Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, June 17, 2011

Dawa ya moto ni moto-23



Inspecta akachukua chombo chake maalumu , ni kama peni ndogo hivi, inaweza kuwa tochii na pia inatumika kugundua vitu vya hatari ambavyo vimefichwa. Akakitoa kenye kiatu chake na kukiongeza urafu, halafu akakiwasha na kikaanza kutoa mlio wa hatari, akaanza kutafuta huku na kule mle ndani anapoishi, kwani alihisi lazima kuna kitu kipya kimepandikizwa humo ndani, alipofika hapo mara ya kwanza, alitafuta na hakuona kitu. Akajaiuliza nani aliweza kuingia humo ndani na kupandikiza kitu kama hicho, …hakuweza kugundua kwa haraka sana, na hisia zake kubwa zikawa kwa huyo dakitari wake, lakini aliondoa hilo wazo  akikumbuka yale maongezi aliyoyasikia siku ile ofisini mwa docta, akiongea na mgeni mwingine aliyemtembelea ambaye pia alikuwa ni dakitari.
 Akafuatilia ishara ya ile tochi yake hadi akakiona kile kidude , ni kidude kidogo sana kama betrii ya simu na kinanatishwa mahala popote ili kunasa sauti, na vingine hunasa matukio na sauti. Akachukua leso na kujifunga mkononi, ili akikiondoa asiache alama za vidole, akakichomoa pale kilipowekwa, kilikuwa kwenye kona ya chumba, na hii ilimpa shaka kuwa kile kilikuwa kinachukua matukio na sauti pia kwahiyo huyo aliyekiegesha kama yupo hewani, au akitaka kujua vyema atakuwa keshamgundua kuwa kagundua hicho chombo …hakujali, alikichukua na kukifungua na kuhakikisha kakizima na kuondoa vile vifaa vinavyokiwezesha kufanya kazi, halafu akakirudisha pale pale.
Hata hivyo ile tochi yake ilikuwa ikionyesha kuwa kuna kifaa kama hicho kipo mahala…lakini kiliashiria kuwa ni mbali na hapo, na sio humo ndani, akaingiwa na wasiwasi kuwa huenda docta wa hiyo hospitali alimua kuweka vifaa kama hivyo kwa ajili ya usalama, akaona ni vyema amuulize, asije akaingilia kazi ya watu au …kabla hajafikia uamuzi mlango ukagongwa, na akaingia docta, alionyesha uso wa wasiwasi, na Inspecta akahisi huenda ni kwasababu ya yale mazungumzo aliyoyasikia.
‘Vipi mtani mbona unaonekana kama umeona shetani kwenye ndoto…jana sijakuona siku nzima, hukutaka kumtembelea mgonjwa wako’ akasema Inspecta
‘Shetani? Aaah, hivi hata nyie maaskari mnaamini hayo mambo…aah, najiona ovyo, na ukizingatia leo sina wagonjwa na hawa mafundi wananichanganya, hawafanyi kazi yao haraka….ok, tell me, upo ok…’ akasema Docta.
‘Off course nipo ok, I always ok, na naona nichomoke humu ndani, sipaamini tena..’ akasema Inspecta.
‘Unataka ufufuke, au ukatalii kidogo, maana sioni kwanini usipaamini , wakati umekaa hapa wiki sasa kama …vipi iwe ghafla hivi….?’ akasema Docta.
‘Mtani, naona nitumie neno hilo,…machale ymenicheza, siunajua tena kazi zetu, lakini kwasababu wewe ni mtani wangu,  na ni ndugu yangu tumetoka mbali, nina jambo muhimu nataka kukuuliza, ila kama nilivyokuambia humu ndani…hebu nikuulize docta, una vyombo vya usalama humu ndani? ‘ akauliza Inspecta
‘Vyombo vya Usalama?’ Docta naye akauliza kwa mshangao na kumwangalia Inspecta, na alipoona Inspecta kakaa kimya akasema. ‘Mimi vyombo vyangu vya usalama ni vipimo vya matibabu, sijui ulikuwa na maana hiyo..’ akasema na kukaa kwenye kiti.
