Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, March 23, 2012

Hujafa hujaumbika-9




`Mtoto wa Msomali.....’ Nikasikia sauti ya kiaskari ikiita.

‘Nipo afande....’nikainuka haraka na adabu tele, huku nikipangusapangusa macho ynagu, ili niweze kuona vyema,maana hapo kidogo ka-usingizi kalishaanza kuniteka, kwani jana sikuweza kulala kabisa, mbu walikuwa hawatupi nafasi, kila mara `nataka, nataka..’ achilia mbali kunguni ambao hawasemi `nataka’ wao wanachukua tu.....

Kuna wengine, sijui miili ao ikoje, wao walikuwa waankoroma usiku kucha, wanauchaoa usingizi utafikiri wapo nyumbani, na hawo mbu wakiwafaidi, na kunguni wakiwanyinya na kutapika....lakini mimi nilishindwa kabisa kupata usingizi..

Jamani jela sio mchezo pasikie tu hivi hivi, naona tukipita maeneo ya Ukonga makonda wanapenda kusema j`wale wa jumba la dhahabu, wewe .....achana na huo usemi,...jumba la dhahabu, .... maana humo ni mateso, ambayo hata akikusimulia aliyewahi kuingia humo hataweza kuyamaliza....sasa fikiria sisi tulikuwa mahabusu tu,hayo mateso tuliyopata ni nusu tu ya huko... je hao ambao wanatumikia kifungo inakuwaje..

Na kuna ambao wanatumikia kifungo bila kosa, huwezi amini hilo , lakini wapo, kwasababu moja au nyingine wamejikuta wakikutana na matatizo ya kubambikiwa kama ilivyokuwa kwangu, sikuua, lakini sasa nimeshikwa kwa kusadikiwa kuwa nimeua, ....oh, niue mtu,mbona nitajinyonga hata kabla sijakamatwa.....siamini, lakini ndio hivyo tulisubiri kesi, maana kama ilivyosemwa bado wapo kwenye uchunguzi.

‘Kuna mgeni wako huku, ...’akasema afande na kuja kufungua mlango, mlango wa chuma, maana sisi hatuaminiki tena, tunalindwa kwa mtutu wa bunduki, sisi sio raia wema tena, hatuhitajiki kukutana na raia wema wa mitaani mpaka kwa amri na ulinzi mathubuti, na unatakiwa kutii amri, na ukiitwa uitoke kwa adabu, la sivyo, mateso ya jela,au mahubusu utayaona kwako aheri ya kifo.

Nilisogea pale mlangoni nikiwa na hamasa ya kumjua huyo mgeni wangu ni nani, na moyoni nilikuwa nikiomba awe mtu ambaye atanipa habari njema kuwa dhamana imekubaliwa,na asiwe mtu wa kuja kunisanifu, ....maana wengine wanakuja hapo kuhakikisha tu kuwa kweli umefungwa na mwisho wa siku anapata cha kuahdithia huko mitaani.

Kwa mbele yangu nikamuoana jamaa kakaa na mkoba wake, akiwa kainama akisoma makabrasha yake,moja kwa moja nikajua ni wakili ambaye mjomba alisema anamtafuta, nikawa na hamu ya kusikia nini alichofanikiwa, na hasa kusikia kuwa dhamana imekubaliwa na leo hii natoka, sikutaka kupitisha usiku mwingine kwenye chumba hicho, ambacho hata hewa ya kuvuta angalau hata iwe chafu, ni adimu.

‘Pole sana ndugu yangu ....nimekuja kukupa habari kuwa mimi ndiye wakili wako, na nimeshaanza kazi, licha ya kuwa kuna vikwazo vya hapa na pale, lakini kila kitu kinachohitajika kwetu tumeshakamilisha, tatizo ni kwa huyo hakimu, sijui anataka nini zaidi....lakini leo nitapambana naye, usitie hofu....’akasema huyo wakili.

‘Ndilo hilo lililokuleta au kuna jingine...?’ nikauliza na kumfanya aniangalie kwa mashaka.

