Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, May 31, 2012

Hujafa hujaumbika-45 hitmisho-3




Tukiendelea pale tulipoachia kuhusu kisa cha binti wa kijijini,

Binti huyu aliyeathiriwa na kutendwa, kutokana na kuvunjwa kwa ahadi ya ndoa ya utotoni, ndoa iliyokuwa baina ya Msomali na huyo binti na mshahidi walikuwa Mungu muumba Wa viumbe na malaika wake. Ilikuwa ni ndoa ua utoto, lakini….Haya tuendelee na kisa hiki;

                                                                   %%%%%%%%

‘Hivi kweli niwaulize, kuna ndoa ya utotoni ambayo inaswihi, mimi najua ili ndoa ikubalike ni lazima watu wawe na umri unaojulikana kuwa hawa wamepevuka kiakili, na pia ili iwe ni ndoa ni lazima kuwe na wafungishaji ndoa na pia wawepo mashahidi, …sasa mnapotoka kunitupia lawama mimi kuwa eti ndiye niliyesababisha hadi huyo binti kuathirika kisaikolojia, nashindwa kuelewa,…ikizingatia kuwa wewe ni mwanasheria unayajua hayo yote kuliko mimi…’nikajitetea pale nilipoona wakili mwanadada akitulia.

‘Ndio hilo unaloongea ni sawa, sijakataa,na wala sijasema ndoa hiyo inakubalika kisheria, ila mwenzko aliichukulia kuwa ni ndoa kamili, najua kuwa haikuwa na yale mambo muhimu yanayohitajika kuitwa ndoa, na kwa ujumla haiswihi kuitwa ndoa, ni michezo ya utotoni, lakini nikuulize wewe wakati mnaifunga ile ndoa ulikuwa na dhamira ya kweli kuwa unaoa, au mlifanya kama mchezo tu, ulikuwa ukimpenda kiukweli au ulikumwa mchzo wa kitoto…?’

‘Niseme kiukweli, wakati tunaifunga ile ndoa, nilikuwa na dhamira ya kiukweli kuwa naoa, na baada ya tukio lile, nilimuona kama ni sehemu ya mwili wangu, na hata leo nahisi hivyo, lakini ujana na damu yangu kuchemka, nikasalitika, na niseme …yakatokea yaliyotokea, …..’nikajitetea.

‘Sasa unaona hilo, mwenzako ilikuwa zaidii ya hilo, alijizuia kwa kila hali akijua kuwa ana mume,….toka siku ile,…na siku ile alipokufumania akajua umehini ndoa, na akaathirika kiukweli, na ndio chanzo cha matatizo yake ya kiafya hadi leo hii..

‘Una maana gani kusema hadi leo hii, kwani una habari zake, kuwa yupo wapi, …?’ nikajikuta nauliza

‘Usiwe na pupa kwani sio wewe peke yake unayetaka kujua hayo , nataak kila mtu aelewe hatua kwa hatua, ili mwisho wa siku muone athari zinazotokana na kusalitiwa katika `kupendana’husuani kwenye ndoa.Tujue kuwa sio wote wenye uthabiti wa kuvumilia matatizo, ndio maana unaona wengine wakipata matatizo kidogo tu wanaathirika na wengine wanadunda, hata iweje, ni hula na maumbile ya kibinadamu.

Tukirejea pale tulipoishia kuwa binti huyu kila akipata mchumba, ndoa hiyo inakuwa haifungiki, ama kunatokea ajali au matatizo ambayo yanaisimamisha hiyo ndoa.Na haikutoka mara moja, ni zaidi ya mara tatu,….Hutaamini hayo, lakini yalitokea kwa huyu binti,na ukianglian sana inapotokea hivyo, anayeathirika sana akilini ni nani….mara nyingi anakuwa ni mwanamke…hayo ni maumbile

Kwa mtizamo huo na maneno ya yule mtaalamu wa mwanzo wa sili, na histora ya matatizo yake ikaonekanahivyo,  kwa hawa wazazi na pia kwa jamii na wanajamii waliobahatika kulijua hilo tatizo kuwa kweli huyo binti anatawaliwa na huyo jinni mahaba. Hapa muwe makini,muone jinsi gani hawa wataalamu wanavyojua kuzichota hisia za watu kisaikojia, sio kwamba na wapinga, lakini sio kweli kuwa wote wapo sahihi kwa yale wanayoyasema.

Wazazi kusikia hivyo,wakaamua kulifungia kazi hilo tatizo, kwa wataalamu ,huku na kule, na kila wapofika wimbo ni huo huo, ….mtoto wenu ana meshetani, anatawaliwa na jinni, ….je ni nani hataacha kuamini hayo, hasa kwa wazazi wa binti,.., zaidi ya wataalmu sitawote wanasema kitu hicho hicho,wakajua ni kweli, sasa wanatakiwa kuliondoa hilo shetani,..wafanyeje.