‘Hapana sikuwa na maana hiyo na nisingetumia msemo huo kama ningekuwa na maana hiyo, nauliza vifaa vya kurekodi sauti, kuangalia matendo ya wagonjwa wako hata kama upo ofisini, usalama wa wezi nk, najua wengine sasa hivi wanakuwa navyo kwa ajili ya  kuweza kuwaona wagonjwa wao au watu wanaoingia kwa ajili ya usalama …au hata kujua kwa haraka wagonjwa wao wana shida gani…’akasema Inspecta.
‘Hapana labda kama unanishauri kuwa niwe na vitu kama hivyo kkwasasa…ni wazo zuri, na nilikuwa nawaza hivyo, lakini nilikuwa nachelea kuhusu sheria, je inakubaliana na hilo, maana kuweka kitu ambacho utamnyima uhuru mgonjwa sipendelei,… ndio naweza kuweka bila wao kujua, lakini sio ubinadamu…unanishauri niweke vitu kama hivyo, au…?’ Docta akasema  kwa kuuliza.
Inspecta akamwangalia yule dakitari na mawazoni akawa kamuondoa kwenye lile kundi alilokuwa akilidhania vibaya, hasa akiunganisha na yale mazungumzo aliyoyasikia na kauli yake hii ya sasa, ila hakutaka kumwamini moja kwa moja,…alijua kazi yake haistahili kumwaminimtu mtu moja kwa moja.
‘Hapana sio kuwa nakushauri ufanye hivyo, ila kwa leo naomba uniruhusu nifanye kazi yangu ndogo, bila kibali cha ofisini, ni kwa manufaa yako, ….’ Akasema Inspecta na kabla Docta hajasema kitu Inspecta akatoa kile kitochi chake, akakiwasha na kuanza kufuatilia mshale unapomuonesha na docta akawa anakuja kwa nyuma yake akiwa na wasiwasi na mshangao, hakujua kabisa nini Inspecta anafanya. Alimfuata Inspecta kwa nyuma mpaka wakajikuta wanaingia ofisni mwake, na mara Inspecta akainama chini ya meza na kutoa kidude kama kile alichokitoa chumbani mwake, akakizima na kukikagua vyema, akaondoa baadhi ya vitu na kukishika mkononi akiwa anataka  kukirudiaha pale pale alipokichukulia.
‘Unafuatiliwa na watu…kama kweli hupo pamoja nao, basi ujue kila ulichowahi kuongea humu ndani umekuwa ukifuatiliwa…’ akasema Inspecta.
‘Weee, hapana maana jana nilikuwa naongea ….hapana oooh, hio sasa nii balaa, lakini nashukuru mungu nilisimamia kwenye ukweli, sikukubali na ujinga wao…au…’ akataka kusema kitu lakini akanyamaza.
‘Au, nini…wewe sema tu, maana hali ilivyo kwa ujumla inakwenda pabaya, na naogopa kusema kuwa hakuna wa kumwamini…hakuna waaminifu  tena, watiifu wa sheria ni wachache sana, …watu wote wamekuwa watumwa wa pesa…lakini ni uamuzi wako, labda mwenzangu unataka kutajirika…’ akasema Inspecta huku akikirudisha kile kidude mahala alipokichukulia.
‘Mbona unakirudisha tena hapo…’ akauliza Docta.
‘Kiache hapo, hapo, na kama inawezekana jaribu kuhakikisha hakuna mtu mwingine anaingia humu ndani wakati haupo, huwa mfagiaji anafagia wakati haupo?’ akauliza Inspecta.
‘Hapana mfagiaji hana ufunguo wa ofisi hii mpaka nifike, ..ofisi yangu hii haiingiwi ovyo, mfagiaji anasubiri mpaka nifike nifungue ndio afagie..’ akasema Docta.
‘Safi kabisa, sasa niambie nini unachojua kuhsusu kundi lolote, au nani aliyeingia humu ndani kwako karibuni…sasa nipo kazini, nauliza kama mtu wa usalama na hili ni kwa manufaa yako, kama ulivyoona,watu wameshakuwahi na nahisi wanakutafutia chambo, unase  wakupate…’ akasema Inspecta.
 Docta aliwaza sana, akajaribu kukumbuka watu walioingia mle karibuni, aliyemkumbuka wa karibuni ni rafiki yake dakitari, mpenzi sana wa rang nyekundu, huwa hata viatu anapenda vya rangi nyekundu. Alikumbuka jinsi alivyomshawishi kujiunga na lile kundi gani sijui, hakutaka hata kuliwaza, hakuona kwaninii ajiunge na makundi kama hayo ya hatari na hakuna ina maana gani kujiunga, eti kwasababu ya pesa, hapana, sidhani kuwa ndilo lengo pekee la kundii hilo lazima wana lengo jingine.