‘Kwani sio muhimu hilo, najua unavyojisikia, lakini kila kitu kina utaratibu wake, na hata hivyo najitahidi kufanya niwezalo ili dhamana ikubaliwe, na mambo mengine pia yakiwa yanaendelea,ujue ni kesi ya mauaji, nakesi kama hizi ni ngumu, kila mmoja anajaribu kuhakikisha kila kitu kinakuwa katika mpango uliokubalika, vinginevyo unaweza ukashindwa kwasababu ya vipengele vidogo tu...’akasema huku akifungua fungua makabrsaha yako.

‘Sawa nimekuelewa,kama hakuna jingine, nashukuru kwa kuja kunitembelea....’nikasema na kuinuka.

‘Bado hatujamalizana, maana kama wakili nahitajika kujua mengi, kama nilivyosema, huku nafuatilia dhamana, lakini pia natakiwa kujua zaidi kutoka kwako kuwa ilikuwaje,ili niweze kujenga hoja ya msingi, ...’akasema

‘Hujaongea na mjomba wangu, hajakuelezea nini kilitokea....hujaweza kujua nini cha kuongea, hoja ipi ya msingi, waakti hata polis wanajua kuwa ni kosalakubambikiwa....?’ nikamuuliza huku nikipiga miayo ya usingizi.

‘Kanielezea mjomba wako,..., lakini nihitaji maelezo zaidii kutoka kwako, na kukuweka sawa, kwani ni vyema zaidi....ujue kila utakachoongea ni ushahidi, na sitaki uje uongee kinyume na itakiwavyo, kutoka sasa, mimi ndiye natakiwa nikuongoze nini cha kusema, ...na nakushauri hata wakikuhoji nini usiongee lolote mpaka niwepo....’akasema wakili

‘Hata ukitaka niseme, kuwa nimeua kweli, nisema hivyo hivyo.....unafikiri mimi mjinga eehe, ndugu yangu, ulishawahi kufungwa mara moja, ulishawahi kuweka sehemu kama hizo...’nikamuonyeshea kule tunapolala,...na wakati huo ndoo ya kinyesi ilikuwa ikitolewa na baadhi wa wafungwa, nikashukuru kuwa nimetolewa mapema kuongea na huyu jamaa, la sivyo huenda mimi ningepewa hiyo kazi ya kubeba ile ndoo ya kinyesi.

‘Kama nilivyosema awali, kuwa tutahakikisha kuwa dhamana inapatikana... , na hilo ndilo nalifuatilia, ndio maana nipo hapa asubuhi na mapema nikitoka hapa naenda kuonana na hakimu, lakini kuna maswali machache nataka kukuhoji, ili nikionana na hakimu, niwe na msingi imara....ndio kanihadithia mjomba wako, lakini yapo mengine unayajua zaidi kuliko yeye..na nahitaji nikuhoji mwenyewe nisikie kauli yako.’akasema wakili

‘Kama yapi...hayo maana naona kama unalalia upande wa polisi, unahisi labda kweli nimeua...., hebu niulize hayo maswali, maana sikuamini....na sizani kama utaweza kunisaidia kitu, naona mjomba kanitafutia mgeni wa kunitembelea,sio wakili, mimi nilijua unafika hapa kuniambia, unatoka sasa hivi, kumbe ndio bado unatafuta cha kwenda kuongea na hakimu....' nikamwangalia kwa dharau na kabla hajaniii kitu nikaongezea kwa kusema;

'Mimi kila kitu nimeshamwambia mjomba...mdomo umechoka kabisa kuongea, mwili umechoka kusulubiwa na kichwa kimechoka kufikiri, sina lakuongea zaidi.

‘Je ulipotoka pale na huyo binti, ulikuwa na silaha yoyote...?’ akaniuliza.

‘Silaha ipi,.....kwasababu pale nje niliona panga wakati naingia ndani,....ndilo nililoingia nalo ndani, nikamtishia nalo huyo mbakaji....kwa kumpiga na ubapa,sio kwenye makali....akatoka na kukimbia, akiwa hana jeraha hata moja, ....na tulipotoka pale, nililiacha hilo panga mle ndani sikuondoka na silaha yoyote...’nikasema.

