Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, July 30, 2012

Hujafa hujaumbika-77 hitimisho-35




Nilimkuta nesi akiwa kakaa kitandani huku kashikilia karatasi mkononi mwake , ilikuwa ni barua,  na nilipomtizama usoni mwake niliona sura iliyojaa huzuni na hata machozi ambayo yalikuwa hayajakauka ambayo yaliacha michirizi usoni yalionekana wazi wazi. Mimi  nikamsogelea, lakini ilionyesha wazi kuwa hakuwepo hapo ki-akili. Nikamsogelea pale kitandani na kumgusa begani, akashituka na haraka akafuta yale machozi usoni, akasema.

‘Leo hii sijisikii vyema…, na ningelifurahi kama nisingelisumbuliwa na mtu yoyote, lakini kwa vile ni wewe nitavumilia tu kwasababu nahitaji kuongea na wewe…’akasema.

‘Kuongea na mimi kuhusu kitu gani, na kwanini upo katika hiyo hali na nimesikia kuwa leo hutaki kuongea na mtu, Ila mimi nikija niruhusiwe kukuona, kuna kitu gani kinakusumbua…au ni katika ile mipango yako ….?’ nikamuuliza.

‘Ama kama kuna kitu gani kinanisumbua, wewe unajua jibu lake, sizani kama ni swali la kuniuliza hilo kama kweli unajali hisia za watu, lakini sio mbaya, nikakuambia ni jambo gani lililonifanya hadi nifikie hatua hii na hali kama hii unayoniona nayo, mimi sio mtu wa kulia lia, lakini nashangaa leo machozii yananitoka….’akasema na kuifunua ile karatasi aliyokuwa nayo mkononi mwake.

‘Najua kuna barua umeipata,…kutoka kwa yule binti wakufikia wa wakili mkuu. Hapa kwenye hii barua niliyopewa na mama yake kaandika kuwa kakuandikia barau iliyoelezea kila kitu, nay eye keshaondoka,….. na hatarajii kurudi tena, labda kama akija ni kwa ajili ya kuniokoa mimi nisiingie matatani…kama itaingia matatani, lakini kwa maelezo yake kasema anajua kabisa mimi sitaingia matatani…..’akasema.

‘Matata gani hayo…..?’ nikamuuliza na yule nesi akainua uso na kuniangalia , na safari hii ulikuwa ule uso wa ujasiri, akasema;

‘Sizani kama mpaka sasa hivi hujajua lolote kuhusu huyu binti, najua unamjau vyema, na hata kabla hajakuandikia hiyo barua,najua ulishajua nini alichokifanya, nikuulize, hiyo bunduki ulipoipata uliangalia alama zote za vidole, sizani kama iliwahi kutolewa pale nilipoificha..kabla hujaigundua wewe…’akasema.

‘Ina maana ni wewe uliyeificha pale, mbona hukutuambia hilo?’ nikamuuliza.

‘Sikuwaambia hilo na mengine mengi, lakini niliyafanya hayo kwa ajili ya huyu binti Yatima na nilisubiri wakati muafaka,…kwasasa  nipo tayari kubeba yote yanayomuhusu huyo binti, namjali na kumuonea huruma,na sijui kama nyie mna huruma na yeye, kwani aliyoyatendewa hayakumstahili….’akasema.

‘Lakini mtendaji wa hayo yote ni mpenzi wako’nikamwambia.

‘Najua hilo,….na siku nilipopata hiyo habari kwa mara ya kwanza nilimlaani sana huyu jamaa yangu, nilitaka nimfanye kitu mbaya,lakini nikiwaza nakujiuliza kwanini alifikia hatua hiyo….huenda yeye mwenyewe angelikuwa na jibu zuri, lakini mimi moja kwa moja namtupia lawama mkewe…’akasema

‘Kwanini umtupie lawama mkewe?’ nikamuuliza.

