Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Saturday, January 21, 2012

Akufaaye kwa dhiki ndiye rafiki wa kweli-75 hitimisho-19



‘Una uhakika na unachokisema, sasa ilikuwaje taarifa zikamfikia kuwa anahitajika huko haraka?’ akauliza Baba Rose.

‘Kwahiyo ndege haijatua na ikitua wapo watu wanamsubiri, kumkamata, na nyie mumechukua hatua gani za kumsaidia..?’ akauliza kwa hasira. Na aliposikia maelezo ambayo hayakuweza kusaidia akasema kwa hasira;

‘Sasa sikilizeni, kama atakamatwa, haraka mfahamisheni wakili wetu, na mimi nipo njiani, na jaribuni kukwepa majibishano ya silaha, sitavumilia kama kutatokea mauaji yoyote, hakikisheni mnamlinda huyo jamaa iwezekanavyo na jaribuni kuhakikisha hakamatwi, na kama hakuna jinsi na akakamatwa , harakisheni kumtafauta huyo wakili amtoe haraka iwezekanavyo,...'akatulia halafu kabla mwenzak hajasema kitu akasema;

`Nitajitahidi niwezavyo kutoa msaada…kama ikibidi nitafika, lakini sijui kama nitawahi..’akasema huku akiwa uwanja wa ndege, na hakutaka kusema yupo uwanja wa ndege anakuja huko.

Baba Rose au Tajiri Mzungu, alifika uwanja wa ndege akiwa hajatulia vyema, kichwani alikuwa akimuwaza ndugu yake ambaye alimpenda sana kuliko maelezo, na katika maisha yao wamekuwa wakisaidiana kwa kila hali. Alikuwa akibahatisha, lakini kwa taarifa alizozipata toka kwa jamaa anaowafahamu ni kuwa ndugu yake akitua uwanja wa ndege tu anakutana na pingu, na kesi anayokabiliana nayo ni kubwa sana, ikiwemo ugaidi na mauaji. Na kubwa zaidi na maelekezo ya Mzee anayemtokea, sfari hii alikuja hadi huko alipo.

Wakati amekaa akisubiri usafiri akakumbuka maonezi yake ya mwisho na ndugu yake , ambaye wengi hawamjui, Alikumbuka alipopokea simu toka kwa ndugu yake huyo kuwa anahitajika nyumbani haraka sana kufuatilia maswala muhimu, na alipoulizwa maswala gani, ndugu yake huyo hakutaka kuyasema akasema tu ni mambo yao ambayo asipokuwepo mambo yataharibika, ikiwemo miradi yake.

‘Una uhakika kuwa huo sio mtego?’ akauliza kaka yake.

‘Sizani kuwa ni mtego, kwani aliyenipa hizi taarifa ni mtu wetu, na nikathibitisha kwa msaidizi wangu na zaidi nikapata uhakika katika vyanzo vyetu vya habari, usitie shaka na mimi....’ akasemandugu yake huyo kwa kujiamini.

‘Ni hilo tu au kuna jingine na vipi kuhusu yule binti na mpinzani wako,,..?’akauliza kaka mtu.

‘Huyo mpinzani wangu, huenda sasa hivi yupo chumba cha kuhifadhia maiti, kama ana roho saba kama paka, safari hii nimemalizia ile ya saba, nilihakikisha kuwa nimeziba ile mirija waliyomuwekea ambayo ukichelewesha muda mchache tu, mawasiliano yanakatika, …sijui kama watakuwa wamemuwahi….’akasema kwa kujiamini.

‘Wewe sio mungu bwana, mbona mke wangu kasema hali yake inaendelea vyema, wameshamwuahi mapema, kabla hajafikia hali mbaya…’akasema kaka mtu.

‘Ilivyo ni kuwa hata kama watamuwahi wajaribu kumshtua ili mapigo yaanza kufanya kazi, haitachukua muda, maana nilishakatisha mawasiliano muhimu, hayo ni mambo ya kitaalamu tunajua sisi kaka…..’akasema ndugu mtu.

‘Basi huyo ana roho nane, kwani hapa tunapoongea huenda keshazindukana anaongea na mpenzi wake, wewe umekosa mwana na maji ya moto….’akasema kaka mtu.

