Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, December 16, 2011

Akufaaye kwa dhiki ndiye rafiki wa kweli-65 hitimisho-9




‘Wifi, …’alisikika shangazi akitamka kwa mshangao, na macho yake yalikuwa yakichezacheza kuangalia, mlngoni kwa huyo mtu aliyeingia na kwa Maua, ambaye ailikuwa kalala pale sakafuni, na kabla hajaeleza nini kilichotokea yule mama aliyeingia mlangoni, na muonekano wa kitajiri kwa mavazi, na vito alivyovaa mwilini, alitabasamu, na kusema kwa sauti ya lafudhi ya kizungu, nzito kama ya dume.

‘My God, ni wewe wifi langu, mume wangu mahabub, oh, sikutegemea kuwa nitakukuta hapa wifi, nimefika hotelini kwako nikaambiwa umetoka, …oh, vipi tena, huyo vipi, ….’akasema huku anamsogelea shangazi ambaye alishamweka Maua vyema, na wakakumbatiana na wifi yake, lakini mkumbatio haukuwa wa nguvu, kwani huyo mwanamama alishatupa jicho kwa huyo aliyelala chini na moyo wake ukamlipuka, na akasema.

‘Oh, Rose, what happens,…kumetokea nini kwa binti yangu, ….kumetokea nini, docta yupo wapi, …?’ akawa anauliza huku anaangali huku na kule..

‘Amepoteza fahamu alipomuona mgonjwa, na ndio nilikuwa na taka nimuweke vyema,…lakini usitie shaka hii ni kawaida..atazindukana, muache atulie, usiwe na wasi wasi…’akasema Shangazi.

‘Nisiwe na wasiwasi, hapana, ngoja nimuite docta, haiwezekani, kwanza kalala chini, hii sio fair, let call the docta, hapa yupo hospitalini, kwanini tuumize vichwa, wakati wataalamu wapo..’akasema na mara akatoka, na kurudi na docta, na nesi, ambao hawakupoteza muda, walimchukua Maua hadi kitandani na kuanza kumpa huduma ya kwanza,

Yule mwanamama hakuwa na amani tena, akawa anahaha kuwaangalia madakitari wanavyomuhudumia Maua, na shangazi halikadhalika, lakini kwa shangazi moyoni alikuwa na mengine ya kuwaza, kwani mambo yametokea haraka kiasi kwamba anashindwa jinsi ya kuyadhibiti, hakutajia kukutana na huyu mtu mahali kama hapa, na isitoshe, hakutaka kabisa yule mgonjwa, aliyefanyiwa upasuaji aamuke na kuwakuta wakiwemo humo ndani, na hakutaka kujielezea lolote kwa huyo wifi wake, kwani sivyo alivyokuwa kajipanga.

‘Wifi tutaongea baaadaye naona akili yangu haipo shwari, kwani huyu binti sikujua nitamkuta hapa, aliniambia atakuja toka masomoni, lakini sikuwa na uhakika kama atakuwa kaja kumuona huyo mgonjwa, maana haambiwi lolote kuhusu huyo mwanaume….yaani watoto wa siku hizi, mume mwenyewe hamjui vyema, wapi anapotoka, ni nani, haijulikani, lakini ndio kazimia kwake, …’yule mwanamke akawa anaongea kama cherehani.

‘Shangazi alichofanya yeye ni kutabasamu tu, huku akimwangali wifi yake huyu ambaye walishibana sana, kwani sio tu kwasababu ya uwifi, bali walisoma pamoja, na kuhangaika pamoja katika maswla ya biashara, na mwenzake alipofanikiwa na kuanza bishara za masafwa wakawa hawaonani tena, akamwangali na hapo kumbukumbu za misha yake na huyu mwanamama zikamjaaa kichwani.

******
‘Wifi yangu..’ usemi wa wifi ulianza mapema kati ya wandada hawa, tangu wakiwa shuleni, walipenda kuitana hivyo `wifi’, kama utani tu, hawakuwa na maana kubwa zaidi ya kuitana hivyo, kwani hakuna aliyekuwa akimjua kaka wa mwenzake kiundani, lakini lilikuwa jina la kuitana kimasihara tu , lakini utani wao ulikuja kuwa kweli siku moja.

Ilikuwa kipindi wamepumzika, na mara akaja jamaa mmoja, na kusalimiana nao, jamaa huyo, hakuchukua muda akaondoka. Alipoondoka, wakawa wametulia, na baadaye yule jamaa akarudi na kukaa pembeni , mbali kidogo na walipokaa wao.