‘Marehemu kafa kwa kukatwa na mapanga, na usemi wako unasema ulikuwa na panga ndani..na panga hilo limetafutwa ndani halipo, ..hapo polisi wanatia mashaka, ndio maana wanakuhisi kuwa ulimkata huyo mrehemu na hilo panga...’akasemawakili.

‘Hebu jiulize, kama ningelimkata na hilo panga, damu sizingeonekana, kutoka hapo nyumbani hadi huko alipofia...?’ nikamwambia huku nikimwangalia kwa makini.

‘Hilo wameliongelea pia, lakini bado wanasema, huenda mlikimbizana hadi huko porini, na hapo ukaamua kumkata na panga...’akasema wakili.

‘Kuna watu wanasema wameniona nikiingia, na wameniona nikitoka na huyo binti kweli si kweli, je walisema kuwa waliniona nikikimbizana na huyo jamaa?’ nikamuuliza.

‘Hawo waliokuona ukiingia, wanasema hawakukuona ukitoka, na pia wanasema hawakumuona huyo marehemu akitoka humo ndani....hakuna aliyekiri hivyo...., ina maana matendo hayo yalitokea wakiwa hawatizami, au walikuwa wameondoka hapo....polisi wanahisi kuna jambo jingine zaidi na wanalifanyia uchunguzi, na hoja yao mpaka sasa ni kuwa hawataki kukuachia kwasasa maana unawezaukaenda kupoteza ushahidi na pili ndugu wa marehemu wametishia amani yako....’akasema wakili.

‘Hiyo sio hoja ya msingi....je mapanga, au panga lililotumika kumua huyo marehemu yamepatikana, .....na hilo panga nililoliacha mle ndani limeonekane...?’ nikahoji.

‘Wauwaji hawakuacha hayo mapanga, ina maana waliondoka nayo....hoja ya msingi ya polisi ni kuwa wewe umedai ulimpiga marehemu na ubapa wa panga, na merehemu kafa kwa kukatwa na mapanga....unaona hapo ilivyo...lakini hawana uhakika na ushaihdii wao, ndio maana bado wanasema hawajakamlisha uchunguzi wao, na mimi hapo ndipo nitawapiga changa la macho..hiyo kesi ndogo tu...’akasema wakili.

‘Kesi ndogo wakati nateseka huku rumande bila kosa, kama sitaweza kutoka humu leo , sikuhitaji tena, nitajitetea mwenyewe..kwasababu nina uhakika sina kosa..., naomba tu,umtete huyo binti wa watu maana yeye kaingizwa kichwa kichwa, asije akasema karuka mkoja kakanyaga mavi...’nikasema.

‘Huyo leo leo anaweza kutoka, ....’akasema wakili.

‘Hapo umenena jambo la muhimu...’nikasema huku nikiondoka.

‘Kazini unahitajika lini...?’akaniuliza wakili huku akiinuka makabrasha yake na mimi bila kugeuka nikasema.

‘Kama litakusaidia kwenye hiyo kesi, ...wiki ijayo...’nikasema huku nikijitahidi kupikicha macho maana macho yalikuwa mazito kwasababu yausingizi.


************


Mchana uliingia kama mchezo, na kikafika kipindi ambacho kila mwenye mgeni anaruhusiwa kuonana naye, na wale walioletewa chochote wakawa wanakula., mimi sikuwa na hamu ya kula kabisa...na mara akaja Yule wakili akiwa kaongozana na binti Yatima.

‘Oh,kaka pole sana,....tangu jana nauliza nitakupataje lakini hawa maaskari wakawa hawanijibu, na sikuweza kulala, nilikuwa nakuwaza wewe...sijui walivyokupiga wamekuumiza sana...’akasema binti Yatima.