‘Kwasasa sina jinsi kwani nilichoitiwa huko ni muhimu sana kaka, nimejaribu kuwapanga watu fulani wanisaidie hiyo kazi, …najua watammaliza huyo jamaa, kazi itakuwa jinsi ya kumshawishi huyo binti…hilo naliweka kiporwa, kwasababu tusipofanya hivyo, mali itakwenda kusipositahili, wewe kwa pupa zako umemwandikisha huyo binti ukijua na binto yako, sasa….’akakatiza.

‘Usinikumbushe,….we acha tu, na wewe ulishanipa uhakika kuwa utamchukua, ….sasa sijui, …haloh, upo hewani….’akajiona kama anaongea peke yake.

'Nipo hewani, nilikuwa nafikiria kidgo, unajua kaka, kama atakubali nimuoe, huoni itakuwa maajabu, mtu na kaka yake wanaoa familia moja hiyo ipo kweli, ….?’ Akauliza.

‘Hili lisikutie hofu, maana nimegundua mengi, hasa baada ya kusikia kuwa ana pacha mwenzake, sasa huyo pacha mwenzake alikuwa wapi, kazaliwa na nani, huoni hawa watu wanatufanya sisi wajinga?....’akasema na kukohoa kidogo.

‘Bado hawajafanikiwa kutufanya wajinga, tutawashitukizia, ngoja nifike nyumbani nijipange upya, utaona mambo yangu…;akasema ndugu mtu

‘Unataka kusema unatka kufanya nini, wakati wahusika weneywe umewaacha nyuma, …’akasema kaka mtu

‘Kwanza ujua hawa watu walishampanga huyo binti kama chambo cha kuninasa mimi, na ilibakia kidogo tu waneninasa pale hospitalini,…..na kitu walichofanya ni kunichanganya , wakijua kuwa hawa mabinti wapo mapacha, wakanitumia huyo ndugu yake asiyehusika…… maana wanfanana kama mtu akijiangalai kwenye kiyoo...na baya zaidi wameshaniwekea mitego ambayo nisipoondoka hapa haraka wataninasa, na wakininasa huku nimekwisha, ....kwahiyo ni bora niwahi nyumbani haraka iwezekanavyo....’akasema ndugu mtu.

‘Sawa, ..kwa mtaji huo huna jinsi, na sasa ina maana tumepoteza ule mpangilio mzima, ....lakini sio mbaya, tutaangalia la kufanya, ila hawa watu lazima tuwaonyeshe kuwa tunajua zaidi, huyu mke wangu kanihadaa toka awali, kuwa huyo mtoto ni wangu,….lakini kwangu sio mbaya sana…atakuja kuumbuka mwenyewe..isingelikuwa hawa wazee na mambo ao ya mizimu, nisingelijali sana….unajua kwasababu yao nashindwa hata kurudi nyumbani, maana nikirudi , yule mzee wa ajabu atanitokea na safari hii akinitokea sijui atahitaji nini, huenda ataitaka roho yangu tu…..’akasema.

‘Hayo mambo ya mizimu sijui ya nini, sipendi kuyasikia, ....mimi nawahi tutawsiliana nikifika huko, , ila nakuomba kitu kimoja hakikisha unanipa habari kamili za Rose, nahisi ana ujauzito, sijakuwa na uhkaika kuwa hiyo mimba ni ya nani, na kwa mtaji huo, tunazidi kuwekewa kizingiti, sijakuwa na uhakika na hilo, maana kama nilivyokuambia wapo mapacha , sasa sizani kuwa wote ni waja wazito….?’ akasema kwa haraka haraka.

‘Unafikiri hiyo mimba ni ya kwako, kwani uliwahi kukutana naye, au ulikuwa ukishika pembe, hahaha, mdogo wangu kweli umezidi upole, yaani ulishindwa kabisa kumpata huyo bint mpaka wengine wanakuja kubebesha mamba, hapo sasa umeshindwa wewe, una uhakika ni mja mzito, na je mamba hiyo ni ya nani, au ni ya kwako....?’ akaulizwa.

‘Kaka sijui zaidi, ..kwaheri muda umefika wa kuingia kwenye ndege, tutawasilina baadaye....’akasemana mawsiliano yakakatika.