‘Huenda mimi ni tofauti na wanawake wengine,huenda nikaonekana mbaya, lakini huwa nasema kuwa mke anaweza akabeba lawama pale mumewe anapokwenda nje ya ndoa.Hebu nikuulize wewe unayejifanya kuwatetea,….hivi  kama mke anamtosheleza mumewe, na kutimiza yote yale yanayostahili, huyo mume angeliweza kutoka nje ya ndoa, ukiona hivyo,kuna walakini, ….na ukiangalia hii  ndoa ya mtu wangu, walioana kwasababu tu ya mslahi fulani , lakini sio kwa ajili ya upendo..’akasema.

‘Maslahi gani hayo?’ nikamuuliza.

‘Wanayajua wenyewe, …huyu jamaa yangu, asingeliweza kumaliza masomo yake huko Ulaya kama asiingeliweza kupata msaada wa huyo mkewe, wakati huo alikuwa binti mwenye nazo,….yapo mengi yaliyotokea huko, …sina muda wa kukusimulia,…Ila jamaa ilibidi ajifanye kuwa anampenda,ili afanikiwemalengo yake, ingawaje ni kweli kuwa binti wa watu yeye alishampenda, ….ikabidi waingie kwenye pendo la kuigiza,mmoja akijua ni kweli anapendwa lakini mwingine akifanya ili apate anachokitaka….’akasema.

‘Una uhakika na hilo kuwa alifanya hilo kwa kuigiza tu, ….kwani kwa hali halisi inaonyesha kuwa jamaa yako huyo hajatulia ni tabia yake, huoni, mara kwa huyu na hata akajikuta yupo kwa Kimwana,ina maana kwa Kimwana nako alikuwa naye kwa ajili gani,?’ nikamuuliza.

‘Kimwana,Kimwana….mmh,sikiliza nikuambie ukweli, Kimwana alivyo, kila mwanaume angejikwaa kwake, alikuwa kajipanga iwe hivyo,..ndio ni mzuri, ana sura ya mvuto, umbo lililojijenga vyema, lakini yeye hakuwa na upendo na mwanaume yoyote,zaidi ya kutaka kile akitakacho kwa huyo mwanaume….bahati mbaya, akawa hajali kuwa anaiangamiza jamii….’akasema na kutulia.

‘Kwa vipi aiangamize jamii?’ nikamuuliza,na hilo swali likamfanya aningalie kwa macho ya ukali, akasema;

‘Maswali mengine bwana, yanakera, wewe siulishasikia kuwa Kimwana alikuwa na ngoma, na yeye ndiye aliyemuambukiza wakili mkuu, na wakili mkuu akaniambukiza mimi, na sijui wangapi wameshaambukizwa kutokana na yeye na kwa udadisi wako unajifanya hujui, haya nimeshakuambi kuwa na mimi nina ngoma, nenda katangaze mahakamani….’akatulia na kuonyesha kuwa alikuwa akivumilia maumivu fulani moyoni.

‘Una uhakika gani kuwa yeye ndiye aliyemuambukiza wakili mkuu,huenda wakili mkuu aliambukizwa na mtu mwingine, na wakili mkuu akamuambukiza Kimwana….?’ Nikamuuliza.

‘Mimi namjua sana Kimwana, namjua kuliko wengine wote,pamoja na kuwa rafiki yake,lakini mimi nilimfanyia uchunguzi wa maisha yake toka alipotoka huko kijijini kwao,….na mtu aliyemuambukiza huo ukimwi ni tajiri mmoja, aliyekuja na mapesa yake, akawa anayamwanga kama njugu, …Kimwana kwa tamaa zake akajiingiza kichwa kichwa, nilimkanya…..’akasema.

‘Jamaa huyo licha ya pesa,….kweli alikuwa mrembo na kila akipita mitaani na gari lake la kifahari, wanawake wenye pupa wakawa wakijipitisha kwake,na yeye hakuwa na hiana, akawa anawamwagia pesa na kuwaachia virusi….’akasema.

‘Wewe ulijuaje yote hayo kuhusu huyo jamaa?’ nikamuuliza.