‘Vipi unamfahamu huyu jamaa, ….’akauliza mwenzake, huku akijiiba kumwangalia yule jamaa.

‘Hivi wewe kumbukumbu zako zimeenda wapi, hukumbuki mara nyingi tumekuwa tukikutana nao, na kipindi kile walikuja na mwenzake nikakutambusliha kuwa wale ni kaka zangu, basi kama umesahau, kutana na kaka yangu, yeye anafanya biashara zake huko mikoani, anakuja huku na kushusha mizigo yake halafu anarudi mikoani,..yeye sio muongeaji sana, kama unavyomuona…’ hapo ilikuwa siku ya kwanza kwa rafiki wa shangazi kuguswa na huyu jamaa, ikaanza kimasihara lakini mwisho wa siku mambo yakakolea.

‘Kaka yako mrembo kweli, nilikuwa sijaligundua hilo, na huo mwili wake duuh , unanisisimua, kajazia kifua kama muinua vyuma, …’akasema wifi.

‘Wifi, acha mambo yako wewe usiseme umempenda kaka yangu, unataka kuhalalisha uwifi bila makubaliano, …sitaki kabisa, kwasababu nakufahamu sana tabia yako hujatulia wewe, wewe hutosheki na wanaume, …pesa kwako ndio mume, usije ukamuumiza kaka yangu bure, najua mwisho wa siku utamuacha solemba…’akasema wifi.

‘Mhh, kweli nimempenda, simuachii, lazima wewe uwe wifi yangu, hata kwa masaa, haitakuwa mbaya, na kwa vile ni mfanya biashara na pesa ipo tutaivana sana, nimemtamani kweli, hebu mwangalie kile kifua, natamani, nikitikise kile kifua, kanitambulishe kwanza…’akang’ang’ania huyu mwanadada hadi wakakutanishwa na kaka mtu, na urafiki ukaanzia hapo, na shangazi hakutia neno, akijua kuwa kweli rafiki yake kampenda kaka yake, na mwisho wa siku itafungwa harusi.

Siku zikaenda na kweli kaka mtu akakubaliana na huyu mwanadada kuwa waoane, na harusi ya nguvu ifanyike, na maandalizi ya hali ya juu yakatakiwa kufanyika, na wote wakakubaliana. Na kipindi hiki, shangazi yeye alishaolewa, na zile biashara za masafa kwake zilipungua sana, kwani walishafikia mbali wanadada hawa kibiashara, walishirikiana mwanzoni, wakawa na hata biashara za masafa, wakisafiri nchi mbalimbali kama Kenya na Uganda, kupeleka mizigo, na kununua bidhaa za kusambaza nchini,..

Baadaye shangazi yeye akaolewa, na kupunguza hizo biashara za masafa, akawa anafanya biashara za ndani ya nchi, labda akihitaji mizigo, anamtuma mwenzake kwa makubaliono na siku zilivyozidi kwenda ikawa vigumu kwa wanadada hawa kukutana mara kwa mara, na kwa vile makubaioano ya harusi yalishafikiwa kuwa kaka yake shangazi atamuoa huyo mwanadada, ilibidi maandalizi ya harusi yafanyike, na shangazi na familia yao wakawa wanahangaika kweli, na wakijua kuwa huenda na upande wa kikeni nao wanafanya hivyo hivyo.

Basi siku moja wakakutana shangazi na wifi, shangazi akaona amshauri wifi yake, kwa kumwambia, ‘wifi unaonaje maana sasa zimebakia wiki mbili utulie nyumbani, ili kupata muda wa maandalizi,..maana harusi inakaribia, na wewe unatakiwa kufundwa na mambo kama hayo, kwani wewe unahitajika kweli kuelekezwa jinsi ya kusihi na mume, sio kuruka, ruka…’akasema wifi mtu.

‘Harusi-ii, harusi ipi hiyo,… ooh, nilishasahau, unajua nilitaka kukuambia kitu, sijui kama utanielewa, unamkumbuka yule tajiri wa Uganda, yule mzungu koko, wanavyomuita, kaniahisi mambo mengi sana, na ule mzigo nilioleta kanipatia yeye mtaji, na kanifungulia duka huko Uganda, na ado memo mengine mengi, hapa nachanganyikiwa maana naona nimelikoroga, lakini nitacheza najua nini cha kufanya, maana bila yeye sitafikia malengo yangu,…kitu ninachotaka kukuamia ni kuwa nataka kuiahirisha hii harusi sijui mapaka lini…’akasema wifi.

