Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, February 23, 2012

Ni nani anayechangia kuvunja ndoa mke au mume-2?




Kwanza nakushuru wewe mwenye blog kwa kuweza kuweka haya matatizo yangu, najua wengi waliopitia hapo wameyasoma na kuyaelewa, na wengine huenda hawaamini kuwa hayo yapo, na hasa ukizingatia kuwa mimi nipo huku Ulaya. Ila ni Ulaya ile ambayo kuna ubaguzi wa rangi usiombe.

Kuna ambao wamejaribu kuniuliza kuhusu maendeleo yangu kielimu,

Nilipofika hapa kitu cha kwanza nilichofanya ni kujifunza lugha yao, kwani ili usome ni lazima ujifunze lugha yao, hapa hawatumii kiingereza au kifaransa, wana lugh yao wenyewe.Ukishamaliza kujifunza lugha yao,unaangalia mwenyewe,kama unapenda kufanya kazi, basi kuna kule kunakoitwa kusomea kazi au kama umeamua kusoma shule basi unaomba kusoma shule.

Kwa nchi kama hii,ninayoishi,kwanza,ukiwa mgeni,kupata nafasi ya kusoma,ni ngumu sana,kama ukienda shule,kuna masomo ambayo,unatakiwa kuyasoma na mengine wanasoma wenye nchi yao…utata unaanzia hapo.

Maana,wanasema kuwa,wageni wamezidi kuwa wengi,kwa hiyo nafasi ya kazi nzuri kwa watoto wao itakosekana, na wageni wanaweza wakajaa kwenye nafasi hizo, kwahiyo wanachukulia kipaumbele kwa watoto wao. Na si wakuja wanatubana tusisome baadhi ya hayo masomo ndio maana wanakuchagulia masomo gani uyasomee. Sio mbaya kama una nia ya kusoma, utasoma , lakini ukumbuke kuwa mimi hapa nimekuja kwa kupitia kibali cha mume wangu….hayo tuyaache kwanza, maana hata mimi mwenyewe yananichanganya…


Tuangalia kuhusu mimi, baada ya kumaliza,kujifunza lugha yao,nikaenda moja kwa moja kujifunza kazi sio kusoma masomo yao wanayotaka wao.. Nilichofanya ni kuomba kujifunza kazi kwenye mojawapo ya supermaket kubwa ya hapa nchini.

Maombi yangu ya kujifunza hiyo kazi yakakubaliwa haraka kinyume na nilivyotarajia, kwahiyo kwa vile sikujua nini kitakachofuata huko, nikiwa na shauku kubwa kuwa nimechaguliwa kwenda kusomea hiyo kazi, nilijiandaa na kujiandaa vya kutosha.

Kesho yake ikafika, nikadamkia kwenye hiyoo supermarket, nikamkuta huyo bosi yupo kazini, akisimamia shughuli zake, kwanza aliponiona tu, akashituka kwanza,halafu akaninyola, kuniangalia toka chini juu, juu chini, baadaye akaniuliza nina shida gani.

‘Mimi ndiye mliyemuita kuja kusomea kazi, ni mmojawapo wa hawo waliochaguliwa kusomea hiyo kazi, kwa vitendo…’nikamwambia.

‘Oh, ndio wewe…basi naona kuna makosa, ….samhani, sikujua kuwa wewe ni mweusi, …..’akasema na kuniita tukaonane ofisini kwake, sikuelewa kwanza kwanini alisema, hakujua kuwa mimi ni mweusi…..

Tulipofika ofisini kwake, akasema; ‘Oh samhani sana, ninasikitika kuwa sikujua kuwa wewe ni mwafrika , mweusi, kwahiyo samahani naomba urudi nyumbani tu, maana nafasi hiyo kwa mtu kama wewe hakuna, ningeliweza kukupatia hiyo nafsi ya kuuza tu kiubinadamu…., lakini, utanifukuzia wateja wangu….’akaniambia na mimi nikabakia mdomo wazi sikuamini hayo maneno, ina maana ngozi yangu haipendwi na wateja, hili nilikuja kulijua baadaye kuwa ngozi yetu inachukiwa, inabaguliwa sana.

