jamaa yangu alipomuona kwenye hiyo hali akamchukua kwake, lakini  kabla hajatahamaki polisi hawa wapo mlangoni pake.

‘Tumeskilia wewe umemchukua msichana  wa watu, umemficha hapa kwako , yupo wapi?’ akaulizwa.

‘Afande, mimi nimemuona huyu binti njiani, akiwa analia, nikajaribu kumuuliza ana tatizo gani, akawa hanijibu, lakini kwa hali aliyokuwa nayo ilionyesha dhahiri kuwa ana njaa, nikaona nimchukue kwangu, ili anywe chai, halafu atanielekeza kwao, au polisi ikibidi, kwani hali aliyokuwa nayo hata wewe ungelimuonea huruma, inaonyesha wazi ana njaa, na pia mahala kama pale nilipomkuta hapana usalama’akajitetea huyo jamaa yangu.

Wale maaskari wakaangua kicheko, na kusema;
‘Hivi wewe kweli una akili, ukutane na binti wa watu,tena msichana, badala ya kwenda naye polsi unampeleka kwako, kwanza wewe una mke, au ndio ulitaka awe mkeo wa muda baadaye umeshamuharibia maisha yake unamtelekeza!’ akasema yule askari  huku akiangalia huku na kule kama ataona mke wa jamaa yangu huyo.

‘Mimi ninaye mke, na kwasasa hayupo kaenda kwao,  hivi sasa nipo peke yangu, alikwenda kwao kusalimia.’akajitetea jamaa yangu huyo

‘Kwahiyo ukaona uchukue mwanya huo, kutorosha mabinti za watu,wewe huoni hilo ni kosa kubwa, linalinganishwana kuteka nyara. Na wewe hujui kuwa utakuwa na mtoto kama huyo siku za baadaye? 

’akasema yule askari huku akitikisa kichwa na mwenzake akatikisa kichwa kukubaliana naye.

‘Jamani, huyu binti wala sijamtorosha, sivyo kabisa mnavyozania nyie, kwanza yupo hapo ndani anakunywa chai, hebu ingieni mumuhoji wenyewe‘akasema na wale maaskari wakaingia ili kuhakikisha, na wakamkuta yule binti akiwa anakunywa chai, na alipowaona wale maaskari, akakurupuka pale mezani akitaka kukimbia, wakamshika.

‘Wewe ulikuwa wapi muda wote huo, ulikuwa na huyu muhuni, ndiyo yeye anayekuhadaa kila siku ehe, utatumabie vyema?’akasema yule askari huku kamkazia macho yule binti.

‘Naogopa..hapana, niliku….njiani’akawa anasema yule binti akiwa na wasiwasi. Baadaye walikuja walezi wa huyo binti na kusema kuwa huyo ndiye binti yaoo wanayemtafuta , na mtego wao umeshagundua kuwa huyo jamaa yangu ndiye anayemuhadaa huyo binti,  na walikuwa hawajajua kuwa ni nani.

‘Lakini mimi ni mara yangu ya kwanza kukutana na huyo binti’akajitetea jamaa yangu huyo.

‘Wote Huwa wanasema hivyohivyo, utuambie ukweli maana tuliamua kumwekea mtego, kwani tabia zake zimebadilika siku hizi, …’akasema baba mlezi.

‘Unajua huyu binti alianza kubadilika ghafla, ukimtuma dukani au sokoni anakawia kurudi, na tukienda kazini tukirudi hakuna kilichofanyika, tukasikia kwa majirani kuwa kuna mwanaume anaonekana akiwa naye mara kwa mara, basi tukaona tuweke mtego, na leo umenaswa…kumbe ndio wewe, sasa utumabie ukweli,mtu mzima kama wewe huna haya kutembea na mabinti wadogo kama hawa …’akasema mama ambaye kumbe ni mama anayeishi na huyo binti kama mama mlezi.

