Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, December 9, 2011

Akufaaye kwa dhiki ndiye rafiki wa kweli-61 Hitimisho-5




‘Maua kuna safari nyingine imetokea bila kutegemea, tena hii ni safari ndefu kidogo, na...na hatuna jinsi inabidi tusafiri tu kwa minajili ya kukuwezesha kujua mengi na kupata jibu mojawapo la swali lako, la kwanini watu wanakuita Rose, na wakati wewe ni Maua, pia kwa jili ya kumuona huyo mgonjwa,...hisia zangu zinanituma kuwa huyo mgonjwa ni mtu tunayemfahamu, bado sina uhakika...’akasema Shangazi.

‘Safari ya kwenda wapi tena shangazi, maana hii ya kuja huku mumenichukua juu kwa juu, na hata kabla, sijajua kwanini nimekuja huku mumezua safari nyingine. Shangazi,.... halafu tena unasema kuna safari nyingine, haya niambie safari ya kwenda wapi tena…na hilo jina la Rose liishie hapa hapa, silitaki kulisikia…umesema safari ya wapi..maana nisiongee sana, mimi sasa nimekuwa bendera fuata upepo?’akauliza Maua.

Shangazi akamwangalia Maua kwa muda, halafu akasimama na kutembea hadi dirishani na kuangalia huko nje bila kusema kitu kwa muda.

‘Maua unakumbuka wakati ukiwa mdogo, uliwahi kuniuliza swali moja ambali nilikuahidi kuwa nitakujibu ukiwa mkubwa, unalikumbuka hilo swali lako, au umesahau?’ akauliza shangazi .
Maua akashikwa kichwa akikumbuka swali gani, kwani amewahi kuuliza maswali mengi na hakupatiwa majibu, ndipo akaumbuka swali moja ambalo aliliuliza akiwa mdogo, lilikuwa kuhusiana na yeye kutokulelewa kwanini wazazi wake hakuwakumlea yeye na badala yake amejikuta akilelewa shangazi yake , mpaka, ilifikia mahali akaona labda shanagzi ndiye mama yake anamficha tu.

‘Shangazi kwanini nikuite shangazi,… mimi nakuona kama ndiye mama yangu, kwasababu wewe ndiye uliyenilea toka utoto, sikumbuki kulelewa na mtu mwingine zaidi yako, na mama na baba yangu wanakuja kuniona kwa muda tu, kwanini hawakunilea wao wenyewe wakati wana uwezo wao…?’aliuliza Maua akiwa mtoto mdogo.

‘Wewe unataka uniite mama, badala ya shangazi, lakini mimi sio mama yako utaniitaje mama yako, mimi ni shangazi yako, ….mimi na baba yako tumezaliwa tumbo moja, ila mimi niliamua kukuchukua wewe ni kule mwenyewe, kwasababu nakupenda sana, kwani hapo kuna ubaya …?’akasema shangazi.

‘Ina maana wazazi wangu hawanipendi, …?’ akauliza Maua.

‘Sina maana hiyo kuwa hawakupendi, ila mila na desturi zetu ndivyo zilivyo, kuwa kama unataka mtoto ndani ya familia unachukuliwa na kulelewa na huyu au yule, hakuna ubaya, ila mengine utayajua ukiwa mkubwa, kwasasa wewe niite shangazi yako , na wazazi wako bado wanakupenda sana huoni kila mara wanakuja kukuona, ….’akasema shangazi.

‘Haya nikiwa mkubwa nataka nitakuuliza tena, kwanini mama hawakunielea wao hata kama wananipenda, ..’akasema Maua.
‘Sawa ukiwa mkubwa nitakusimulia mengi, ambayo sasa hivi hustahili kuyafahamu, tuombe uzima tu..’akasema shangazi.

***
‘Shangazi kweli umenikumbusha, sasa ni wakati muafaka wa swali moja nililowahi kukuuliza kuwa kwanini umenichukua nikiwa kinyaa, kitoto kichanga, kama ulivyoniambia, ukanilea hadi leo, kwanini wasinilee baba na mama, mama alikuwa na mataizo gani, hata hivyo , niliwasikia ndugu zangu wakisema mimi sijazaliwa na yule mama yangu, niliskia wakiteta, na nilipowauliza wakaka kimiya…hebu niambi ukweli mama yangu mzazi yupo wapi, …?’akauliza Maua.

‘Kweli Maua sasa umekuwa mkubwa, na huu ni muda muafaka wa kukuambia ukweli, lakini sio mimi nitakaye kuaambia huo ukweli, utaambiwa na mhusika maalumu, ambaye tutakutana naye kwenye safari yetu hiyo, …’akasema shangazi.

‘Hiyo safari ya kwenda wapi tena, hujaniambi tunatakiwa kwenda wapi tena, na huyu mtu maalumu ndio nani…?akauliza Maua kwa mashaka.