**********

Wakati anaongea na ndugu yake huku akipata kinywaji baridi, akataka kuinuka kuondoka, mara, ikasjisikia kizunguzungu, kichwa kikawa kinamuuma isivyo maelezo, mara…kukawa kama kitu kimempitia machoni, akatulia kwa muda hadi ile hali ikapita, akainuka na kutoka nje, alipofika kwenye kona ambapo ni karibu na aliposimamisha gari lake, akaona mwanga mkali ukipita mbele yake. Alitizama huku na kule, lakini hakuona kitu kilichomulika, akatulia kwanza na kuwatizama watu ambao walikuwa wakiwa na sughuli zao na hakuna mtu aliyekuwa akishangaa kama yeye.

Akaanza kuinua mguu kulifuata gari lake, mara ule mwanga ukatokea tena, na safari hii ulikuwa mkali kiasi kwamba ulifanya macho yake yashindwe kuoan vyema, na hata wale watu waliokuwa wanapita au kusimama karibu naye akawa hawaoni tena, anachoona ni ule mwana tu. Na cha ajabu ule mwanga ulikuwa ukionekana njiani ambapo watu wanapita, lakini watu hawo hakuweza kuwaona zaidi ya ule mwanga.

Na wakati anahangaika kusafisha macho yake kutokana na ule mwanga mkali ili ajaribu kuona vyema, mara kukatokea kitu kama kivuli, kwanza kilinza kwa kuonekana kitu kimoja kimoja kama vile mtu anachora picha, na chaki kwenye ubao, lakini ubao huo ni mweupe, na chak ni nyeusi, kukaanza sehemu ya kichwa, sehemu ya kiwiliwili, ikashuka hadi kwenye mguu, na kuelekea upande wa pili wa mwili, mguuni, ikapanda hadi kiwiwili, hadi kichwani na kuja kuunganika na sehemu ile ya upande wa kwanza na baadaye kikakamilika kiwiliwili kizima….

Kabla hajamliza kushangaa, ile sura ya mtu, ikafunuka mdomo, na kuanza kuongea hapo hapo….

‘Unafikiri kuja kujificha huku nchi za watu ndio umenikimbia, mimi nitakufuata popote pale, isipokuwa kwenye kaburi lako, ambalo sasa linakaribia kuchimbwa….’ Ile picha ikawa ianongea, na sauti ilikuwa ikisikika waziwazi, kiasi kwamba jamaa yetu alijua kila mtu anasikia hayo maneno, kumbe yalikuwa yakisikiwa na yeye pake yake.

‘Umeshahu nilichokuagizia au unataka tuanze vurugu zetu, umesahau yale mateso uliyokuwa ukiyapata kabla hatujakusaidia, au kwa vile umepata mwanamke mrembo, unahisi kila kitu kimekunyookea, au kwa vile unaona biashara yako huku nje inakuwa ndio unazania hutafirisikia. Kwanza nikuambie ukweli, wewe unadanganyika na huyo mwanamke humjui vyema huyo mwanamke, yeye anachokupendea ni huo utajiri, na ukiisha, na wewe hakutaki tena, je untaka tujaribu hilo ili uone ukweli…?’ ile sauti ikatulia kwa muda. Na kabla hajasema kitu, ile sauti ikaendela kusema;

‘Tunaweza tukakufanya hohe hahe, ili uthibitishe huo ukweli, kuwa huyo mwanamke yupo kwa ajili ya mali yako, na ukifilisika anakukimbia, na kama unataka tufanye hivyo, hatari yake ni kuwa ukifirisika utaishia kuchanganyikiwa na katu hutakuwa tajiri tena, kitakachofuata ni kaburi lako, nasi tutakukaribisha huku kuzimuni, ….unasemaje….?’ ikasema ile sauti na kutulia tena kwa muda…na jamaa yetu hakujibu kitu.

Baada ya muda mfupi ile sauti ikitokea tena, ile picha kama mtu ikawa kama inafifia na kubakia meno, au sehemu ya mdomo tu, huenda ni kutokana na ule mwanga ulivyo mkali.

`Kwani wewe ni nani na unataka nini kwangu?’ akauliza baada ya kuvumilia kwa muda mrefu akimsikiliza, moyoni alishahisi kuwa ni nani huyo, lakini alitaka kujena ujasiri, kwani alishachoka kuwa mtumwa wa mambo hayo, hakuona tena raha ya huo utajiri, lakini je angeliweza kuachana na hayo mambo kirahisi hivyo!.