‘Mimi ni jasusi …licha ya kuwa niliacha hiyo kazi, lakini huwa naifanya kama sehemu ya starehe zangu, na huwa kila jambo nalifanyia uchunguzi kwanza kabla sijaliingia. Siwezi kukudanganya kuwa mimi sikuvutika kwake,….kama wengine nilitamani awe mpenzi wangu,lakini mimi nilichowaza zaidi ya wengine ni kuhus hizo pesa, na wapi kazipatia, na katokea wapi?’ akasema.

‘Uligunduje hayo?’ nikamuuliza.

‘Mtandao,…..na nina washikaji wengi idara ya mambo ya nje,na ….naona huko tusiende, ila kama nilivyokuambia mimi ni jasusi, yule jamaa niliweza kuingia hadi chumba alichofikia, na nikaweza kupitia mizigo yake, na hatimaye nikapata kile nilichokitaa…..nilikuta kitabu chake cha kumbukumbu, na katika maelezo yake, kuna sehemu kajielezea kabia, kuwa siku alipojua kuwa ana ukimwi, ndipo alipojua kuwa utajiri wake hauna maana tena, na aliapa kuwa atawaambukiza watu zaidi ya elifu, kabla hajatulia na utajiri wake….’akasema.

‘Uliwafahamisha watu wa usalama?’ akaulizwa.

‘Wewe unanionaje mimi, unaniona kama mtoto mdogo, unafikiri mimi sina huruma na wanadamu wenzagu,…aliyefanya huyo jamaa akamatwe ni nani kama sio mimi….lakini niliwaambia kuwa wasinitaje kabisa, maana mimi sio askari..nashukuru kuwa nilitimiza wajibu wangu, na nikawa nawapitia wale wote niliowajua kuwa waliwahi kutembea na huyo jamaa kuwaonya, na ikibidi wakapime….’akasema.

‘Ulifanikiwa kwa hilo?’

‘Nikuambie ukweli, hawa akina dada ambao wameamua kujiingiza nah ii tabia,….hawajli kabisa, wenyewe wameshajichukulia kuwa wapo kazini, na kwenye kazi yoyote kuna ajali yake,…kuna hatari yake, na moja ya hatari ni huo ugonjwa,kwao wao ni tumia upatapo maana maisha ni mafupi…’akasema.

‘Kimwana naye alisemaje?’ nikamuuliza.

‘Kimwana nilipomuambia, alichukulia kuwa ni ule upinzani wetu,na hata nilipomshurutisha, hakunijali,akasema hajali, kwani kama anao, hata mimi nitakuwa nao,na wengine wengi,kwahiyo kifo cha wengi ni harusi…nilimchukia kweli kwahiyo kauli yake,….’akasema.

‘Kama wewe ulijua hilo kwanini bado ukawa una mahusiani na wakili mkuu….?’ Nikamuuliza.

‘Kwa kipindi kile sikujua kuwa ana mahusiano na wakili mkuu,na nilipogundua nilikuwa nimeshachelewa….na hakuna siku nilipoumia sana kama ile siku niliposikia kuwa alimbaka binti wao wa nyumbani,…oooh, niliumia sana…’alisema.

‘Ni nani alikuambia hilo…?’ nikamuuliza.

‘Aliniambia yeye mwenyewe, siku hiyo nilimkuta alikila, na hakuteka kusema kuna nini kimtokea, nilimdaddii sana na hatimaye akaniambia,….,lakini sijui …maana niliwahi kumkanya yule binti kuwa asimuamini sana huyo jamaa, maana nilimuona anavyomtizama nilipokuwa mle ndani,….huyu jamaa namjua mimi vyema, na bahati mbaya hakuwahi kuwa mume wangu, mimi ningehakikisha kuwa namuweka sawa..’akasema kwa kujiamini.