‘Lakini muulizeni mwenyewe huyo binti, kwanini mnanishinikiza mimi kuwa nimemtorosha, wakati mwenyewe yupo hapa anaweza kujielezea, jinsi ilivyokuwa, nakuomba tafadhali wewe mama usikashifu, mimi siwezi kutembea na huyo binti’akajitetea huyo jamaa na yule binti alikuwa kainama chini akionyesha aibu na kuogopa.

‘Tumuulize mara ngapi, kwani ukimuuliza anasema ukweli, yeye ukimtuma mahali iwe dukani au sokoni, akichelewa, au akifanya kosa, ukimuuliza yupo kama bubu, hivyo hivyo unavymuona, ainaimana chini akama anatunga sheria zake, hasemi kitu, akini akiwa na wenzake, huwezi amini, au akikutana na wavulana, ni muongeaji hodari, ngoja mfike, anakuwa kama hajui kuongea, ‘akasema huyo mama.

Mabishani hayo hayakusaidia kitu, na hakuna kilichokubalika hapo, ikibidi jamaa yetu huyo, akakamatwa na kupelekwa kituo cha polisi, huko jamaa kama unavyowajua walianza kumtesa huyo jamaa eti asema ukweli, mateso ambayo yalimuathiri sana, na ilibidi asema uwongo kukubali tu , ili asiendelee kuumizwa.

‘Ilibidi nikubali tu, maana mateso yalikuwa makubwa, hata sasa hivi ubavuni nina maumivu makali, ’akajitetea

Raia wema majirani wanaomjua huyo jamaa waliposikia ikabidi wafike kituo cha polisi kwenda  kumtetea, na baadaye hyo binti aliitwa na mkuu wa kile kituo ili ahojiwe vyema. Yule binti aliulizwa, akasema ilivyokuwa, lakini walezi wa huyo binti walisema huyo binti sio mkweli, kwani mara nyingi akifanya kosa hukana, na kusema uwongo hadi ukweli ukidhirika, ndipo anajikanyaga.

‘Sasa nyie mna uhakika gani kuwa huyu mwanaume ndiye huyo anayemuhadaa huyu binti yenu?’ akauliza mkuu wa kituo.

‘Ni baada ya kuweka huu mtego, ndio tumemnasa huyu jamaa,atakuwa ni yeye tu, kwani wanaume wana maana’akasema mama mlezi.

Baadaye ya siku mbili jamaa akaachiwa kwa dhamana,huku akiwa kateswa, kadhalilika kwa huruma yake.

Mke wa jamaa huyu aliporudi akayasikia hayo yaliyomkuta mume wake, na siku kabla hajaondoka, alishasikia kwa watu kuwa mume wake hajautulia, na alipomuhoji mume wake, alikana kabisa, na leo hii kasikia jambo kama hilo, akajua kweli kumbe mume wake ana tabia za namna, hiyo.

‘Kama ni hivyo, mimi wala sikai hapa, narudi kwetu, kwani huko ninaye baba na mama na kuna wanaume wengi tu walikuwa wakinihitaji, na hata leo naweza kuolewa, nenda kwa hawo mabinti wa mitaani  unaowataka’akasema mke wake huku akijiandaa kuondoka.

‘Mke wangu sio kweli, hayo waliyosema watu ni uwingo, ni fitina za watu, mimi sina tabia hiyo kabisa, hata kama ni kuapa naweza , twende tukaapishwe kwa watu wa dini, mimi nipo tayari’akasema lakini haikuwa rahisi keshi yake mke wake akarudi kwao, na ilibidi asubiri kesi hiyo ya huyo binti iishe ndio aende nyumbani kwa huyo mkewe wakasuluhishwe.

‘Huyu jamaa kasingiziwa, mimi namfahamu sana, kwani nafanya akzi naye, kuna mabinti wanamtaka huyu jamaa, na kwa msimamo wake ulivyo, wakaona dawa ni kumpakazia ubaya. Sasa ukiongezea na hili, ndio wamezidi kumtangaza kwa kusema; `Sasa mnaoana anajifanya msafi kipo wapi, na bado...mpaka akome ubishi, mjini hapa’

Basi watu ikabidi wamshauriu huyu jamaa, ili awahi kuikoa ndoa yake, ni bora akaongee na walezi wa huyo binti,;

‘Ukiongea na walezi wa huyo binti, yataisha kienyeji, kwani wao bado hawana uhakika kuwa kweli wewe ndiye unayemuhadaa binti yao, ukamaliza nao, waatenda kuifuta hiyo kesi huko polisi, kama ujuavyo   kesi kifika huko polisi ina utaratibu wake, na nimesikia wakisema kuwa kesi hiyo wataifikisha mahakamani, kwani matendo kama hayo yanazidi kila siku, inatakiwa kutolewa adhabu kali kama fundisho’akasema jamaa mmoja.