‘Umeshanisahau sio, au kwa vile siku hizi unaishi nchi za ugenini..?’ ile sauti ikacheka kwa kebehi, halafu ikasema;

`Au kwa sababu ya huu mwanga mkali, ndio maana hunioni vyema, hebu pikicha macho yako halafu halafu uniangalie tena….’kile kitu kama picha kikasema. Na jamaa akapangusa macho yake kama alivyoambiwa na alipoondoa mkono wake machoni akajikuta anatizamana na mzee mmoja , mzee ambaye kila alipokutana naye alikuwa kama kakutana jinamizi la kutisha, na aheri ingelikuwa ni jinamizi , kwasababu ni ndoto, sasa hiyo haikuwa ni ndoto, unakutana na hilo jinamizi moja kwa moja.

Ile sura ya yule mzee ilipotokea, kwenye ule mwanga, na ule mwanga mkali kufifia, Jamaa yetu alianza kuishiwa nuvu, miguu ilikuwa kama imevunjwa vunjwa, alijitahidi kusimama imara, kuogopa kuanguka pale mbele za watu. Tukio kama hili lilipokuwa likimtokea awali, alikuwa akiogopa na hata kuzimia, lakini huyu mzee alipokuja kumtokea na kumpa ujasiri, akawa anajitahidi kuvumilia n kukabiliana nalo. Akimtizama yule mzee huku kumbukumbu za mateso ya nyuma zikimrejea akilini.

Wakati akiwa mtoto, Tajiri Mzungu, jina alilokuja kuitwa baadaye baada ya kuibuka na kuwa tajiri, na kuanza kuishi kizungu, licha ya masharti makali aliyokuwa kawekewa, kuishi huko ilikuwa tu kwa nje, lakini kiundani alikuwa hana raha.

Maisha ya utoto wake yaliubikwa na ndoto za kuogofya karibu kila siku, na mara nyingi aliombea usiku usije, ili asije akakutana na hayo mauza uza ya usiku. Wazazi wake walimuhangaikia huku na kule na hospitalini yote walimaliza na mwishowe waliishia kusema hana tatizo na hali itakuja kwisha tu akiwa mkubwa. Na kwa vile akiwa mtoto, alikuwa akilala chumba kimoja na mdogo wake, matatizo yaliyokuwa yakimtokea yalimuathiri sana ndugu yake huyo aliyekuwa akilala naye kitandu kimoja, maana kaka yake akikurupuka usingizinii anaweza hata kukimbia nje, kwahiyo mdogo mtu ndiye aliyekuwa akijitahidi kuhakikisha kuwa milango imefungwa kabisa….

‘Baba mimi nitakuwa ninamfunga kamba kaka usiku maana akiota anakuwa mtu wa ajabu sana, anakuwa kama sio yeye, kwani anajibamiza chini na wakati mwingine anakimbia kwenda nje, naona jambo jema ni kumfunga kamba, ili akianza fujo zake asiweze kuumia….’akasema mdogo mtu ambaye zoezi hilo alishalianza kulifanya bila hata kuwaambia wazazi wake, ambao mara nyingi wakifika wanakuta mtoto keshatulia, kwahiyo hawakujua zaidi ya hayo wanayohadithiwa, hadi pale walipoamua kukaa naye karibu na walichokiona , kiliwafanya wahangaike zaidi.

‘Haya mambo ya kimila yapo, na kote tulipoenda tumeambiwa kuwa hayo yanatokana na mizimu ya mababu, huyo anayemsumbua ni babu yangu…babu huyu alinipenda sana, na kabla ya kufa alisema sikuu moja atakuja kunitokea kwa kupitia mtoto wangu, sasa naona ndiyo huyo kamjia mwanangu, na hili kuliondoa inabidi kafara kubwa sana….’akasema baba wa huyo mtoto.

‘Hapana mambo hayo yanakwenda kinyume na dini, mimi sitayakubali….’akasema mama wa mtoto kwa mara ya kwanza, na yeye akaamua kwenda kwa watu wa dini, ambao walihangaika kiasi cha uwezo wao, lakini walikutana na vizingiti vya baba mtu, na hata kutishiwa uhai wao, na walipooona hivyo, ikabidi wasalimu amri na kuwaachia wanafamilia wao wenyewe. Mama alijitahidi sana, lakini mwishowe naye akatishiwa kuuwawa, na hata kuachika, na kuambiwa hilo halimuhusu, amuachie baba mwenyewe, anajua nini cha kufanya. Hayo mambo yalipozidi sana, mama ikabidi ashirikiane na mumewe na ndipo siku moja wakampata mzee wa kale akawaongoza na kuwapelaka kwa mtu aitwaye ‘mtaalamu’ .