Kwanza walifuata hayo waliyoambiwa na wataalamu wa kiasili , dawa za kufukiza, sijui maji ya baharini, kuku mwekundu,…vitu vingi tu, ….lakini wapiiiii….tatizo likawa linajirudia ingawaje si mara kwa mara ila ni pale tu inapofikia huyu mwanadada kapata mchumba au rafiki wa kiume. 

Basi wazazi wakaona hilo sasa tuwaendee watu wa dini, wakawatafuta waombezi wa kidini, wakaombewa, na wao hawakuchagua dini gani, kila wanayemuona ni mtu aliyesomea dini na anajua jinsi gani ya kumuombea mgonjwa aliyeathirika na mshetani, wanamuomba atoe msaada huo.,….imani ni kitu cha pekee yake na mungu hamtupi mja wake, baada ya maombezi hayo, hali  ilionekana kuwa imetulia, lakini sasa likazuka tatizo jingine.

Kila mwanaume aliyakutana na huyo binti, akampenda, wakakubaliana na hata kufikia hatu ya kujimbulisha kama wachumba, mwanaume huyo akirudi nyumbani kwao kutoa taarifa, akiulizwa na mwanamke gani, akamtaja huyo mwanamke, naambiwa wewe, unataka kufa na jinni mahaba, shauri lako, angalai wenzako, mtoto wa nani na anni wako wapi sasa,…achana naye , wanawake wapo wengi, katafute mwanamke mwingine usiingie kwenye balaa….

Basi ikawa mkosi kwa binti huyu, wanaume wengi, wakawa wanamuogopa, na hali hii ya kunyanyapaliwa, ikamuathiri zaidi, akajiona ni mwanamke wa mikosi,  kuwa yeye sio mtu wa kawaida,..na kuanzia hapo, akawa hataki urafiki na wanaume, chuki ikajijenga akilini,  na hasira kwa wanaume  ikazidi.

Chuki hiyo ilikuwa kwa wanaume wote,na wakati huo, akili yake haikuwa ikitambua kuwa chanzo cha yote hayo ni athari iliyojijenga akiwa msichana mdogo, kuwa yeye bado nafsi yake ipo kwenye pendo la mwanzo, pendo lake na mvulana wa utotoni na ujanani ambaye ndiye aliyeathiri akili na nafsi yake….

‘Mume wangu, mimi naona tuhame kabisa hapa, maana kwanza biashara haiendi vyema, pili, binti yetu anaathirika kisaikolojia,turudi kwetu, ama kijijini au mahali pengine , ambapo watu hawajui lolote kuhusu binti yetu….naona anateseka sana’akasema mke.

‘Hilo wazo lako sio baya, hata mimi nilishaliwaza hilo, sio kuliwaza tu, bali nilishawasiliana na ndugu yangu anayeishi huko Dar, ana jengo lake lipo sehemu nzuri ya kibiashara, tutahamisha baadhi ya shughuli zetu na nyingine zitaendelea kuwepo hapa, …bado mambo machche ya kisheria kama leseni lakini hilo litakamilika hivi karibuni….’akasema mume.

‘Je na huyu binti yetu kuhusu kazi yake ambayo keshaianza hapa itakuwaje?’ akauliza mke.

‘Hilo nalo nimeshalifanyia kazi, kuna nafasi nyingi zakazi za madakitari huko Dar, na ni swala la yeye kupeleka vyeti vyake hukoo na barua ya maombi, atapata kazi hilo halina shida…sisi tuanze tu kujiandaa.
Na binti yao akafahamishwa, na yeye hakuwa na pingamizi, na safari ya kuja Dar ikakamilika


Sasa turejee kwa familia ya madakitari, familia ambayo baba, mama na watoto wote walibobea kwenye fani hii ya udakitari, na hata kufikia hatua ya kuanzisha kliniki yao, na sio kliniki tu,bali kikawa chuo cha kufundisha madaktari au watu  waliotaka kujua maswala ya kimaumbile,hulka na hisia hasa katika maswala mazima ya mahusiano, huku kwetu tunaita kufundwa, wao waliyaweka kitaalamu zaidi.

‘Unataka kuoa au kuolewa, una matatizo ya kindoa, una matatizo ya uzazi, una matatizo ya kifamilia na mengine mengi, fika kwa kliniki ya mama Docta, …’ hilo ni moja ya tangzao lao, ukifika huko Kenya utalikuta.

‘Unasema Mama Docta,ina maana ni yule mama aliyetoroka hapa nchini…..?’ nikauliza huku nikiwa nimewaka kwa hasira.