`Tunakwenda India,..’ akasema shangazi na mara simu ikalia na shangazi akaipokea, akasikiliza kwa muda halafu akamgeukiwa Maua, na kusema;

‘Kila kitu kimewekwa sawa, tunakwenda kwa kibali cha kumuona huyo mgonjwa, na tiketi kila kitu kimeshakamilishwa, kwahiyo tupo safarini, …..huko tutamaliza kila kitu, kila kitu utakijua, na isitoshe lengo letu la safari ni kuja kumuona huyo mgonjwa, na itakuwa ni ajabu kubwa kama tutarudi nyumbani tukaulizwa mgonjwa anaendeleaje, tutajibu nini..bahati iliyoje kila hatua tunakuta mipango imeshapangwa, ….najua akili yako inatatanishwa na huu mlolongo wa siri, lakini haya yote yamefanyika kwa sababu maalumu, na isikutie shaka, kabisa, ingawaje najua kaka atagomba sana, lakini sioni kwanini usijue ukweli…’akasema shangazi.

‘Ukweli gani huo ambao wewe huwezi kunifahamisha, shangazi wewe ndiye ukiniambia jambo naliamini, kwanini usinisambie wewe mwenyewe….’akauliza Maua.

‘Hapana ukweli huo utaambiwa na wahusika wenyewe, nataka hili litoke kwenye kinywa chao wao wenyewe, …usijali, utafurahi sana, ingawaje bado nina mashaka na huyo mgonjwa, kwani sijawa na uhakika kamili kuwa ni nani hasa,…ni kaka yako mwingine ambaye humjui au ni mtu mwingine ambaye nashindwa kumkubali akilini,….lakini yote tutayajua huko….’akasema shangazi.

‘Nina kaka mwingine ambaye simjui, tulizaliwa tumbo moja, anaitwa nani, mbona hamjawahi kuniambia….shangazi kwanini mnanificha mambo mengi kama hayo, kama tungekutana na huyo kaka kimjini na hata kuoana mngelisemaje…!’akasema Maua.

‘Sio kosa langu ni kosa la wazazi wenu, mimi ni shangazi tu, na hayo niliwaonya sana, nikaonekana mtu mbaya, lakini hakujaharibika neno, tuombe uzima, utajua kila kitu , hata kama tumechelewa, ….ila huyo mgonjwa, ….tusubiri tuone kuna nini na ni nani haswa, maana hata huyo niliyewasilina naye hakutaka kuniambi ukweli kuhusu huyo mgonjwa, eti mpaka tufike huko, tukamuone wenyewe kwa macho yetu…’akasema shangazi.

‘Sawa ngoja na mimi nikaione hiyo India nasikia kuna watu matajiri sana, na kuna watu masikini sana, hata kuliko kwetu, ni kweli shangazi,..?’akauliza Maua na kabla shanagzi hajajibu, mlango ukagongwa na akaingia Inspekta. Maua akainuka haraka na kuondoka hapo ndani na kukimbilia chumba kingine, akamuacha shangazi akiongea na Inspekta.

‘Binti yangu huyu, mimba yake haitaki wanaume, nahisi ni kudume kipo tumboni, haya sema mkuu, kuna lolote jipya, aua ni kama tulivyoongea,

‘Hakuna jipya, maana naona kila kitu kinakwenda kama tulivyotaka, kama tulivyoongea sina mambo mengi sana ya kujua kutoka kwenu. Nimewadhamini kuwa hamuhusiki kwa lolote lile,kwahiyo mambo mengina nakuachia wewe mwenyewe na binti yako, kwani kwa upande wetu tumeshamalizana, ila kwa huyo mgonjwa bado ana kesi ya kujibu,akipona tu, ni vyema akaja huku wakamalizana na wahusika, maana mimi nitakuwa sipo nitakuwa kwetu, ..najua hakuna lililo bakia ingawaje kuna mtu mmoja katoweka kiajabu, hatujui katowekaje, ..’akasema Inspekta na kushika kichwa akijikuna.

‘Hayo ni mambo yenu, naona mumepigwa changa la macho, ….mimi sijui kama ananihusu sana, maana sikuwahi kumjua kabla,..ni sijui kama huyo binti atakuwa anajua alipo, naombeni msije kumhangaisha, tafadhali, …’akasema shangazi.

‘Atapatikana tu, maana miradi yake ipo na hospitali aliyokwa akifanyia kazi bado ipo, na nyumba zake, na kumbe alikuwa na miradi yake mingine aliyokuwa akiimiliki kisiri, sizani kuwa ataitelekeza, hutaamini kuwa hata hela za kumsafirisha huyo mgonjwa zimetoka kwenye fungu la hela zake alizoziacha kwa jina la Rose. Na Rose alipopewa hiyo taarifa akaagiza kuwa hela hizo zisaidie wagonjwa wasiojiweza hasa wanaotaka kusafirishwa kwenda India na mmoja wa watu aliowapendekeza wasafirishwe kwa hela hizo ni huyo mgonjwa wenu,…’akasema Inspekta.