Kwa jinsi alivyokuwa akipata taabu na ndugu yake huyu, akawa kajenga ukaribu sana na hawakuweza kukaa mbali na hata kaka yake alipochaguliwa kwenda sekondari, mdogo mtu alipinga kwa nguvu moja, akijua kuwa ndugu yake hatakuwa na mtu wa kumlinda pale akianza kukurupuka na ndoto za usiku. Mtaalmu wao alikuja na kumpa dawa za kumsaidia na akasema huko anapokwenda hatapata shida sana, na ikitokea shida wamuite, atayamaliza hayo matatizo.

Kaka mtu akaenda sekondari ya bweni, na mwaka wa kwanza hali ilikuwa nzuri, na mambo yaliazna alipofika kidato cha pili na mbaya zidi kidato cha nne. Siku moja akiwa amelala, aliamuka usiku wa manane na kuanza kupiga makele, hadi bweni zima likaamuka, na wenzake walipomkaribia akaanza kuwapiga, na hata kuanza kujibamiza ukutani. Hali hiyo ilikuwa mbaya hadi asubuhi, ambapo ndipo alipata usingizi na alipozindukana wenzake walipomuuliza alibakia kushangaa tu, hakujua kulitokea nini.

Hali hii haikuishia hapo jamaa huyu akawa anaona vitu vya ajabu ajabu, na wakati mwingine anaona watu ambao wengine hawawaoni, na hali hii ilifikia hatua hata wanafunzi wenzake wakaanza kumuogopa. Wengine wakamuita mwanga, wengine, mganga wa kienyeji, maana wakati mwingine, aliweza kutafuta dawa zilizoweza kuwatibia wenzake , pale wanapoumwa magonjwa kama ya kichwa au matumbo, …na wakati mwingine aliweza kutoka nje ya bweni na kuanza kukimbia ovyo akidao anakimbizana na watu wasioonekana, akadai alikuwa akiwakimbiza wachawi….

‘Hivi wewe una matatizo gani, …?’ akaulizwa na mwalimu wao baada ya kesi yake kupelekwa kwake.

‘Mwalimu hata mimi sijui, maana sijitambui, inakuwa kama ndoto, au sijui nisemeje, haielezeki, ila mara nyingi inaanza kwa kusikia maumivu makali kwenye kichwa, najisikia vibaya vibaya…au wakati mwingine inaaanza kama ndoto, najikuta kama nakabwa halafu kunatokea majitu ya kutisha, yakiwa na meno makubwa na sura mbaya, yote yanataka kunivamia mimi, ndipo hapo naanza kupiga ukulele, na wakati mwingine yakitokea napotelewa nafahamu na wala sijijui kabisa kinachoendela, nasikia watuw akisema nakijibamiza, nakujiga- piga, mimi hayo siyajui, nasikia kwao tu….’akasema huyo kijana.

‘Na wakati mwingine anajibamiza sakafuni au ukutani, usipomshika anaweza kuumiza watu, na huwa anabadilika hata sauti anaongea kama mzee, sauti ya kizee nay a kutisha, ….cha ajabu anadai kuwa anamuhitaji yeye….yaani anataja jina la huyu kijana kuwa anamuhitaji arudi kwao, akapewe majukumu….’akasema mwalimu wa malezi.

‘Majukumu gani hayo anatakiwa kupewa mtoto kama huyu badala ya kusoma kwanza...mbona mimi siyaelewi hayo mambo…hebu nifahamisheni kwa mapana….’akasema mwalimu mkuu.

‘Kuyaelewa kwake mpaka umuone akiwa katika hiyo hali, kwakweli anateseka sana, mimi ningelishauri arudishwe kwao kwanza wakamuangalie kienyeji, maana akipelekwa hospitalini hakuna kinachogundulika, hana malaria wala hana tatizo jingine lolote….’akaongezea mwalimu wa malezi.

