Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, July 11, 2011

Dawa ya moto ni moto-33


 Maneno aliona moto mkubwa ukiwala mbele yake, alitizama vyema akagundua kuwa moto huo unawaka kwenye nyumba yao, akajaribu kuisogelea ili kuangalia vyema, lakini ule moto ulikuwa mkali kupita kiasi, …akarudi nyuma, na moyoni akasema ngoja nikachukue maji niumwagie ule moto kabla haujashika nyumba nzima, lakini hakuona chombo cha kuchotea …wala maji yaliyopo karibu, na wakati huo huo akawa anasikia sauti ikiita jina lake,…`Maneno, Maneno…’  akawa anajiuliza ni nani huyo anayemuita, mara akasikia sauti ikiongeza kwa kusema, `Maneno njoo uniokoe naungua na moto, mume wangu …jamani nakuufa…’
Aliposikia `mume wangu nakufa’ ndipo akakumbuka kuhusu mke wake, akawaza mbona yeye anakumbuka kuwa mke wake kaenda kazini, je alirudi saa ngapi akaingia ndani ya hiyo nyumba, akasema moyoni,…hayo ya kuwa karudi saa ngapi hayana umuhimu sana, cha muhimu ni kutafuta njia za kumuokoa mke wake…akasema kwa vile maji hakuna nitatumia mchanga….akajaribu kuchota mchanga ardhini, lakini ardhi ilikuwa ngumu kama jiwe…akaanza kuhaha, kwani moto ulikuwa ukiongezeka kwa kasi, na sasa ulikuwa ukimjia pale alipo, na kwa kasi ya ule moto ulianza kuzunguka nyumba nzima, na sauti ya mkewe ilikuwa bado ikiita kwa nguvu kuwa anaungua na moto…`mume wangu mbona unaniacha..nife kwa moto…tafadhali nakuomba uniokoe, njoooo, nakufaaa…., nakufa….;
 Maneno alishituka, na kuinuka pale alipokuwa amelala, kumbe ilikuwa ni ndoto mbaya, akajizoazoa pale mafichoni alipokuwa amelala, na kuanza kutafuta ustaarabu wa siku, kwani alishaanza kuishiwa na hakuwa na njia ya kurudi nyumbani kwake, akijua kuwa ama anatafutwa na polisi au wale maadui waliotaka kumuua…alishangaa kwanini amekuwa akiota ndoto za ajabu ajabu, na kila mara anamuoata mkewe akiwa anamuomba msaada, na anajikuta katika mazingira ambayo hawezi kumsaidia..!
 Nahisi kuna jambo limemtokea mke wangu, nawajibika kwenda kuangalia, lakini kwanini nifanye hivyo wakati kanisaliti…hapana cha muhimu nirudi kwangu kwanza niangalie nitaishije…alijiona atakuwa mwoga kuendelea kujificha, wakati hana kosa lolote, akatoka kule mafichoni, na kuingia mitaani, alichofanya ni kutafiti kuwa kule kwake kuna nini kinaendelea, aliambiwa na jamaa yake mmoja hakuna kitu chochote, basi akarudi kinyemela, na alipofika alikuwa vitu vimepangulia juu chini, akajua nini walikuwa wanatafuta, akaendea kabati lake la nguo, akakuta kumepangulia, na alipoinua pale anapoweka vitu vyake, akakuta kile alichokuwa anakitafuta, hawakubahatika kuviona vitu vyeka, na ule mzigo aliochukua toka kwa rafiki yake bado upo vile vile….
`Sasa, ni safari kwa baba mkwe, nikamuonyeshe huu ushahidi..sina utani tena na wasaliti…’ Moja kwa moja hadi kwa baba mkwe alipofika aliambiwa baba mkwe hayupo kaelekea `Ufukweni hoteli’ akauliza anawezaje kumpata, akaambiwa kama ana jambo la haraka amfuate huko huko, kwani atachelewa sana kurudi, kwani inavyoonekana kuna shughuli kubwa huko, wakubwa wengi  wamealikwa huko, na matajiri wa nchi hii nao wamealikuwa huko…, ! Akasema kimoyoni, hata masikini wa nchi watajialika huko, ngoa name niende huko huko, akashukuru akaondoka! Kwanza akarudi kwake na kuvalia nguo za shughuli, maana anajua huko hawataruhusiwa walivalia `kienyeji’, akavaa suti yake ya harusi…aaah, naye yumo, akamshukuru mkewe kwa kumjali …!Lakini moyoni alikuwa akijiuliza kwanini amfuate baba mkwe huko kwenye shughuli za watu ilihali hajaalikwa, hata havyo hakukata tama, kwani nafsi yake ilikuwa ikimvuta kwenda huko huko.