‘Kwahiyo mnataka kusema Rose atakuwa anajua wapi alipo, ….hapana, huyo mtu ni mjanja sana, anataka kuwakoroga tu, katoa hizo pesa kwa maslahi yake, labda kwa vile ulivyosema alikuwa akimpenda sana huyo binti, bado hajakata tama…’akasema shangazi.

‘Hilo ndilo linalofuatiliwa na mikakati imewekewa kuhakikisha kuwa ananaswa, ama kwa kupitia kwa Rose, kama chambo au kwa njia nyingine yoyote, ingawaje Rose amekataa kata kata kujua wapi huyo mtu alipo,labda kuna lolote tunaweza kupata kutoka kwa huyo mgonjwa wenu..’akasema Inspekta

‘Nashindwa kukubali kuwa ni mgonjwa wetu au la, maana hakuna ushaidi wowote mpaka sasa wa kujua kua ni nani, nimewasiliana na jamaa yangu huyu aliyepo India kwenye biashara zake, lakini cha jabu na yeye kaamua kunificha, eti mpaka niende huko nikajionee mwenyewe , najua kwanini ananifanyia hivyo, siku nyingi amekuwa akitafuta mwanya kama huo, na hii kaiona ndio nafasi ya kufanikiwa malengo yake, sawa, kanipatia, nitakwenda tu huko…mengine yatajileta, heri nusus shari,…’akasema shangazi akimwangalia Inspekta kama anajua zaidi.

‘Mimi nilimjua hyuo mgonjwa kama ni mume wa Rose, sasa huo utata uliojitokeza baadaye, unaniweka nisiweze kusema lolote,…lakini hata hivyo kwasasa hakuna haja ya kuumiza vichwa vyetu, hayo yaliyobakia ni yenu ndani ya familia, mkikutana na huyo mgonjwa, mtajua zaidi, kama sio jamaa yenu au jamaa yenu, sioni kama kuna tatizo, na kama lipo linahitaji msaada wangu, usiogope kuniambia, au kunishirikisha,… ila hata hivyo kama ulivyonidokezea ndivyo ilivyo, bado ni jamaa yenu, ni mkwe wako huyo au sio….?’akasema Inspekta kama anauliza huku akiinuka kutaka kuondoka.

‘Sawa tutayaona huko huko, nisingependa kusema lolote kwa sasa,maana hali ilivyo inaniweka katika wakati mgumu, nimeamua kujichukulia maamuzi makubwa peke yangu, nogopa sana kuja kulaumiwa baadaye,lakini hata hivyo yote ni heri, na ndio maana sikutaka uongee lolote kwa binti yangu huyu, nataka kila kitu kiende kama vile kimetokea chenyewe, na naona ndivyo inavyokwenda….sitaki mwisho wa siku nivunje udugu wangu na kaka yangu…’akasema shangazi mtu. Na mara wakasikia sauti ya Maua ikiita kwa sauti kubwa, iliyomfanya shangazi alipukwe na moyo, akahisi kuna jambo kubwa limetokea tena...

‘Shangazi njoo huku uone, njoo haraka, nimeona kitu nataka kukuonyesha…’akasema Maua kuonyesha kuwa kuna jambo muhimu kaliona na shangazi mtu alitaka kuinuka haraka na kukimbilia huko kama asingekuwepo huyo askari, lakini akajikausha na kujifanya ni jambo la kawaida tu, na akamgeukia Inspekta na kumwambia;

‘Hayo hayakuhusu ni mambo ya kifamilia, tutawasilina zaidi , wewe ondoka tu, huyo najuana naye mwenyewe...’akasema shangazi huku akijiuliza kilini, huyu binti kagundua kitu gani huko ndani kilichomfanya apige ukulele, kiasi hicho, maana hakutaka kabisa jambo lolote linalohusiana na usiri uliopo ligundulikekabla hajaonana na mhusika mwenyewe, akainuka kwenda huko alipoitiwa, na alipofika mlangoni simu yake ikaita na akaipokea harakaharaka bila hata kuangalia ni nani aliyepiga hiyo simu,....

‘Dada ndio umefanya nini, nani aliyekuambia umchukua binti yangu hadi huko bila ruhusa yangu, mbona unakiuka masharti yangu, tulikubaliana nini,…kama wewe ni ndugu yangu,…nataka mrudi haraka huku na binti yangu….!’sauti ya ukali ikasikika kwenye simu. Shangazi akajikuta akiishiwa nguvu, sasa mambo yammeharibika...ooh, nitafanyaje...

NB Haya shangazi atachukua hatua gani, kumbe aliondoka bila kuaga, na huku safari nyingine imeibuka, hiyo safari ni kwenda kuonana na nani...?, maswali mengi yanahitaji majibu, tusaidianeni! tuwe pamoja!

BLOG YAKO INAKUTAKIA MAPUMZIKO MEMA YA KUSHEREHEKEA SIKUKUU YA UHURU , HATA KAMA NI KWA KUFUNGA MKANDA, SIO MBAYA

1 comment :

Anonymous said...

Mkuu usijali tupo nawe kimia kimia