‘Hivi sisi tutaelewekaje na hawo wazazi wa mtoto, wakituona tunamrudisha mtoto wao nyumbani eti anaumwa bila ushahidi wa dakitari, …..mimi bado sijarizika na hilo, tunahitaji ushahidi wa kimaandishi, na ushahidi huo utoke kwa dakitari, maana huo ni ugonjwa, au sio uonjwa jamani, ….?’ Akauliza huku akiwageukia wenzake ili kupata ushauri, na walipokuwa kimiya akaendelea kusema;

‘Na ni bora likitokea tena hilo tatizo awepo huyo dakitari alishuhudie mwenyewe, nami nitafurahi nikiliona hilo tukio, ili njirizishe mwenyewe. Akiwepo dakitari, basi ataweza kuandika lolote kuhusiana na tatizo lenyewe, na huo utakuwa ushahidi wetu kwa wazazi, na yeye ataweza kuanisha kitaalamu zaidi, ili hawo wazazi kama wataamua kuendelea na matibabu zaidi wajue ni wapi pa kuanzia….’akasema huyo mkuu wa shule na kuwangalia wenzake kuwa wana la zaidi na alipohakikisha kuwa hakuna la nyongeza, akauliza;

‘Je mnakubaliana na hilo, au kuna jingine la nyongeza..?’ akauliza na wote wakakubalika na hilo wazo na kweli siku moja likatokea tukio la aina yake, maana bweni zima walitoka nje kumkimbia, jamaa alikuwa akinuruma kama samba, na aliyemsoelea alipata kipigo cha aina yake, akaja mkuu wa shule na dakitari ambaye alipoona hivyo, alisaliu amrii na kusema;

‘Haya mambo siyo ya kihospitali, mimi ni dakitari na kazi yanu haishughuliki na mambo kama haya, mimi nawashauri kuwa, huyu mtoto mrudisheni kwao, wao kama familia watajua nini la kufanya, vinginevyo apelekwe wodi ya vichaa, hilo ndilo lipo ndani ya uwezo wanu, lakini swali ni kwa ugonjwa upi, maana ukimpima na ukimchunguza vyema, hana tatizo, na akiwa hana hiyo hali huwezi kujua lolote….’akasema huyo dakitari ambaye siyo mara ya kwanza kuletewa huyo kijana mweney hayo matatizo.

‘Basi tunaomba utuandikie huo ushauri wako, ili tupate ushahidi wa kuwapelekea wazazi wake….’akasema mwalimu mkuu na dakitari huyo akakubali, akafanya kama alivyoombwa, ni ikawa ndio mwisho wa mtoto huyu kusoma kwenye shule hiyo, kwani aliporejea nyumbani na kukutaa na mtaalamu aliyekuwa akimtibia alitoboa siri kubwa ni kwanini hayo yalikuwa yakimtokea huyo mtoto.

Waliambiwa ndani ya familia yao kuna mizimu ambayo inamuhitaji huyo mtoto ashirikishwe katika mambo yao ili kuendeleza desturi za mila za mababu zao, ambao wamekasirika kwa kutengwa…., la isipofanyika hivyo, hayo matatizo kwa huyo mtoto hayatakwisha…na yanaweza kuwa ambaya zaidi…, na hata hivyo huyo mtoto ana nyota ya utajiri ambayo imeshikiliwa na hawo mizimu, kwa masharti ambayo atakuwa akielekezwa mwenyewe…’akasema huyo mtaalamuu na kuwaacha hawa wazazi hawana la kufanya.

‘Sasa tufanyeje maana haya ni mateso kwa mtoto wetu..’ akauliza mama akiwa an huruma ya mwane ambaye kwa wakati huo alikuwa kalala chini hoi baaada ya kujibamiza chini na ingwaje walijaribu kumshika lakini walishindwa kabisa, hadi alipokuaj huyo mtaalamu na kumpa dawa zilimyamazisha . Dunia hii kuna mambo…

‘Cha kufanya kwa sisi hakuna, ila nitajaribu kuliondoa hilo tatizo kinamna , hilo jambo lisiwe linamtokea mwilini mwake, litakuwa linamtokea moja kwa moja, yaani hiyo mizimu atakuwa akiiona moja kwa moja na kuongea naye huyo mtu au mzimu wake unaomsumbua, lakini inatakiwa ujasiri, na yeye mwenyewe ataambiwa nini la kufanya, …mimi sitaweza kuingilia huko zaidi…’akasema huyo mtaalamu.