‘Eti, nini, umechanganyikiwa nini, unajua unaongea na nani, ..mbona unanitia kiwewe, hapo sikuelewi kabisa, hebu sema tena..’akasema wifi mtu kwa hasira.

‘Sikiliza, nikuambie kaka yako keshafaidi kile alichokitaka kwangu, sioni kwamba atapata zaidi ya hicho, inatosha, na baya zaidi ameniharibia mipangilio yangu, kwasababu nahisi ni mja mzito…lakini sitaki kuzaa, …sijajiandaa, siku ile alitumia nguvu, mimi nilimwambia kuwa sipo salama, yeye akatumia misuli yake na sasa mambo yameharibika, …lazima niitoe hii mimba, hiyo ni siri yako, wewe ndiye rafiki yangu ninaye kutegemea, …’akasema huyo mwanamama, bila kujali kuwa anaongea na nani…

‘Wifi,kama kuna siku umeniumiza moyo wangu, ni leo, nakuona kama mtu gani sijui, natamani hata kukumeza, nini unachoongea hicho, hujui yule ni kaka yangu, na hilo unaloniambia ni kama unanifanyia mimi..hapana, ukiitoa hiyo mimba, basi umekuwa adui yangu..urafiki unakufa na nitahakikisha nakukomesha, hunijui mimi eeh, siunanjiua zangu za shuleni, za kidume dume, nitahakikisha unazama ardhini ila kufa, hilo nakuhakikishia…’akasema wifi.

‘Usinibabaishe kabisa na maisha yangu, haya ni maisha yangu, na kilichopo tumboni ni changu, mimi nimeamua kukueleza wewe kama rafiki yangu mpendwa, badala ya kunisaidia unanitishia amani, mimi sio wakutishiwa amani kabisa,ninajua nini ninachokifanya… hahaha, eti sikujui vyema, yale maisha ya shule hayapo tena, mimi nilivyosafairi bila wewe nimejifunza mengi, na hapa ninachokuambia ni kuwa huyo tajiri wa Uganda, nimeshambambiki hii mimba, anajua ni ya kwake…’ akaonyeshea tumboni huku anabenua mdomo wa dharau.

Shangazi alimwangalia kwa macho yasiyoamini, ilikuwa kama anaongea na mtu asiyemjua kabisa, kweli kipindi kifupi walichoachana, baada ya yeye kuolewa na kutulia mwenzake amabedilika kiasi hicho, hakuamini kabisa…akabakia kimiya kusikiliza.

‘Unafikiri mimi mtoto mdogo eeh, hii mimba ni yakwake huyo tajiri kihivyo, kwa kubambikiwa, lakini kidamu siyo ya kwake, ni damu yenu, ni mimba ya kaka yako, hilo nakuhakikishia, kwahiyo kuanzia sasa nisisikie kuwa nina mimba ya kaka yako, nitajua mwenyewe jinsi ya kulicheza hili rumba, na kama rafiki yangu nisaidie kwa hili, fanya ufanyalo hii harusi iahirishwe mpaka niweke mambo yangu safi…’akasema wifi.

‘Hapo hatutaelewana, kabisa….harusi ipo na mimba hiyo itunze, achana na tamaa za kijinga…unafikiri utajiri ni kila kitu, na ukumbuke yule ni kaka yangu, nampenda sana, sitakubali aumie kwa ajili yako, nilishakukanya kwa hilo ukaniahidi kuwa sasa utatulia kwa ajili yake na kuwa mke mwema, ndio mambo yako hayo,…huvi wewe utatulia lini, unajua ujana una mwisho wake, hunioni mimi nimeolewa na nimetulia na mume wangu..’akasema shangazi.

‘Wewe kwasababu ya ushamba wako, umekimbilia kuolewa na huyo mume asiye na mbeel wala nyuma, tafuta mume mwenye nacho, wewe nione hivihivi, nimechuja na kuwa na uhakika kuwa hicho chombo cha Uganda kitanifiksiha mbali, …kwanza unamuonaje, …sasa sikiliza, tukubaliane mawili, mimi nitaitunza hii mimba, lakini kwa msharti, kwamba ufanye kila juhudi kuiahirisha hiyo harusi, nitatoweka kabisa hapa nchini hadi nitakapo jifungua, baada ya hapo nikirudi nitajua la kufanya, sawa, vinginevyo, tusijuane..’akasema huyo mrembo, maana siku hizo hizo alikuwa mrembo wa kikweli.