‘Mimi nipo tayari kwenda huko mahakamani, hata nikifungwa nifungwe tu, lakini siwezi kukubali jambo ambalo sijalifanya,na tutaongea nini na hawo walezi wa huyo binti, wakati wameshashikilia kuwa mimi ni mkosaji, yaaani huruma yangu ndiyo inaniponza’ akasema huyu jamaa kwa sauti ya huzuni.

‘Hapo huna jinsi ni vyema ukajishusha, na kwenda kuongea na hawo wazazi,maana hata kama ingelikuwa ni wewe binti yako kakutwa hivyo, usingelikubali, moja kwa moja ungelifikiria hivyo, sisi tupoo na wewe tutakutetea’ wakasema wenzake wanaomjau vyema.

********

Basi nilipokumbuka hilo tukio, nikawa na tahadhari ya kuongea na huyu binti, hata hivyo moyo wa huruma  ulinituma angalau nimuulize huyu binti ni nini kilichomsibu asubuhi kama ile yupo upenuni mwa nyumba huku akiwa kavaa nguo ambazo baridi ilikuwa ikimpenya bila ya huruma, akiwa analia.Mimi kama mzazi moyo wa huruma uliniingia nikiwaza mbali, kuwa haya yanaweza kutokea kwa mtoto wa yoyote yule na lililojema ni kusaidiana. Ukiwa mzazi hisi akama hizi zitakujia tu, kwani uchungu wa mwana anayeujua vyema ni mzazi.

‘Habari yako binti?’ nikamsaili na akawa kama kashituka aliposikia sauti yangu na kitu cha kwanza alichofanya nikujiweka vyema.

‘Sija-shikamoo..’akainuka pale na kusimama huku akisalimia kwa kigugumizi akaishika ile ndoo na kuangalia huku na kule.

‘Samahani nilikuwa napita tu, bahati nikakukuta ukiwa katika hiyo hali, kwanini upo hivi na asubuhi hii, na jinsi ulivyovaa, huoni kuwa unaweza kuumwa na magonjwa ya ubaridi?’ nikamuuliza.

‘Kama nikuumwa nimeshaumwa sana, na taabu niliyo nayo anayejua ni mungu, iliyobakia ni siku ifike roho yangu itolewe tu, ili nikapumzike huko ahera, ingawaje sijui kuwa kuna kumpumzika huko mbeleni lakini naona ni heri tu nijifie…na ipo siku tu, nitaamua moja, maana nimechoka,kwanini mimi…’akasema huku machozi yakimtoka.

‘Kwanini uwaze hivyo,hujui kujiua ni dhambi, ni sawa na kuua mtu’nikasema nikiwa nahisi kuwa anaweza kweli akafanya hivyo.

 ‘Mungu ndiye anyejua ni kwanini nawaza hivyo, kwani hakuna ambaye nitamsimulia matatizo niliyo nayo akanielewa, hakuna atakayejua jinsi gani ninavyoteseka, na ninaendeela kuteseka, hakuna anayejali, …. Ina maana mimi nilizaliwa katika dunia hii ili nije kuteseka, hapana,….labda sistahili kuishi’akasema huku akifuta machozi.

‘Kwani wazazi wako wapo wapi?’ nikamuuliza.

‘Wazazi wangu..?, sijui wapo wapi, baba keshaoa mke mwingine, mama naye kaolewa na mume mwingine, na….ooh, Lakini yote maisha, kwani hata hivyo siwezi kuwalaumu sana, kwani hayo yaliyotokea huko nyuma huenda hawakuyatarajia, lakini adhabu naipata mimi‘akasema na kuniacha nikiwa na maswali mengi kichwani.