Na kweli baada ya jitahada za huyo mtaalamu, akafanya alichofanya na ile hali ikaondoka na jamaa yetu akawa anatokewa na huyo babu moja kwa moja. Wanasema ni babu yake aliyekufa zamani….
Kwa mara ya kwanza jamaa huyo aliogopa sana, kwani sura ya huyo mzee mwanzoni ilikuwa ikija kwa sura ya kustisha kidogo, na baadaye alipoona hivyo, huyo mzee akajiweka aktika sura ya kawaida isiyo ya kutisha.

Na siku zilivyokwenda akawa anazoeana na huyo mzee, na akimtokea anajua kuna jambo anataka kuambiwa. Huyu mzee akawa anampa mashrti ambayo yalianza kumjenga huyo jamaa katika hali ambayo hakuwa nayo, akaanza kupewa utajiri , lakini utajiri huo ulikuwa na masharti kadhaa, na kwa vile aliutaka huo utajiri, akawa anayatimiza hayo masharti, hadi pale alipoanza kuyavunja baadhi ya hayo masharti moja baada ya jingine, na mambo yakaharibika, na alichoona ni kukimbilia nje,akijua kuwa hatakutana na huyo mzee!.

*********

`Oh, ni wewe mzee tena, unataka nini tena huku, tulishaahidiana kuwa hutaniingilia mambo yangu yangu ya biashara nikiwa huku nje, sasa mbona umevunja ahadi yetu…oh, tafadhali hapa ni sehemu za watu….nakuomba usiniumbue, tafadhali….’akasema huku akitetemeka.

‘Nani aliyevunja ahadi yake, mimi au wewe, unakumbuka nilivyokuwa nikikuambia, ..unakumbuka mashrti uliyokuwa umepewa , na sasa umayakaidi hayo masharti moja baada ya jingine. Umeniahidi mengi, ambayo hujatimiza, wewe hujui nimekuwa nikiteseka kwa ajili yako, mimi nimekuwa mdhamini wako, na nikawaahidi wenzangu kuwa utatimiza yote,…wao walishanimbia kuwa wewe hufai, wanataka damu yako …lakini nikawaomba na kuahdii kuwa nitakudhibiti…. je lipi ulilowahi kulitimiza, au unataka niwaachie wenyewe wafanye kazi yao…?’ akauliza yule mzee.

‘Wenyewe akina nani, mimi nilishasema sitaki tena mambo hayo… sitaki tena, na kama ni utajiri wenu chukueni, ni heri niishi masikini kuliko kujiingiza kwenye mambo kama haya, siwezi tena kujiingiza kwenye kuua watu ili eti nipate utajiri….utajiri gani usio na raha, kila mara damu ya mtu, damu ya nini sijui, kwani lazima iwe damu ya mtu, hakuna kitu kingine kwanini isiwe damu ya kuku, ng’ombe au mnyama yoyote, lakini kwanini iwe damu ya watu, wasio na hatia….hapana, naombeni mniache huru, sitaki tena…’akasema jamaa yetu huyu.

‘Hahaha, sasa hutaki utajiri tena, sasa umechoka na utajiri, au kwa vile unaishi kwa raha huku nje, sawa hatukatai, umeshajena jina la kibiashara…., ila nakuonya jambo moja,..hilo linahitaji uharaka wako, usijali cha mkeo au nani…na hapa unavyozidi kupoteza muda ndio unazidi kuweka mambo hayo katika hatari zaidi. Unavyozidi kuchelewa huku, ndivyo unavyozidi kuhatarisha maisha ya damu yenu, …na tulishakuambia kuwa kama sio damu ya mkeo, basi damu ya mwanao, au damu ya ndugu yako, na naona damu ya ndugu yako ni bora zaidi….’ila taswira ikaanza kupotea.

‘Hebu tafadhali subiri kwanza, una maana gani kusema damu ya ndugu yangu ni bora zaidi , ndugu yangu yupi huyo….?’ akauliza kwa mashaka.