Mrembo huyo akasafiri kuelekea Uganda ambapo ndipo anaposafiri baada ya kumpata tajiri wake, huku nyuma ikabakia kazi ya shangazi kutafuta njia kuiahirisha hiyo harusi, na ukatoke gomvi mkubwa kati ya shangazi na kaka yake, kwani hakuwa na hoja ya msingi ya kumwambia kaka yake, na kaka mtu akasema asijuane kabisa na dada yake, na ilichuku muda sana watu hawa wawili kuongea, hata waliposuluhishwa na wazazi, lakini chuku ilikuwa haisemeki, kaka mtu akisema dada yake anajua wapi mpenzi wake alipo, na hataki kumtajia kwanini..

Siku zikaenda na siku moja, shangazi akiwa katulia na mume wake akapata simu, na alipoiskiliza akakutana na sauti ile iliyomchafua moyo wake,hakuwa ana hamu tena na rafiki yake baada ya kumfanyia aliyomfanyia, sauti ile ikajaa masikioni, alitaka kuikata ile simu, akijua kuwa huyo mtu ndiye aliyevunja udugu wake na kaka yake, lakini kumbukumbu za urafiki wao, zikamzidi na akataka kusikia nini anachoambiwa;

‘Sikiliza wewe mwanamke,hapa nilipo nakaribia kujifungua, sasa naomba ufike huku Uganda,chapu chapu,maana hii mimba inaniletea matatizo,madocta wanasema nina mapacha, na mimi nitawaleaje hawa mapacha, na biashara zangu hizi, na hata mume wangu hataki watoto , sembuse mapacha…’akasema huyo mrembo.

‘Hivi nyinyi watu mna akili kweli…huyo mume wako ni binadamu kweli…kwahiyo unasemaje..?’

‘Sikiliza nimewahi kuongea na kaka yako nikamwambia kuwa nilikuwa nina mimba yake, sikutaka kumficha, na siku hiyo sikuwa najua kuwa nina mapacha, sasa huoni hapa mambo yamejiseti, ni mchezaji wa kimataifa, huyu huku atapata mzigo wake, hata kama ni kubambikiwa safi tu, iliomradi keshakubali, na kaka yako atapewa zawadi yake, mambo yamekwisha, njoo haraka, la sivyo utasikia mengine baadaye, tusije tukalaumiana…’akasema kwa sauti iliyoonyesha kuwa anasikia uchungu.

Shangazi hakuamini, hakujua kuwa rafiki yake kabadilika kiasi hicho ina maana pesa zimembadili hadi kuondoa ubinadamu, hakuamini… na alivyohisi alijua kama asipokwenda huko, hao watoto wanaweza wakatupwa, …au ..alishindwa hata kufikiria mabaya mengine, na kesho yake akachukau ndege hadi Uganda na kweli alipofika hospitali kama alivyoagizwa, akakutana na rafiki yake huyo akiwa tayari anapelekwa `leba’ tayari kwa kujifungua.

‘Sikiliza kama nilivyokuambia, wakitoka hawo mapacha, mmoja chukua, sitaki hata kumuona huyo mmoja utakayemchukua na mwingine utaniletea mwenyewe, wewe fanya ufanyalo, kama ni matumizi nitakutumia kinamna yangu nijuavyo, lakini sitaki kujua zaidi…huhitajiki kujua kwanini nafanya hivyo, lakini ipo siku nitakusimulia, usione watu matajiri ukafikiri utajiri wao ni wa hivihivi, watu wana imani za kiajabu ajabu we acha tu, sasa ili kuliondoa hili, wewe nisaidie hilo, mungu atanisamehe, na ipo siku nitakusimulia zaidi…’akasema huku akigugumia uchungu.

Na kweli mungu ajalia watoto wakazaliwa na afya njema kabisa, na shangazi akafanya kama alivyoambiwa, akamchukua mtoto mmoja, na mwingine akamfikishia rafiki yake, ambaye alikuwa kachoka, hakuwa na raha, lakini inavyoonekana hakuna na jinsi , ni lazima tendo hilo lifanyike..