‘Hebu nikuulize swali, huyu mama aliyetoroka hapa ana umri wa kuweza kuzaa watoto wakubwa wakuolewa…jinsi ulivyomuona wewe?’ akauliza wakili mwanadada.

‘Hapana ,…yule mimi nilishakutana naye, hana umri huo,licha ya kuwa anavaa miwani mikubwa na nywele zake ni nyingi, nafikiri ni za bandia, ..huwa kama akaficha sura wakati wote, lakini ukimwangalia kwa karibu,sio mtu mzima wa kuwa na watoto wakubwa kiasi hicho,,maana mwanamke aliyezaa mabinti waliofikia umri wakuolewa,hajifichi….’akasema mkuu.

‘Sasa… mbona hapo mnanichanganya, hebu endeelea tusikukatize…huenda nikapaat jibu…’nikasema.

‘Ndio maana nawaomba mnipe nafasi,maana mimi nimelifanyia hilo utafiti wa kina, najua kila kitu, kuhsu hawo watu, mkianza kunikatisha-katisha, nitalipua lipua na hamtaelewa vyema….’akasem wakili mwanadada.

‘Haya endelea…’nikasema huku nikajaribu kumkumbuka huyo docta mama, sikuwahi kukutana naye uso kwa uso, nilikuwa namuona kwa mbali tu….

Ukumbuke kuwa ndani ya kliniki hii, pia alipitia binti ,aliyekuwa mchumba au mke wako wa utotoni, na hapo ndipo alipopatia mafunzo  mazuri ya uzazi, hulka za kimaumbile, na ukichanganya na fani yake ya udakitari, basi akaamua kuusomea kabisa udakitari  bingwa wa matatizo ya kina mama , na kwa vile alishaanza kutibu hapo, kusaidia na hata kufundisha wengi wakawa na yeye wanamuita mama-Docta.

Kwa jinsi alivyofaulu, na kuweza kufikia kiwango cha hali ya juu, katika kliniki hiyo, au chuo hicho,wenyewe waliamua kumchukua kabisa awe mmoja wa dakitari wao, au mwalimu wa chuo hicho, lakini mara ikaja hiyo hoja ya kuhama hapo Kenya na kuja huku Dar,ikabidi asamehe kwanza hiyo nafasi, kwani hata yeye alishachoka na hali iliyopo hapo, kila mtu anamnyoshea kidole yeye, kuwa ni mke wa jinni mahaba.

Yeye mwenyewe baada ya kusoma sana na kupata mafunzo hapo, na kukutana na mama mtaalmu mwenyewe,akajijua kuwa sio mambo ya mshetani kama wanavyojua watu, lakini ni athari za kisaikolojia na hutaamini huyu mwanamama alikuja  hata kulifichua hilo, katika kumsaidia huyu binti, alichimbua historia ya huyu binti ahdi akagundua chanzo cha matatizo hayo ni nini …nakweli huyo binti akakubaliana na huyu mama kuwa kweli  chanzo cha hayo yote ni athari za yale yaliyojijenga akilini mwake akiwa mdogo,..

‘Sasa nitaondokaje na hili tatizo ,nifanyeje mama docta…?’akamuuliza huyo mama.

‘Kwani inavyoonekana bado akili yako inampenda huyo mtu, lakini kwa yale uliyoyaona na kwa jinsi ulivyokuja kuona kuwa huenda mwenzako alikuhadaa, mapenzi kwako yakaanza kuingiwa na wivu, na chuki za kutaka kulipiza kisasi, ….inawezaisiwe kwa kutumia nguvu, lakini kwa kutaka kumuonyesha yeye kuwa ni mbaya, akili ikawa inahagaika kutafuta njia,..na ikiwezekana umrudishe katika iel hali mliyokuwa nayo, akili imekuwa ikimtafuta,….mwili hautaki…kunatokea mgonganoo hapo, ‘ akasema huyo mwanamama.

‘Nakushauri kama  inawezekana jitahidi ukutanae na huyu mwanaume,au tafuta mume ambaye ataweza kuteka nfsi yako,akuoe,..mume ambaye ataweza kukusahaulisha hayo yote yaliyojijenga akilini mwako, muelewevu…..’akapata huo ushauri na kila mara alijaribu kukutana na huyu mwanamama,na kwakuw akaribu naye sana, na hata aliposema anaondoka,mama yule alimuomba sana abakie, lakini haikuwezekana.
Naomba tuwe tunawasiliana, na kama ukibadili mawazo, nitafurahi sana,na ikibidi tunaweza tukafungua tawi huko Dar, nipi mbioni kwahilo….