‘Huyo binti nikamkanya kuwa kama ilitokea hivyo, basi atafute sehemu nyingine, na kama inawezekana aje tushi na mimi, hakukubali, na alisema atajitahidi kujilinda kuanzia sasa, na kila mara namuuliza kuwa je kuna lolote linaloendelea kati yake na huyo jamaa, yeye alikataa kata kata kuwa hana mahusiano tena na yeye, alipobawa mara moja na safari nyingine, alipobembelezwa aliacha kabisa kuwa naye tena….’akasema.

‘Ni kweli kuwa alikuwa kesha acha kabisa kutembea na huyo baba yake?’ nikamuuliza.

‘Hapo nilifanya uchunguzi , na sina uhakika zaidi maana watu wanaishi nyumba moja, na lolote linaweza kutokea…..ila yeye nilipokutana naye baada ya kusikia mama yake akiongea na huyo mumewe,na kuambiwa ukweli kuwa Kimwana ana ngoma, huyo binti alichanganyikiwa kabisa….’akasema.

‘Huyo binti ilikujaje mpaka akakuambia  kuwa alisikia hayo mazungumzo?’ nikamuuliza.

‘Nikuambie ukweli kama isingelikuwa mimi  ,huyo binti angelishaondoka hapo nyumbani, na huenda angelishajiua, mimi ndiye niliyemfundisha ujasiri, na nikamfundisha mazoezi ya viungo kwa jili ya kujilinda, na hata kutumi silaha…’akaniambia,

‘Kwanini umfundishe hadi kutumia silaha,ulikuwa na mipango gani na y eye?’ nikamuuliza.

‘Najua utasema hivyo kuwa labda nilimfundisha kutumia silaha,nikiwa na mipango fulani na yeye au bila yeye kujua, lakini sikuwa na mipango yoyote na yeye….hili ulielewe kiukweli. Wakati namfundisha kutumia silaha, nilimfundisha kwasababu tu nilimuona akiwa muoga wakati risasi inapolia kipindi kile tulipokuwa pamoja kama familia ya wakili mkuu, tukienda kuwinda,….’akasema na kutulia kidogo baadaye akasema;

‘Mimi nilitaka tu kumuondoa huo uwoga, kwa kumfundisha kuitumia hiyo silaha kwa nia njema kabisa, na baadaye ndipo nikagundua kuwa kumbe ana kipaji cha kutumia silaha…kipaji cha kulenga shabaha….’akasema.

‘Ulisema kuwa ulipokutana naye siku ambayo, alikuambia kuwa alimsikia mama yake akimkanya mumewe kuwa asitembee na Kimwana, kwa vile imegundulika kuwa Kimwana ameambukizwa ukimwi, ulimkuta kachanganyikiwa, ulimasaidieje katika hali hiyo….maana natumai wewe kama nesi unayajua mambo hayo vyema, ulitakiwa umchukue akapime….au sio?’ Nilimuuliza.

‘Pamoja ya kuwa mimi ni rafiki yake wa karibu, lakini huyo binti ana tatizo,…nahisi hivyo…nafikiri ni kutokana na maisha yake huko alipotokea, ….yeye mwenyewe anadai kuwa ana mashetani…..ambayo humsaidia na kumkinga na matatizo, na hata siku aliyobakwa na huyo baba yake wa kufikia aliambiwa akapuuza,….na kuna mengine anadai akikanywa hivyo hivyo akapuuzia, …..matokea yake alikiona cha mtema kuni, na akaniambai kuwa kuanzia sasa hatapuuza tena maagizo yao…’akasema.

‘Alisema kuwa aliambiwa kuwa kama atapima,  kwasasa, ataonekana kweli kaambukizwa huo ugonjwa, na ili aokoke na hilo tatizo anahitajika kufuata masharti, ambayo ni pamoja na kufika huko kwao kijijini,huko atakutana na mzee mmoja ambaye atamfanyia dawa, itakayosafisha damu yake, kwa kupitia hayo marue rue anayoyaita mashetani, mimi siyajui hayo  mambo….’akasema.

‘Sasa kwanini alichelewa kuondoka,..?’ akauliza.