‘Sawa rafiki yangu nimefanya kama ulivyoniagiza, lakini, sitakusahau katika masiha yangu, wewe umenifanya nikosane na kaka yangu, na family yangu, na pili unafanya unyama huu, sitakuelewa kabisa….’akasema Shangazi.

‘Ndugu yangu wewe ni rafiki wa kweli, umeifaa wakati wa dhiki, sitakusahau katika maisha yangu, hujui umenisadiai kiasi gani, lakini siwezi kukuambia kwanini imetoeka hivyo, ila nakuomba unisamehe, na nakuomba mlee huyo mtoto, sizani kama kaka yako atakubali huo mzigo, kwani lilipoongea naye kweney simu aliniita Malaya ninayetaka kumbambikia mimba zangu za umalaya, sasa wewe achana naye, mlee huyo mtoto, na majina yao, kwa vile ni mabinti wataitwa Rose na Maua…unasikia, sasa chagua wewe unataka jina la Maua au Rose..?’ akasema huyo mrembo.

‘Kwetu ni Kiswahili nitachagua Maua, nakutakia kilalaheri, lakini ujue kuwa mungu hachezewi, utatafuta mtoto usimpate, huwezi jua kuwa huenda hawa ndio waliokuwa Baraka zako, na wewe umamua kufanya hilo, …kwaheri, na kama huyo hutaweza kumtunza ni bora niondoka naye pia…’akasema shangazi.

‘Wala usifikirie kuwa kuna huyu huku, huyu ndiye roho yangu kwa sasa, nitamlea kama mtoto alwavyo, ila inabidi nifanye hilo ambalo sikulitegemea, huyo tajiri ana mambo yake ambayo hayaeelzeki, lakini hayo hayakuhusu ilimradi pesa ipo sijali, huyu usijali hana neno kabisa …atalelewa vyema kabiasa, wasiwasi wangu ni huyo maana sasa unasafiri naye…lakini kama nilivyokuambia, usiniweke roho juu na mengine, sitaki kusikia lolote kuhsu huyo, labda kama utahitaji pesa za matunzo…sawa..kwaheri….

Shangazi akamchukua Maua na kufika naye Tanzania, alichofanya ni kumuita kaka yake kumwambia kuwa mwenzake kajifungua na mtoto ndiye huyo kaja naye…ilikuwa kama katonesha donda, kwani kwa wakati huo kaka yake alishaona mke na kwa kipindi hicho naye alijifungu mapacha..kwahiyo hakuhitaji mzigo mwingine zaidi.

‘Dada kila nikijaribu kuyasahau haya machungu unaniletea machungu mengine, kwanini mnataka kuniua kwa chuki, kwanii dada unataka kuvunja udugu wetu, kwa alzima, huyu malaya unamuona wa maana kuliko hata mimi ndugu yako, au sio…’akafoka kaka mtu, lakini dada mtu alitumia hekima hadi akamweka sawa ndugu yake, na alipoona katulia akasema.
‘mtu hata siku moja hakimbii damu yake, wewe unishukuru nimeipigania hadi kuileta hapa, je angaamu akukuficha, na kusihi nayo…?’ akasema shangazi mtu.

‘Asingeliweza huyo Malaya, kwasababu alishanipigia simu mapema kuwa ana ujauzito wangu, lakini sikumwamini, hebu niambie, hiyo mimba nilimpa lini,…ilinipa shida kuamini hivyo, licha ya kuwa nilikuwa na mahsiono naye, lakini kwanini asingelianiambi mapema, .. wakati ananikataa kufunga ndoa, hebu niambia hata kama ingelikuwa wewe ungelimuamini mtu kama huyo, …sijui, kama ni kweli au la, lakini nakuomba kaa na huyu mtoto, nitasaidia kila iwezekanavyo, lakini akikua ili kuondoa dukuduku langu, nitakwenda kupima, kuhakikisha kuwa kweli ni damu yangu, na kama siyo damu yangu,…sijui..’akasema kaka mtu.