Akaingia kwenye bajaji, mpaka `Ufukweni Hoteli,  alipofika maeneo ya karibu, akaamua kutembea kwa miguu, ili kuangaza na kupata usalama zaidi , ilikuwa  bado mapema kwahiyo aliona magari yakija moja baada ya jingine…baadaye akajisogeza kwenye geti wanapokaa walinzi…kama alivyotarajia akaulizwa kuwa ana kadi ya mualiko, akabaki anashangaa, lakini alishajua nini cha kusema, akadai yeye ni mpiga picha, wa mzee mmoja anaitwa baba Maua na aliahidiwa kuwa atakunata naye hapo! Wale walinzi wakacheka, halafu kama vile hawakumsikia, wakawa wanendelea na kupokea wageni wengine, walishamuona kuwa ni muongo…wakamdharau na kumwanmbia akae pembeni kwani wao wana kazi leo, hawataki utani…!
 Baada ya muda kitambo, akaja mlinzi toka ndani akasema ‘Bwana nasikia gesi imelipuka humo ndani, kuna dalili ya harufu mbaya, wanasema ni kama `acid’ ikiingia mwilini, mwili unamomonyoka kama uji…’ akasema huyo mlinzi aliyetoka ndani
‘Acha uongo wako, gesi gani hiyo..mimi nimeingia, ni kweli kuna sehemu gesi imevuja, baadhi ya vyumba, na walikuwa katika juhudi za kumaliza hilo tatizo, …ni tatizo dogo tu, wewe unafikiri hoteli kama hii itashindwa kitu kidogo kama hicho…halafu nikuambie, wakati namsindikiza yule mrembo..wanasema anaitwa nani vile, yes, anaitwa Maua, au ndiyo huyu jamaa anasema anamtafuta baba yake nini…!’ akageuka kumwangalia Maneno ambaye alikuwa bado kasimama nje ya lile geti akiwa karibu kukata tamaa ya kuingia mle ndani, ingawaje masikio yake yote yalikuwa yakiwasikiliza wale walinzi wanachoongea, akijfanya hawasikilizi, ..lakini aliposikia wanataja jina Maua, akajisogeza karibu…ina maana hata Maua yupo humu ndani…lazima ajitahidi aingie humo ndani kwa njia yoyote ile, akasema kimoyomoyo..
Mara wakasikia kelele za mlio wa hatari…wale askari wakawa wanaulizana, na mmoja wao akaondoka kufuatilia kuna nini, yule mwingine akaingia kwenye kibanda chao akijaribu kupiga simu, na hapo hapo Maneno akapata upenyo wa kupita, haraka akaingia ndani, alipofika eneo la maegesho ya magari, aliona watu wengine wakiwa na haraka zao kuondoka hapo, walikuwa wakiingia kwenye magari yao huku wana mashaka shaka…ilionekana kuna kitu kimetokea huko ndani…alipoangalia kwa mbele zaidi kwenye eneo la baharini akaona kama boti linaingia pole pole…
Akavutiwa  sana na lile boti,…badala ya kutafuta nia ya kuingia ndani ya hoteli akaanza kwenda taratibu kulifuta lile boti hadi akafika eneo ambapo kuna ukuta umezuia kuingia upande wa pili yake…akatizama huku na kule, akaona ili alione vyema ni bora azunguke upande wa nyuma wa hiyo hoteli, akafanya hivyo mpaka akatokea nyuma ya lile jengo na akaona mlango wa unaingia upande huo wa pili akajaribu kuufungua, akaona unafunguka, akatokea sehemu ya pili yake na hapo akarudi kwa kujificha ukutanii hadi karibu na bahari pale alipoliona lile boti likiingia, alipofika akaona lile boti limesimama, akaona watu wanapakua maboksi wanaingiza kwenye kigari, kinaondoka halafu baada ya muda kinarudi kuchukua mengine…akasema kimoyomoyo, hiyo ilikuwa tenda safi, kama angewaona wenyewe, angejitosa, angepata vijisenti..lakini akakumbuka kuwa yupo mafichoni, akishikwa na walinzi ataulizwa nani kamruhusu kuingia humo, akaona ajifiche kwanza aone nini kinaendelea…
‘Huu mzigo ukiiuza mzee..utapata pesa mingi…veve vutakuwa tayiri…mkuwa sana..’ akasikia mzungu mmoja akiongea kwa Kiswahili cha shida, walikuwepo wazungu wawili…na yule mzungu aliyekuwa akiongea aliposhindwa kuendelea zaidi kuongea  kwa Kiswahili, akawa anaongea kwa kiingereza…Maneno akawa anajaribu kuchunguza wapo watu wangapi pale, aligundua kuwa wapo wazungu wawili na waafrika watatu, na akwa anajiuliza yale maboksi yatakuwa na mizigo gani …akajilaumu kuwa yupo mbali, alitakiwa asogee ili agundue zaidi…akasogea kwa kujificha ficha…!