‘Aliniambia kuwa kuna kazi kaagizwa aimalize kwanza kabla ya kuondoka, na hiyo kazi ni mojawapo  ya 
msharti ya matibabu yake,….’akasema.

‘Kazi gani hiyo?’ nikamuuliza.

‘Unaweza mwenyewe kukisia,…na najua kuwa atakuwa kakuandikia kwenye hiyo barua uliyopewa, …kwani kwenye hii barua yangu kasema kuwa amekupa barua iliyoelezea kila kitu,sijui kwa vipi kakuelezea, …je kuna barua yoyote umepewa?’akaniuliza huku akiniangalia kwa makini.

‘Mimi nashindwa kuelewa, maana kutokana na maelezo yako na tabia yako toka awali, nashindwa kukuamini,inaonekana kabisa kama mlipanga …au ulipanga iwe hivyo, na hata kumuelekeza huyu binti afanye mambo gani ili mwisho wa siku, iwe kwa ajili ya maslahi yako,…kwani hayupo hapa kuthibitisha hayo, na huenda ni wewe uliyemshauri aandike hiyo barua kama ilivyo,…..’nikasema.

‘Mimi sijali kwa vyovyote utakavyowaza wewe…sasa hivi sijali tena lolote, ndio maana nikakuita wewe kwanza,nakufahamu sana, kuwa unafuatilia mambo kiundani, ….sio tu nimekuambia wewe, baadaye haya yote nitayaongea kwa wahusika, mahakamni,kwani sasa nina amani kama huyo binti keshaondoka… cha muhimu wewe ukitaka kuthibitisha hili, jitahidi umalizie uchunguzi wako kwa vidhibiti mbali mbali, na ikiwezekana ulizia watu, wapo watu waliona…’akatulia na baadaye akasema.

‘Watu gani hao walioona,….au…?’ nikataka kumuuliza swali, na yeye akadakia.

‘Wewe ni wakili, na unajua jinsi gani ya kuwapata, siwezi kukufundisha hilo, maana utasema nimewapandikiza mimi, …fanya kazi yako utawagundua…’akasema na wakili mwanadada akatabasamu, kwani hili alishalifanyia kazi, alichotaka kwa huyo nesi ni maelezo yake binafsi.

‘Nlishamwambia huyo binti kuwa asijali, kama kuna lolote limetokea mimi nitajitolea kwa ajili yake, na nilimshauri kabla ya yote, atafute sehemu salama,..kwani hapo anapoishi sio salama tena,… licha ya kuwa yeye alishaniambia kuhusu mpango wake wa kwenda huko kwao,…’akasema na kutulia kwa muda.

‘Kwahiyo unafikiri kwa kufanya hivyo ndio umemsadia, huoni kuwa umemuweka kwenye hatari, ya kushukiwa jambo ambalo halina uhakika ……’nikamwambia.

‘Kwangu mimi nimemsaidia vya kutosha, nab ado nipo tayari kumsaidia,….nachojutia mapaka sasa ni kuwa sikuweza kuisafisha ile bunduki, kuondoa alama za vidole, kama ningelifanikiwa hilo, nisingelikuwa na wasiwasi juu yake, mimi nilikuwa tayari kujitolea kwa ajili yake….’akasema.

‘Hapo sijakuelewa unataka kusema nini…?’ nikamuuliza, nikikumbuka kuwa kwenye ile bunduki kuna alama za vidole, alaam zile zilikuwa hazijagundulikana kuwa ni za nani, na wakili mwanadada, alishaingiwa na wasiwasi na mmojawapo kwenye ile familia huenda aliigusa ile bunduki, lakini ni nani zaidi ya huyo binti Yatima na kwanini hakutaka kusema ukweli, maana alimuuliza, huyo binti akakataa kata kata kuwa hajaigusa hiyo bunduki,…

‘Hilo kabati naliogopa, mimi naogopa sana nyoka…..’alisema huyo binti. Kwahiyo akilini mwake hakuwa na wazo kabisa na huyo binti, kwahiyo hakuahangaika kabisa kama walivyokuwa polisi, na kwa vile wote walishaamini kuwa nesi ndiye muuaji, jambo hilo likawa limeachwa kihivyo. Sasa kwa maelezo ya huyu nesi wakili mwanadada akawa na uhakika wa kile alichokuwa akikiogopa kukifanya.