Maua akalelewa na shangazi yake, hadi akawa Maua kweli, na tangu alipokuwa mdogo alikuwa akijua huyo ndiye mama yake, lakini baadaye akawa anapelekwa siku moja moja kwa baba yake na huko ndipo anaambiwa huyu ndiye baba yako na huyu ndiye mama yako…akawa anachanganyikiwa, na alipomuuliza shangazi yake ilikuwaje, akaambiwa na shangazi yake huyo kuwa yeye alimpenda sana, na akamuomba amchukue akiwa mdogo, lakini kiukweli yeye sio mama yake, yeye ni shangazi yake…

‘Hapana mimi sikubali wewe ndiye mama yangu, sitaki kusikia hivyo kuwa wewe sio mama yangu , mnanidanganya, kwanini mnanidanganya hivyo….?’akasema Maua na kulia, na ilichuku amuda kukubaliana na usemi huo

Hakupenda kabisa kusikia hivyo, kuwa shangazi sio mama yake, mwanzoni alipata taabu na akawa analia, lakini baadaye alipopewa maelezo na umri ukawa umepevuka, ikabidi akakubali shingo upande, lakini hata hivyo hakuwa karibu sana na mama yake huyo wa kufikia , ingawaje hakuambiwa kuwa huyo ni mama yako wa kufikia, hilo lilifichwa kabisa, waliokuwa wanajua, baba, shangazi na hata huyo mama, walikula amini ya kutokusema lolote kwa watoto wao . Cha ajabu Maua hakuweza kumchukulia kama mama yake…hata pale alipojaribu kufanya hivyo moyo wake ulikuwa haumkubali kama mama yake mzazi. Sio kwamba aliteswa au kuonyeshwa chuki yoyote ile, lakini ni hisia tu zilijijenga kwa.

‘Maua mwanangu kwanini ukija huku hutaki kuwa karibu na mimi sana, kama wenzako, mimi ndiye mama yako,licha ya kuwa umekuwa ukilelewa na shangazi yako, lakini wewe na wenzako hamna tofauti, ukija hapa udeke kama mtoto atakiwavyo kudeka kwa mama yake, au kwanini unakuwa kama unaniogopa ogopa…?’ siku moja mama huyo akamuulizia.

‘Wala sikuogopi mama, tatizo ni kuwa sijakuzoea tu, kama nilivyomzoea shangazi, yeye ndiye nimekulia kwake, nijijua nipo naye, na sikujua kabisa kuwa yeye sio mama yangu,..’akasema Maua.

‘Ndio utamaduni wetu, unajua mimi nilizaa kwa karibu karibu sana, kama unavyoona hampo mbali mbali sana na ndugu zako hawa, kwahiyo ili kupunguziana majukumu ndio wewe ukachukuliwa na shangazi yako…alikupenda sana,…lakini hata hivyo usijali sana, nakupenda sana mwangu, jisikie huru kama wenzako..sio kwamba nilikuteleekza kwa Kiswahili chenu cha siku hizi…la khasha…’mama yake huyo alijaribu sana kumweka karibu kila walipokutana, na hakuonyesha ile tofauti ya moja kwa moja, lakini kwa Maua haikufanikiwa haraak hivyo.

Siri hiyo ilifichwa sana, lakini ikaanza kuvuja, na watoto wa mama huyo wakawa wakati mwingine wanaongea peke yao, kuwa Maua sio mtoto wa mama yao, na hili liliposikika, baba aliwakalisha kikao na kuwasema kwa hasira, kumbe baba huyu hakujua kuwa kuongea vile ndio kulifanya mioyo ya watoto ianze kupekenyua kutaka kujua ukweli, hata Maua hakuacha kuulizia hilo kwa shangazi yake, licha ya kuwa wazazi hawa walijitahidi kuficha ile kuna wambea wapembeni waliojua wakawa wanatoa siri hiyo.

Siri ya maisha ya familia hii ilibakia kwa kiasi kikubwa mikononi mwa shangazi, kwani yeye ndiye aliyebeba dhamana kubwa zaidi kuliko baba mtu, kwani yeye ndiye aliyeshuhudia kuzaliwa kwa Maua, kulelewa hadi hapo alipofikia, na baba mtu hakujua mengi zaidi ya hayo aliyoambiwa na dada yake. Lakini hauchi hauchi kunakucha, siri ya familia hii ikaanza kuvuja, na chanzo kikubwa ni hiyo ajali ya MV,Bukoba, pale Rose alipokutana na huyo mgonjwa…

*****

‘Haya sasa niambie wifi za kutangulia hebu niambie hali ya huyo mgonjwa, maana mimi nilimuona akiletwa tu, huwezi amini aliletwa hapa hajitambui, …yupo yupo tu, …hata sasa siamini kuwa atapona, …’akasema wifi huku akigeuka kuangalia kitandani ambapo alilazwa huyo mgonjwa, na wao walikuwa wamekaa pembeni ya kutanda ambacho Maua alilazwa na kwa na Maua alishafunua macho, lakini hakuwa anaongea, alinyamza kimiya tu.