 Wale watu walipomaliza kupakua hiyo mizigo kwenye lile boti, akaliona lile boti, likigeuza kuondoka, lilionekna linarudi huko lilipotoka, na wale watu wakaingia ndani ya hoteli kwa kupitia mlango mmoja ulioonekana hapo, na hapo Maneno akapata nafasi ya kujipenyeza hadi akafika eneo ambapo wale watu walikuwa wamesimama awali, …aliangalia huku na kule kuhakikisha kuwa kuna usalama, alipoona kimiya, alichunguza ule mlango , haujafungwa moja kwa moja, nusu ulikuwa wazi, akachungulia kwa ndani na kukiona kile kigari kidogo kama `mkokoteni’ kimesimamishwa pembeni,na kwa ndani aliona sehemu ya `lifti’, …Maneno akajiuliza afanyeje, kaona ni hatari,…kwanza akajiuliza kwanini hawajafunga ule mlango…ina maana bado watatoka nje…au hawajamaliza kazi zao…hakutaka kupoteza muda zaidi akaingia kwa ndani, na bahati nzuri akaona kuna ngazi zinaelekea kwenda chini, …akajiuliza huko chini kuna nyumba,…lazima ajue hiyo nyumba ya chini ipoje, akaanza kushuka kwa kutumia zile ngazi za kwenda chini….!
 Alishuka kidogo kidogo kwa tahadhari na alishngaa kuona kuwa nagzi hizo zilikuwa zilikimpeleka chini sana, na kujiuliza ina maana ni shimo…., mara akafika mahali kuna mlango akajua lazima kuna sehemu nyingine inatokeza kwenye jengo kubwa, lakini huku ni chini ya ardhi, atatokea wapi, akaona ajaribu kuufungua ule mlango ajionee mwenyewe kuna nini, akaufungua, akaona ni kama uvaranda ambao unaingia sehemu kama jengo, na kuna ofisi nyingi upande wa pili yake,…akawa hana shauku ya kuzichunguza zile ofisi, shauku yake ilikuwa kuona zile ngazi zinishia wapi, kwani bado zilikuwa zinaelekea kwenda chini, akaurudishia ule mlango, na kuendelea kushuka kwa kutumia zile ngazi kwenda chinii…
 Akiwa na shauku wa kujua hizo ngazi zinatamfikisha wapo ,mara akatokea kwenye mlango mwingine ambapo ngazi zimefikia kikomo, taratibu akaufungua ule mlango , na akasikia watu wakiongea…alipochungulia kwa ndani akawaona  wale watu watatu aliowaona juu, wakiwa na wale wazungu wawili wamesimama,…walikuwa wale wale watu watano, na walionekana kuwa wanajadili jambo fulani, akajipenyeza taratibu hadi akaingia na kujikuta nyuma ya maboksi yaliyojazana hapoi, alipowachunguza wale watu ,walionekana hawana wasiwasi, kwani hakuna aliyeonakana kugeuka huku na kule …na kumpa nafasi Maneno kuingia hadi kwenye varanda inayoelekea kule walipo, na hapo pia palionekana kuna vyumba, lakini havionyeshi kuwa ni ofisi, kutokana na milango yake kuwa kama ya mageti na imara zaidi…..
Akaona ajifiche nyuma ya maboksi ambayo yalikuwa hayana kitu, kuwachunguza wale watu wanafanya nini, akatulia hapo kimiya, baadaye wale wazungu wawili waliingia kwenye lifti wakaondoka, wakabakia Waafrika watatu, wakawaka wanaingiza baaadhi ya maboksi ndani ya chumba na wanatoka na maboksi matupu ambayo waliyarushia pale Maneno alipojificha
‘Hii ndiyo yenyewe, ukisikia madawa ya kulevya ya asili ndiyo haya mzee, au unasemaje mkuu…?’ akasema mmoja wapo
‘Jamani nahisi kuna harufu…au pua yangu inahisi yenyewe…’ akasema jamaa  aliyeitwa mkuu…akawa ananusa huku na huku.
‘Hata mimi nimeisikia muda mrefu..lakini …kuna jambo..’ akasema huyo mwingine ambaye alionekana ana kitambi kidogo, na alionekana kama mtu mwenyewadhifa kidogo
‘ Unajua nimeshangaa kidogo, kwanini nilipozima `remote’ ili mitambo ya kutoa gesi izime, lakini haikukubali…nikahisi kuna jambo, na kama ni hivyo, kuna kesi kubwa…duuh, sasa haya yatakuwa mauaji, haikuwa nia yangu…na wale wazee kule…anyway, wale wakifa sioni uchungu, ila Inspekta na Binti …Maua…ooh, hapana yule binti kule sikuamrisha gesi itoke…yeye atapona, ila hali ya hewa kule ni baridi sana, kama…ok, jamani ngojeni nipande juu,nyinyi rudini kwenye ofisi yenu, nitaawaambia nini cha kufanya, kama kuna lolote baya, mtajua la kufanya,…lakini kama kuna lolote baya nitahakikisha eneo lote hili linasambaratika kwa bomu, kwahiyo nikiwaamrisha mtoke, mtoke kweli, na huku najua kutakuwa salama…ila tahadhari kama lolote litatokea, muhakikishe familia yangu haiguswi na ….’ Akasema yule waliyemuita bosi.