Alikumbuka siku alipoona ile bunduki, alijaribu kufuatilia kujua imefikaje hapo, na ndipo akagundua kuwa huyo binti Yatima ana mchumba wake, …akamfuatilia mpaka akamjua, na kuongea naye kwa kifupi,hakutaka kujua undani wa mahusiano yao, lakini kwa hali ilivyo, aliona ni muhimu akamshauri huyo kijana akapime.

******************

‘Samhani sana, kwa kuja kwako bila taarifa, lakini mimi ni wakili na naisaidia familia ya wakili mkuu katika matatizo, ni  pamoja na familia yao, akiwemo yule Binti ,….msichana anayeishi hapo kwenye hiyo familia, ambaye nimeambiwa wewe ni mchumba wake, au sio…?’nikamuuliza huyo kijana.

‘Sijui nani kakuambia maana mimi na yeye tulipanga haya mambo yawe siri hadi hapo nitakapojitambusliha kwao, siunajau tena ile familia ilivyo, unaweza ukafungwa, na ukaoze jela…., lakini haina shaka, ..mimi ndiye mchumba wake, na natarajia kujitambulisha hivi karibuni…kuna lolote limetokea…’akasema.

‘Nashukuru kwa kuwa muwazi kwangu, na mimi sina nia mbaya, na hakuna baya lililotokea, ninachotaka kujua ni jambo moja tu, nimeona hiyo pikipiki hapo nje,na najua wewe ulishamfundisha mchumba wako kuendesha hiyo pikipiki, alishaniambia kuwa anajua kuendesha pikipiki, je huwa mara kwa mara anakuazima pikipiki yako?’ nikamuuliza.

‘Ndio….mimi ndiye niliyemfundisha, na katika kumfundisha huko ndio tukazoeana, na niligundua kwua ni msichana mwema, nawezakuishi naye kama mke,…nampenda sana,…kwa vile nampenda na kumjali mara nyingi anaiomba pikipiki yangu, sipendi kumuuzi,ila naogopa sana anapoondoka nayo, hadi akirudi ndipo moyo wangu unakuwa na amani,….’akasema.

'Urafiki wenu ni muda mrefu?' nikamuuliza.
'Ni wa muda, maana kwa vile nipo karibu na wao, wakihitaji kwenda mahali wananipigia simu mimi, na mara nyingi huyu binti akienda, sokoni ananiita mimi, tukazoeana....'akasema huku akionyesha wasiwasi

‘Siku gani alikuazima na kwenda nayo mbali,akachelewa kurudi….?’nikamuuliza.

‘Kwa mara ya mwisho kuniazima ndipo aliponiambia kuwa anakwenda mbali kidogo, na akichelewa nisiwe na wasiwasi, ….kawa hali sikukubali nikasema kama ni mbali nitampeleka mimi mwenyewe, akasema hapana hiyo safari anahitaji kuwa peke yake, akanisisitizia hadi nikakubali kumpa…..’akasema.

‘Alisema anakwenda wapi?’ nikamuuliza.

‘Hakuniambia kabisa,yeye alisema nisiwe na wasiwasi, ana ulinzi nyuma yake,…alisema kuna jambo analifuatilia…’akasema.

‘Ana ulinzi nyuma yake,ulinzi gani huo,…?’nikamuuliza.

‘Yeye huwa anadai kuwa hua ana ulinzi wake wa asili, sijui ni ulinzi gani,….huwa namshangaa sana, anaweza akakuamba jambo ulilolifanya hata kama hayupo, sijui anajuaje, wakti mwingine namshauri awe mnajimu, ….huwa namtania hivyo,ila sipendi hiyo tabia na yeye alisema hana tabia hiyo , na wala hataki kuwa mnajimu…’akasema.