‘Msimsumbue huyu mgonjwa,mwacheni kwanza akili yake itulie, …inaonyesha kapata mshituko mkubwa, sasa kwa hali yake ilivyo hahitajiki kusumbuliwa…’akasema yule docta, na wifi akamwangalia shanagzi kutaka kujua zaidi.

‘Unajua Rose anasiri sana, sikujua kabisa kuwa ana ujauzito…sijamuuliza vyema ni ya nani,lakini uhakika ni inawezekana ni ya huyo mgonjwa, ndio maana kamganda kama ruba…sasa wifi tumekuwa tukiongea kwenye simu, na wewe ukawa unanipiga chenga, safari ile nikaja ukanificha nisimuone mtoto, hili limenikera sana, na imefiki ahatua naota ndoto za ajabu sana, …nataka nimuone mtoto wangu yupo wapi, umemuacha wapi, maana hapa moyo unapita kutaka kumjua yupoje, sura yake…na sijui nitajielezaje kwake, mungu anisamehe na anipe huo ujasiri, maana sio kusudio langu…hutaamini namuota mara kwa mara, lakini sura ninayoiona ni ya Rose….

‘Mbona umeshamuona mwanao tayari, wasiwasi wako tu, lakini kabla sijakutambulisha kwako, nahitaji ile ahadi yako, maana ahadi ni deni, ..’akasema Shangazi kwa utani na kule kitandani alipolala Maua kukaonyesha kuwa mgonjwa kazinukana na anaongea na docta.
.
‘Kweli ahadi ni deni, …zawadi yako hii hapa..’ wifi akiwa na uso wa furaha alipoona yale yanayotokea kitandani, haraka haraka akawa anatoa kitu kwenye pochi, na mara ghafla mlango ukafunguliwa na wote wakageuza nyuso zao kuangalia mlangoni…na nyuso zikaonyesha alama ya mshangao, kila mmoja akabakia kujiuliza bila majibu, na mihema ikaongezeka, na macho, akili zikawa zinajiuliza kulikoni, na hata bila kuambiwa kitu wote kwa pamoja wakageukia upande ule wa kitandani, ….

******

Je siri hiyo itafikishwaje kwa walengwa, ndugu wapendwa wa blog hii, kisa hiki kimegubikwa na mtukio mengi tofauti, lakini chanzo chake kilitokana na ajali hiyo ya MV Bukoba, kutokana na ajali hii ndipo tukafanikiwa kugundua siri ya familia hii, ya mungu ni mengi, unaweza kusema bila hii ajali huenda haya yangefunikwa au yangegunduliwa kwa njia nyingine…hatujui.

Nawashukuru sana wale wote waliochangia kwa maoni na hata wale wenye moyo kutaka kuchangia kigharama …kwani kwa ujumla inabidi nigharimie ili kufanikisha hii blog, lakini haitakuwa jambo jema, kama nitakubali kuchukua mchango wowote kwa mtu, bila mimi mwenyewe kujipanga vyema, …au mnasemaje, huenda kuna njia nyingine mbadala sijui kwa sasa.

Kuhusu sehemu ya kujishikiza, bado nipo pale pale napigwa danadana kama mpira wa kitenesi, mara kapumzike kidogo, mara njoo…ndivyo maisha ya bongo yalivyo…hata hivyo kutumia vifaa vya watu inakuwa ngumu, mtandao na komputa zao, inabidi kutafuta muda wa ziada hasa asubuhi sana kabla wenyewe hawajafika,….lakini wiki mbili hizi nilikuwa nyumbani, na ndio nikawa natumia internet café, leo nipo ofisini tena, nimekuta mtandao haupo, nimekuja kusikia nitaambiwaje…tupo pamoja na mungi ndiye mtoa riziki. Nawatakia IJUMAA NJEMA

Ni mimi: emu-three

1 comment :

Anonymous said...

Mambo mazuri mkuu, ijumaa njema na wiki endi njema, twashukuru kwa kutujali, nauliza tukitaka kukuchangia gharama tufanyeje, angalau kama una Mpesa, au Airtel pesa, tupe namba yako.