‘Mbona unasema hivyo bosi…kama vile tunaagana, hakuna jambo baya, kila kitu kipo shwari…’ akasema mmoja wapo
‘Mimi machale yamenicheza, nahisi kuna hatari…hebu angalieni kile chumba nilichomweka Inspekta, ….’ Akasema yule wanayemuita Bosi inaonekana ndiye kiongozi wao….na yule ambaye alionekana mwenye kitambi akasogea kwenye chumba kilichokuwa mbele kidogo na kukifungua,… alikifunga haraka huku akikohoa na kusema…`hakuingiliki bosi….oooh..’ akawa anakohoa  mfulululizo
‘Sasa kwanini umeweza kukifungua…ina maana kuna mtu karuhusu milango ifunguke, hata kama Inspekta yumo humo ndani, atakuwa keshakufa…lakini,…milango nani kairuhusu ifunguke…?’akasema huyo kiongozi wao
‘Bosi kwa kutokufanya `romote’ isifanya kazi mimi ndio` niliblock’…kwasababu nilitaka Inspekta afe..yule ni mhasimu mkubwa kwangu, nilishakuambia siku nyingi, unajua nilivyo na uadui naye…unajua kile cheo nilikuwa nakililia sana, na isingekuwa yeye ningeshakichukua, au vipi mheshimiwa, yeye ndiye kikwazo kwangu…kwahiyo kama Inspekta kafa ni swala la kujipongeza kwani nitachukua ile nafasi, halafu mambo yatakuwa shwari…lakini kwanini milango ipo wazi..ngoja  mimi niangalia…maana muheshimiwa majambo haya hayaulii sana…’ akachukua `maski’ ya kuzuia hewa na kuivaa usoni, halafu akaelekea kule kwenye chumba, baada ya muda akatoka
‘Hili sasa ni balaa inavyoonekana Inspekta hayupo, keshatoka…sijui katokaje, …mambo sasa ni magumu…sasa, ngoja twende ofisini tukaangalia usalama, mimi baada ya hapa inabidi nirudi ofisini haraka iwezekanavyo…vinginevyo sijui itakuwaje, inaonekana mambo ymeharibika…naomba muweke mambo sawa, ndio maana nilikuwa natamani tungemumaliza huyu mtu mapema…’ akasema huku wanapanda ngazi kidogo kwenye ofisi iliyopo juu kidogo na wakafungua mlango na kupotelea huko ndani, na yule waliyemtambua kama kiongozi wao, yeye alibakia hapo akiwaza na baadaye aliingia kwenye lifti huku akisema kwa sauti …`hayo ni kawaida tu, labda wakati umefika, wakati umefika, …moto uanze kuwaka….nafikiri namba ya kutumia kwenye lile boomu ni namba one three, nine seven nine…au sio waungwangwana…safi kabisa waungwana, tupo pamoja…’akawa anabonyeza hizo namba kwenye simu yake, na kunyosha mikono juu kama anaomba kitu. Maneno naye bila kujua kwanini akawa anayakariri zile namba kimoyomoyo  `namba one three nineseven nine’
Alipoona kupo shwari akatoka pale mafichoni na kuelekea kwenye ile lifti, aliifungua ka kuingia ndani yake, akajaribu kubonyeza iende juu, lakini ikawa haisogei, alipoona hivyo akatoka haraka na kujiuliza afanyeje…baadaye wazo likamjia kuwa, arudi tena kwenye zile ngazi alizokuja nazo hadi kule juu alipoona kuwa kuna kama ofisi, akafanya hivyo hadi juu, kwa hivi sasa liona kazi kweli kupanda juu, aliona kama kumezidi kuinuka zaidi… akajitahidi mpaka akafika sehemu ile ya mlango aliouona kabla, na akaufungua ule mlango na kutokea sehemu zile zenye ofisi nyingi nyingi, akajiuliza aifanyeje…
 Kwa tahadhari akawa anafungua chumba cha ofisi moja baada ya nyingine,  kimoja baada ya kingine kwa uangalifu…alipofungua chumba cha tatu..ooh, alimuona mwanamama kalala sakafuni….akaingia haraka na alipomwangalia vyema, akagundua ni Maua….oooh, akaanza kuchanganyikiwa,…Maua tena,…. ina maana wale walinzi walikuwa wakiongea kuhusu Maua kumbe ndiye yeye mkewe, akamwinua na kuanza kumtingisha tingisha…akimwita kwa sauti ya chinichini…`Maua, Maua…..’ alipoona kimiya akaamua kumbeba hadi eneo la nje, kwani mle ndani kulikuwa na ubaridi mkali…alimtingisha tena na tena, halafu akakumbuka kuna njia ya kumrudisha mtu aliyezimia kwa kumpulizia kwa kupitia mdomoni, akafanya hivyo,…kimiya…akashika mapigo ya moyo kimiya…oh, mungu wangu ina maana Maua kafa…hapana, haiwezekani… na mara …..