‘Eti unasema `Ndugu yangu gani huyo…!’…’ila sauti ikatulia halafu ikasema kwa haraka;
‘Hivi wewe unafikiri hatujui hilo, ndugu yako huyo anayejibadilisha kama kinyonga, na yeye kavunja masharti na ahadi yetu tuliyompa, unafikiri kujibadili kule anafanya kwa utaalamu wake mwenyewe, hahaha..yote hayo ni kutokana na miujiza yetu,…’akatulia na kuwa kama anapotea potea, halafu aaksema tena;

‘Yeye ndiye aliyeanza mapema, kuvunja masharti, akijiona kawa mtaalamu, eti docta…sawa ni docta, lakini mengine hayaendani na ujuzi wake, ni yetu sisi tuliompa…anajua lakini sasa anatuzarau….alianza kubadilia mapema, lakini hatukuwa na kazi naye sana, maana mengine alikuwa akiyafanya hata bila ya sisi kumwambia….na sasa tulipokutana naye anajidai kuwa hataki tena kumwaga damu, ….huyo ndugu yako tunamjua na ananijua mimi kwa sura nyingine,…ananiita mwalimu, wewe ukikutana naye muulize habari za mwalimu wake, atakuambia….hahaha…..’akasema huyo mzee kwa dharau.

‘Sasa mbona mumeniambia mimi hayo na wakai nilikuwa siyajui….?’ Akauliza huyo jamaa kwa mshangao.

‘Kwasababu mambo yameharibika …hilo ndilo ninaloweza kukuambia kuwa mambo yameharibika na mlioharibu ni nyie wenyewe……Ndugu yako anakwenda huko alipoitiwa, na huko ndipo mambo yanaenda kumaliziwa,hakuna jinsi …yeye sasa hivi anakuja kwenye mikono yetu kilaini, ….damu yake tutaipata bila ya kukutegemea wewe…umesikia `anajileta mwenyewe…’ na wewe zamu yako itafuata….ndivyo mambo haya yalivyo, hasa ukikiuka masharti…’akasema yule mzee na kuanza kupotea.

‘Subiri tafadhali, subiri kwanzaaah, nakuomba tafadhali, nitatimiza mnayotaka,ila kwa sharti kubwa msimfanyie lolote ndugu yangu, naombeni msimdhuru ndugu yangu, kwani mnataka nini zaidi…kama ni damu ya mwanagu nitawapa, na hata mkitaka ya mke wangu ni-na-na-weza kuwapa-pa-tiaah…., lakini nawaomba msimzuru ndugu yangu…..’akasema huku akianza kuogopa.

‘Hahaha, hata ya damu ya mke wako unaweza kutupatia kweli…mbona unasema kwa kigugumizi, najua damu ya mtoto wako ukitaka utaipata tu, kwasababu huna huruma naye kwasababu sio damu yako, au sio, lakini mke wako je, ….’ Ile sauti ikanyamaza kidogo, na baadaye ikaendelea kuongea kwa kusema;

‘Haya tunaisubiri hiyo damu ya mkeo….hahaha….unajidanganya, mambo yamefikia tamati, kinachotakiwa ni kumuwahi ndugu yako kama unampenda kweli, ….kwani kwasasa hatuna la kufanya, unachotakiwa ni kumwahi ndugu yako, kabla hajaingia kwenye makucha ya watu wanaomsaka, huenda ukafanikiwa kwa hilo kwa muda, ukichelewa unajua nini kitakachofuata….’yule mzee akapotea na ule mwanga ukapotea pia, na hali ikarudi kama kawaida, na jamaa akazindukana kutoka kwenye ile hali.

Ile hali ilipokwisha, na akili ikamrudia vyema, akatizama huku na kule na kugundua kuwa baadhi ya watu walikuwa wamemzunguka wakimshangaa,…hakutaka hata kuongea nao, kwani wengine walishaanza kumuhiji na kumbe wengine walishaita watu wa usalama, …alipogundua hilo, akaona sasa ataumbuka, akakimbilia gari lake na kuondoka harakaharaka. Na aliofika sehemu ambayo alikuwa kaiweka kama ofisi ya muda akampigia mkewe simu kumwambia kuwa anatakiwa kurudi nyumbani haraka….

NB Naona hii ni zawadi ya wiki end. Na wazo la leo ni kuwa; Matendo mema ni msingi mwema wa maisha, usijali wasemayo, wewe tenda wema hata kama kwa kufanya hivyo ni kuwauzi wengine, kwani Wema katu hauzi.
Ni mimi: emu-three

2 comments :

Anonymous said...

Mkuu unachukua muda mrefu sana kutupa hivi vitu, au ndio umekwama, sema tukusaidie?

EDNA said...

Jirani kwema? nimepita kutoa zangu salamu.Siku njema.