‘Aheri wangeliniumiza tu, ili nikalazwe hospitalini, kuliko kulala pale sakafuni, maana hewani mbu, sakafuni kunguni na chawa....usiombe, ...sikulala kabisa, hadi huu mchana, na kila ukitaka kupata usingizi kidogo, mara kaja mgeni, mara mnatakiwa huku...yaani ni taabu...lakini usijali yote haya ni kwasababu nakupenda....’nikasema bila kujali watu waliopo.

‘Nashukuru kusikia hivyo kuwa hujambo,mimi nimezoea maisha ya shida, ingawaje hapa unakuwa huna uhuru zaidi, lakini maisha yangu yote yamekuwa kama hivi, nimelala sana sakafuni sana, kunguni ,chawa ni mrafiki zangu, ....nimenyanyaswa,nimeishi maisha mabaya zaidi ya haya ya jela, kwahiyo sioni tofauti,labda ya kupta hewa ya nje....’akasema Yule binti.

‘Huyu tumeshakamilisha kila kitu,na kaja hapa kukuambia kuwa dhamana yake imashapita, na baadaye ataruhusiwa, na kahitaji sana muongee na y eye kabla hajaondoka hapa...’akasema wakili nay eye akaondoka kutuacha tuongee.

‘Sema mpenzi,maana hawa watu hawatutakii mema, muda kama huu tungelitakiwa tuwe kwenye harusi, au fungate...?’ nikasema baada ya wakili kuondoka, na binti Majuto akiniangalia kwa makini.

‘Mimi nikitoka hapa nataka niondoke kabisa hiki kijiji, kuna ndugu wa upande wa mama, ambapo nilikuwa nikiishi na bibi aliyenilea awali ...nataka nikaishi huko huko, sitaki tena kuishi nyumba hiyo ya mateso...’akasema binti.

‘Huendi popote, ukitoka hapa nenda ukaishi kwetu, wewe sasa ni mchumba wangu, ...na nipo tayari kuhakiskiha kuwa unaishi kwa amani na usalama,....kwasasa usufikiria kabisa kwenda hukoi, na kwanini ukimbilie huko..?’ nikamuuliza.

‘Naogopa mama atarudi na kunifanya lolote, siamini maisha yangu nikiishi hapa tena, ...kwasababu baba mawazo yake yote kwa huyo mkewe.....na kama unataka kunioa utaniolea huko, sio hapa....’akasema binti.

‘Sikiliza binti, huamini kuwa nataka kukuoa,au ..ngoja nina wazo moja, leo hii, au kesho tutafunga ndoa, hilo linawezekana, nitamuomba mjomba, aje na baba yako, na wafungisha ndoa, tufunge ndoa, ili upate uhuru wa kuishi kwetu, je hilo unalionaje....?’ nikasema na binti Yatima , kwanza akaniangalia kwa kutoamini, na pili kwa mshangao,machozi yakaanza kumtoka, ....sikumuelewa kwa kweli, ni kwasababu ya furaha au ni kwasababu gani..

Jamani natamani kuendelea lakini muda umekwisha. Tuonane sehemu ijayotukijaliwa

WAZO LA LEO: Mtembea bure sio sawa na mkaa bure, kwasababu kwa kutembea kwake anaweza hata akaokota chembe ya mchele...Tujitahiji kuhangaika kuliko kukaa tu, na kuomba, maisha ni kuhangaika, kwani muomba Mungu hachoki,nakuomba sio kwa kuinua mIkono juu tu hewani, ni pamoja na kuhangaika.

emu-three

3 comments :

Preciuos said...

Nimelipenda wazo la leo sana sana.
nakutakia weekend njema M3 na wadau wote wa blog hii

Yasinta Ngonyani said...

Pole sana kuwa gerezani bila kosa...nadhani binti alilia kwa furaha...Nimelipenda wazo la leo. Ahsante...pamoja daima.

emuthree said...

Wapndwa wa ukweli, Precious na dada Yasinta nawashukuruni sana kwa kuwa pamoja nami,pia nawashukuru wote wengine ambao kwa kimiya kimiya tupo pamoja. Mungu awabariki sana