NB. Ina maana kisa hiki hakiishi leo, maana naandika tu...mambo yanazidi kuja,... lakini ule mwisho haufikii…Hata, lazima nifanya kitu,... ngojeni tuishie hapa kwa leo, tuone sehemu inayokuja itatufikisha mwisho wa kisa hiki au bado…au nyie mwasemaje? Je Maua amekufa…na kumetokea nini baadaye, tuzidi kuwemo kwenye mfululizo wa hitimisho la kisa hiki..tusichoke jamani kwani natamani kisiishe, lakini kisipokwisha visa vingine vinalala.....



Ni mimi: emu-three

3 comments :

Anonymous said...

Aaaaaah!!!!!!! Boss mbona una2katishia mtamu tena??????

Lete mambo, mzee. sasa ndio kwanza kumekucha.
BIG UP, MY BOSS.

2PO PAMOJA BOSS WANGU. USICHELEWESHE MAMBO.

BN

samira said...

m3 upo juu unajuwa kisa kikiwa kizuri kinakuwa kirefu nahisi kinaweza kwisha mwisho wa wiki
mimi kwangu ni sawa tu hata kama kisa kinaendelea
sasa mambo na vipi bosi na mkewe imekuwaje bora nisubiri

emuthree said...

Bosi, bosi, hata mimi sipendi kukatishia patamu, ila muda unakweisha haraka sana, huku nyuma kasimama bwana mkubwa, unasikia unaulizwa, `what are you doing?' inabidi ukatishe tu hata kama palikuwa patamu...Tupo pamoja bosi, tuone itakuwaje, ...mungu akipenda kesho!