‘Unajua wengi wa wateja wetu ni wazee,na wazee hawa hawapendi ngozi nyeusi, kwa hiyo siwezi kuwapoteza wateja wangu kwani mwisho wa siku nitafunga duka, na kisa ni wewe ngozi nyeusi,….’akaniambia huku akiniangalia juu hadi chini na akizungumza kuhusu ngozi yanu bila kuona aibu. Nilijiskia vibaya, nilitamani nimpasulie yale yaliyojaa moyoni mwangu, lakini nikavumilia tu.

Nikarudi nyumbani na kumuelezea mume wangu, ili kama kuna sehemu nyingine nikajaribu. Mwenzanu alichukulia hicho kama kigezo cha kunifanya mfungwa, kwanza alikasirika kutokana na hiyo lugha au tabia ya kuzarauliwa….sisi waafrika, na hili sio yeye tu hata mimi, lakini kwake ilikuwa kama kisingizio kingine.

Na pili, akaona haona haja kwa mimi kufanya kazi, kwanza kama alivyosema mimi ni mwanamke, na mke wake, nastahili kukaa nyumbani na kumfanyia kile anachotaka yeye. Kwa mara ya kwanza nilimkubalia ingawaje moyo wangu haukutaka hivyo, nilikuwa nataka kufanya akzi ili tuweze kuinua kipato chetu, na huku Ulaya sio kama nyumbani, gharama zake ni kubwa, kuna kodi, kuna madeni mengi unabambikiwa hata hujui ni ya nini…..

Basi mambo yakaanzia hapo nikawa kibarua , mfanyakazi wa nyumbani, …hilo kwangu sikulijali sana, lakini kama mimi ni mfanyakazi wa nyumbani nastahili haki zangu, nastahili haki ya mke wa nyumbani, sio zarau, sio kunyimwa hata uhuru wa kutoka nje, ….hayo mume wangu hakuyatambua, na baya zaidi , hata haki ya ndoa nanyimwa, hutaamini hayo, lakini ndivyo ilivyo.

Nimeona nisiongee zaidi maana najion kama nijiweka uchi mbele za watu, pili sipendi kumsema mume wangu kwasababu kiujumla nampenda, licha ya kuwa yeye halijali hilo, na najitahidi kutimiza wajibu wangu, maana hapa sina jinsi nyingine, ningelikuwa nyumbani ningeliamua la kuamua, lakini hapa ni nchi ya watu…naishi kwa kibali, ….

Nawashukuru sana kwa ushauri wenu mungu awabariki, na akubariki wewe mwenye blog, mengi zaidi kama yapo nnayasubiri kutoka kwenu.

Samahani kama nimewakwaza wenzangu, ambao wanaishi hapa, labda wao wana maisha mengine zaidi yangu, labda mimi, ni mzaifi fulani, lakini niwaulize kama wangelikuwa wao wangefanyaje….

Ni mimi: emu-three

4 comments :

Anonymous said...

Pole sana chamuhimu ni kuvuta subira, ukirudi bongo utajua la kufanya, ila kama ingeliwezekana ungelisoma, hilo ni muhimu sana, lakini kama haiwezekani, haiwezekani, ni hayo tu

Subira said...

Lame excuse, mtu yeyote aliyezoea kuwa abused mara nyingi haoni njia ya kujitoa kwenye hiyo abusive relationship. Ushasema unampenda mumeo na umeridhika na hiyo hali tukushauri nini? Maana itakuwa sawa na kumpigia mbuzi gitaa. Nina mpwa wangu yuko nje, anafanyiwa kama hayo unayoyasema, mume anafanya umalaya wazi wazi, watoto kila kona na yeye ukimwambia suala la kujiendeleza atakuletea visingizio lukuki.

Kwa hiyo bidada hauko peke yako mmejaa tele, shida yenu hamujiamini na mmezoea hiyo hali na mazoea yana tabu! Endelea tu kuvumilia mwaya iko siku akili itafunguka utaona kuwa hayo si maisha!

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

ni sehemu ya maisha. kama huwezi kuachana naye usilalamike pia wala kuomba ushauri. chukulia kawaida tu

Anonymous said...

umeshasema unampenda,la sivyo ningekushauri utafakari halafu uchukue hatau kuishi kwa kibali kitu gani bwana kwani huna kwenu? au ndio kuishi ulaya?utaendelea kuburuzwa mpaka utie akili.