******

Tukija kwenye familia yetu hii ya madakitari, ukumbuke kuwa binti mmoja alijiengua ndani ya family ahiyo mapema, na kuja kufanya kazi  huku Dar, na ushawishi huo ulitokana na urafiki uliokuwepo kati ya binti huyu na mavulana toka Tanzania, ambaye walikutana huko chuoni walipokuwa wakisoma Ulaya. Ingawaje walikuwa wakisoma fani tofauti, lakini wakajikuta wakipendana…..

Na wazazi hawakuwa na pingamizi maana siku hizi watoto wakikutana popote, na wakapendana, hakuna udadisi tena wa family ahiyo ipoje, kuna matatizo gani ya kurithi, hayo wanasema kuwa yamepitwa na wakati, ….wazazi wakabariki uchumba huo, na ilipifika sehemu wazazi wanataak kukutana, ikawapeleka wazazi wa binti kusafiri hadi nyanda za ziwa. Nia na lengo ni kujua wapi huyo mvulana anatokea.

Walipofika huko, wakajikuta kumbe asili yao ni moja. Maana familia hiyo ya madakitari,asili yao ni huko huko mikoayaziwani,Tanzania, ila wazazi wao walihamia huko Kenya muda mrefu na wakazaliana huko Kenya kukawa ndio nyumbani.

Ikawa ni shangwe wenyewe walisema ng’omba karudi zizini. Basi, ndoa ikahalalishwa na kufungwa ndoa ya kifahari, baada ya ndoa bwana yeye alikuwa akifanyia kazi Dar, na ikabidi amfanyie mipango mke wake na yeye akafanyie kazi huko Dar, na hapo ndipo maisha yao yalipoanzia…

‘Mimi nataka tuwekane wazi, unakumbuka wakati tupo chuoni, kuwa mimi sitaki mambo ya kuchungwa, amri za ajabu ajabu,mimi nakuhakikishia kuwa nakupenda, na sitakusaliti kamwe, na na wewe nataka iwe hivyo hivyo, nakuomba sana, tuchunge misingi ya ndoa, na kama kuna tatizo tuambiane,mimi najua sana maisha ya ndoa kinadharia na najua mengi katika mwaswala ya mahusiano, tutasaidiana ukiwa muwazi kwangu,….’akasema mwanandoa huyu.

‘Kwani una wasiwasi gani na mimi,…mimi nakupenda, na kilichonifurahisha ni kuwa unajua mapenzi,ila mimi ni mume wako,…unatakiwa utii amri za mume wako, na sio ujiwekee mashari yako,haiji namna hiyo….unajua mila na desturi zetu zilivyo,…..mume ndiye kichwa cha familia, usiniletee mamabo ya Ulaya hapa….’akasema kiutani, lakini kumbe moyoni mwake, haikuwa ni utani.

Bwana huyu kila akikutana na wenzake, ambao walitoka pamoja huko kijijini wakawa wanamcheka kuwa katawaliwa na mke,anafugwa,wenzao wanandoa lakini wana uhuru, wanakutana kwenye mabar, wanakunywa ,wanabadilishana mawazo, …..yeye kila mra yupo nyumbani, kusaidina na mkewe kupika, wakawa wanamzihaki, na kweli kauli na maneno ya wenzake yakaanza kumteka akilini, akaona hayo maisha anayoishi na mkewe, sio sahihi,hatayaweza, akaanza kubadilika….

‘Mume wangu unatatizo gani….’akaja kuulizwa na mkewe,ambaye ni dakitari, dakitari anayejua mambo hayo, lakini wahenga walisema kinyozi hajinyoi, na penye miti hapana wajenzi. Mume akaanza kujenga dharau, mkeatakufundisha nini,mke anajua nini…

‘Mimi sina tatizo,…..kwani kuna shida gani,…?’akauliza huku akiwa kakunja uso kiaskari.

‘Naona mabadiliko,huwi karibu na mimi tena,na huo mtindo wakunywa pombe kupitliza umeuanzia wapi, hebu niambie una tatizo gani ili niweze kukusaidia….’akauliza mke.

‘Nimeshakuambia sina tatizo,….kwani wewe unataka nini,mimi ni mwanaume,natakiwa niwe huru,sio kufundikwa ndani kama mwali,…..unanielewa,…na kazi yangu ilivyo, nahitaji kuwa hivyo,..usijifanye kwavile ni dakitari unajua kila kitu,kwangu hujui kitu kuhusu ndoa….’akasema kwahasira na kuondoka,…

Mambo yakaanzia hapo…..

Ni mimi: emu-three

2 comments :

Precious said...

mambo yanazidi kuwa matamu... leo umetuonjesha tu.

Rachel Siwa said...

Duuhh Hongera sana Ndugu wa mimi,nafurahi mnoo kuona kazi inaendela vyema, Mungu azidi kukubariki kila iitwapo leo.Pamoja daima ndugu wa mimi!!!!!!