‘Kwani hapa unaishi na nani,?’ nikauliza.

‘Nimechukuliwa na huyu mama , ni ndugu tu, wa karibu, alinichukua akidai atanilea na hata kunisomesha, lakini tangu nije kwake ni mwaka wa tatu sasa, sijui cha kusoma wala nini, nimegeuka kuwa mfanyakazi wake wa ndani, aheri angeliniacah tu kule kijijini nikaishi kama alivyonikiuta’akasema.

‘Ohh, kama mfanyaakzi wa nyumbani, ina maana anakulipa mshahara?’ nikamuuliza.

‘Hahaha, anilipe mshahara, yeye anadai kuwa nakula chakuala chake cha bure, na nalala kwake bure, gharama yake ni kubwa kuliko huo mshahara’akasema.

‘Sasa kwani huna jinsi ya kukutana na wazazi wako ukawaambia maisha unayoishi, kama inawezekana ukaishi na mmoja wa wazazi wako, kwani wao ndio watakuwa na uchungu na wewe kuliko huyu mtu baki, wao ndio watakuwa na uchungu na wewe kama wazazi?’nikamuuliza.

‘Hayo mengine tena, hujui jinsi gani wazazi wangu hawo walivyokuwa, siku ile kiumbe mimi nilipoingia tumboni mwa mama yangu, …huenda mimi naadhibiwa kwasababu yao, na hapa nilipo nahisi hakuna kati yao anayenihitaji tena,kwani kila wakiniona hasa mama, huwa anaishia kulia, akikumbuka machungu yalimkuta.

Ama kwa baba naye sijui anawaza nini, maana keshaoa  mke wake, mkewe ni  mbaya kuliko hata huyu ninayesihai naye hapa, nakumbuka siku moja nilikwenda kuwatembelea akasema waziwazi kuwa yeye hajaza, kwani kipindi hicho alikuwa hajapata mtoto, alisema yeye hataki kuishii na mtoto ambaye sio wake..’akasema na kuinama chini na mara sauti ikatoka ndani

‘Wewe Maua unafanya ninii huko nje, hujui nachelewa kazini, umenishanileta maji nataka kuoga niondoke, na hizo nguo nikija nizikute hapo hapo, utazifua kwa mate yako …na vyombo hivyo, vyote usafishe, na huyu mdogo wako hakikisha umemnyoshea nguo zake, atachelewa shule……?’ sauti ya mwanamke ikaita toka ndani, na yule binti alikurupuka utafikiri kasikia sauti ya nani, nikabakia nimeduwaa.

Kwakweli nikawa na hamu kubwa ya kutaka kujua historia ya huyo mtoto, naifuatilia kwa karibu tuzidi kuwemo ili tuweze kuisikia.

NB: Hiki ni kisa kingine, sijajua kitakuwa na ukubwa gani, ambacho kina ujumbe maalumu, hasa kwa jamii yetu hii. Naombeni tuwe pamoja .

WAZO LA LEO: Ujumbe kwa vijana wetu na wale ambao hawajaingia kwenye ndoa: Tusiwe wepesi kukimbilia tamaa za kimwili, tukishajiona tumependana, kwanza tujenge tabia ya kutafakari matokeo ya hilo tendo. Tujiulize Je tumeshajiandaa na hayo matokeo, je kweli ni sahihi kwa muda huo, Je likitokea lolote tutafanyaje, tusiwe wepesi wa kukidhi mataminio ya nafsi zetu, kwani majuto huja baada ya kitendo, na majuto ni mjukuu.


Ni mimi: emu-three

1 comment :

Yasinta Ngonyani said...

Duh! nimesoma hiki kisa huku machozi yakinitiririka kama huyo mtoto..kuna mambo mengi nimeyakumbuka...ni kweli katika maisha watu tusiwe wapesi kama wazo lisemavyo...kwa vile wanaoteseka ni watoto/wengine...FIKIRI KWANZA NA BAADAE TENDA.