‘Unasema alisema kuwa atachelewa sana , je alichelewa kihivyo, na wewe ulipoona hivyo, ulifanya nini…?’ nikamuuliza.

‘Nilikwenda kwao, kuulizia na nikakuta hapo nyumbani hakuna mtu, niliingiwa na wasiwasi sana, lakini baaadaye alirudi, na kuniambia alichelewa kwasababau ya foleni, na yeye anaogopa sana kupita katikati ya magari….’akasema.

‘Hukumuuliza alitokea wapi kwenye hiyo foleni..?’ nikamuuliza.

‘Nilimuuliza , akasema alitokea Mwenge,…..alipitia Mwenge, akiwa katokea sehemu nyingine ambayo hakutaka kuitaja, na mimi sikutaka kumdaidisi sana…’akasema.

‘Nikuulize kitu kimoja ni muhimu sana….katika maisha ya sasa, ni muhimu sana kupima kabla ya kuingi kwenye mahusiano, je wewe na mpenzi wako mlishawahi kufanya hilo..?’ nikamuuliza na yeye akaonyesha uso wa kustaajabu, akasema.

‘Kwanini nipime, wakati sina mahusiano na mtu mwingine yoyote, na hata huyo binti hatujawahi kuwa na mahusiano naye, ni ucchumba tu, mtu mwenyewe mgumu kama nini kasema hadi tuoane kwanza….’akasema huku akionyesha uso wa aibu,

‘Kupima ni muhimu hata kama huna mahusiano na yeye au na mwingine yoyote nakushauri ufanye hivyo, na umshauri mwenzako, hilo ni muhimu sana,kwa ajili ya misha yenu ya baadaye, nakuomba sana, ufanye hivyo,kwani mimi ni wakili na nawajibika kuilinda ile familia kwa kila hali…’nikamwambia.

‘Mimi nitapima na nakuhakikishia kuwa mimi sina ugonjwa wowote mbaya, na kama inawezekana nataka siku hiyo tuongezane mimi na wewe na nitamshauri huyo binti, tuongozane, maana najua hata yeye hana matatizo…mengine niliyosikia kwa watu siyaamini, kabisaaa..mimi namwamini sana yule binti…’akasema.

‘Wanasema nini hawo watu?’nikamuuliza.

‘Eti baba yake mwenyewe kambaka..haiwezekani, siku niliposikia hivyo, nilitamani kwenda kupambana na huyo mzee, lakini baadaye nilipomuuliza huyo binti akasema ni uwongo, nikamwamini.


**************.

‘Ina maana kwenye huyo barua hajakuelezea vyema,….?’ Akaniuliza nesi.

‘Kunielezea kuhusu nini, …maana kaelezea mengi, na hata hili la mwisho, hakufafanua vyema, na hata hivyo, sikuweza kukubaliana na hisia hizo, nahisi kuna kitu kimefanyika ili kuficha ukweli,….ndizo hisia zangu,….ndio maana nataka kusikia maelezo kutoka kwako wewe uelezee jinsi ilivyokuwa, na naomba uwe ukweli mtupu, ili tumalizane na haya mambo….’nikamwambia.

‘Sawa mimi nitakuelezea jinsi ilivyotokea siku ile Kimwana alipouliwa,na hivyo ndivyo ilivyokuwa, mengine yaliyotokea, yalitokea ndio,…lakini haya ninayokuelezea sasa ni siri niliyotaka ibakie na nife nayo ili mwisho wa siku, ….niweze kumsaidia mtu asiye na hatia,nasema asiye na hatia, kwa vile aliyotendewa jamii haikuona, ila alichotenda yeye inaonekana ni kosa…ni kosa kuua,lakini huyo anayeua wengine polepole, haonekani, na anaua wtu wangi. Nasema hivi mimi nimejitolea kwa ajili yake, hata kama atatokea leo, naomba ….’akatulia na kujiweka vyema.

`Narudia tena, mimi nimeamua kubeba mzigo wake, naomba tena sana kuwa mimi nihukumiwe kwa yale yote yaliyotokea, kwa jili yake, …’akatulia.

‘Mimi nilishaamua nife na siri hiyo ,ili kiumbe huyu asiye na hatia asizidi kudhulumiwa katika maisha yake,lakini naona bado uhai wangu upo, labda ni ili niwe shahidi, labda ni ili nione machungu ya jela, labda ….labda’akatulia na kufumba macho,

‘Ninacho kuomaba kwa sasa ni wewe ukae chini na unisikilize kwa makini usikie nini kilitoea, lakini kilitokea kwasababu ya hayo yaliyotokea nyuma, jamii ikaziba masikio, ikafumba macho, haikuona machozi na kilio cha aliyedhulumiwa, yule aliyeuliwa na huenda kifo chake kikawa cha taratibu, hakionekani,……na kwa vile yeye ni masikini, ni yatima, hana thamani mbele yao.

 Leo hii mtu mashuhuri, katendewa, kwasababu yeye matokea ya kifo chake ni ya moja kwa moja, macho na masikio yamefunguka wameona na wanataka kuhukumu, wanamtafauta muuaji,,….’akasema na huku akiwa kakunja uso kwa hasira, na baadaye akayafumba macho yake tena na kutulia kwa muda…nikajua eehe,….ni yale yale yaliyotokea siku zilizopita….nikageuka kuangalia kama docta yupo tayari,  Lakini nikasikai sauti, ikiongea.

Nilipogeuka nikamuona akiwa kaniangalia kwa yale macho yake ya ujasiri, akasema hivi;

‘Hivi ndivyo Kimwana alivyouliwa…’

NB: Naona nitaandika mambo mengi kwenye sehemu hii, kwani nakimbilia kukimaliza hiki kisa, lakini kila ninapoandika najikuta kuna mengi yalitokea na sijayaweka hewani…..msichoke, tunafikia ukingoni….

WAZO ZA LEO:

‘Hivi wewe mbona wenzako wameinuka, wamejenga,na mlikuwa ofisi moja, ….una tatizo gani?....nilimuuliza rafiki yangu ambaye yupo kwenye ofisi za kodi.
Swali hilo lilionekana kumumiza sana, akasema ;

‘Sasa hivi sipo huko tena, kwasababu zanu binafsi, ila kiukweli ninakumbuka maisha ya ofisini, jinsi wenzangu walivyokuwa wakiishi, wao wakifika ofisini, kazi yao ni kutafuta jinsi ya kupata pesa, mimi nikawa nahangaika na kazi, uaminifu wangu, kufanya kazi kwangu kwa bidii sikuambulia chochote zaidi ya mshahara wangu, na wenzangu wakawa wanajijenga,…je uaminifu wangu na kufanya kazi kwangu kwa bidii hii ndio adhabu yaka….’akasema jamaa yangu huyo kwa uchungu.

Usijali,…maisha ndiyo yalivyo, huenda ni wengi ambao sasa ni wazee, na wanajutia hayo maisha kuwa kama wangelijua na wao wangelifanya hivyo…..lakini ni vyema ufe masikini kwa uaminifu wako, kuliko kuwa tajiri kwa dhuluma, maana dhuluma haidumu, dhuluma huumiza wengi kuliko unavyozania wewe..je hivyo vilio vya hawo uliowadhulumu, unafikiri vitaishia hapa hapa tu….tuogope kuishi kwa kudhulumu,kwani dhuluma ni dhambi kubwa sana.

Ni mimi: emu-three

2 comments :

Anonymous said...

Kama naangalia movie,hongera M3, Ubarikiwa sana.

Anonymous said...

Simply want to say your article is as surprising. The clarity
for your publish is just nice and that i can suppose you're an expert on this subject. Fine along with your permission allow me to take hold of your RSS feed to stay updated with forthcoming post. Thank you 1,000,000 and please carry on the enjoyable work.
Also visit my site ... Phone Counseling