Akamkumbuka mtu mwingine, ambaye walikutana naye lakini ilikuwa nje ya ofisi hiyo, hakuwahi kuingia ndani huyu alikuwa dakitari, wana ubia naye kibiashara, walikuwa wakijadili kuhusu mgonjwa mmoja waliyetaka kumuhamishia hapo kwasababu ya usalama, alikumbuka vyema mgonjwa huyo ni mwanamke, ambaye likuwa anasakwa na watu wasiojulikana, wakapanga ahamishiwe hapo haraka iwezekanavyo…hakuingia ndani.
Wengine waliowahi kuingia humo ndani ni siku mbili , au tatu zilizopita na n i wateja wake muhimu ambao hawatakiwi kujulikana na wakati mwingi anawaendea majumbani, labda kuwa na jambo muhimu la kukutana kiofisi, …na wengine ni waheshimiwa ambao hazanii kabisa kuwa wanaweza kufanya jambo kama hilo…akamwangalia inspecta akiwaza mengi kichwani kuwa kweli amwamini  kiasi hicho na kumwambie kila mtu aliyeingia hapo…hapana atakuwa kakiuka misingi ya kazi yake.
‘Sikulazimishi kuniambia kila mtu, huenda mwenzangu upo kundini, nakushauri hataka kama haupo kundini, ujiunge na hilo kundi, ila kwa sharti moja, uwe `kigeugeu’, kwa manufaa ya taifa lako…najua ni hatari na kweli unatakiwa ujitoe mhanga, kwasababu sas hivi ni mawili ujiunge kwa wepesi, kwa kukubali au utajiunga kwa mitindo yao, kwa kudhalilika, na ukijiunga ujue una mawili kufa au kupona, kufa kama utawasaliti ukipona kwa muda ujue umeisaliti nchi yako….lakini kipi bora ufe kama kondoo na usahaulike kwenye watu wema, au ..’ simu ikalia na kuwafanya washituke, wakaiangalia bila kuipokea na ilipoendelea kuita Inspeta akamwambia aichuke kwa ishara.
‘Halloh, nani mwenzangu…nini unasema nini…mbona sikuelewei…hapana hakuna mtu kama huyo hapa..nani kakuambia hivyo….’ Na simu ikakatika.
‘Oooh, hajanitajia jina kuwa ni nani lakini nahisi kuwa ni yule rafiki yangu docta, aliyekuja hapa jana…nashangaa kaniulizia nipo na nani humu ndani, na kabla sijamjibu akasema kuwa anajua kuwa wewe upo humu hospitalini, halafu akakata simu…., sasa naona nii bora utafute sehemu nyingine ya kwenda haraka iwezekanavyo, hali sio swhari kabisa…’ akasema docta huku akiangalia huku na kule.
‘Usiwe na wasiwasi wewe ni mpiganaji mwema, unakumbuka wakati tupo shule kwenye skauti, wewe ulikuwa ni jasiri mkubwa, unakumbuka wakati tupo jeshini, wewe ulikuwa shujaa, mpaka jeshi likataka kukuchukua, sasa ni wakati wa kuionyesha dunia kuwa hiyo hukubahatisha, jitolee kwa taifa lako…nakushauri ujiunge  na hilo kundi lakini kama nilivyokuambia uwe `kigeugeu, na ni mimi na wewe tu tulijue hilo la `kigeugeu’ hiyo ndio `password yetu’, sehemu maalumu ya kukutana sio hapa au popote, ni kule ufukweni, kwenye mazoezi yetu…’akasema inspecta.
‘ Kundi, kundi gani hilo..’ akauliza Docta.
‘Usijali natumai umenielewa, ..wewe ni mtaalamu bwana…’ akasema Inspecta, na docta akifikiria sana halafu akasema `Kweli jana alinitembelea docta mwenzangu wa hospitali kuu Muhimbili, bingwa wa maswala ya akili, bingwa wa kila kitu unamkumbuka tulikuwa naye jeshini…basi anataka kuniletea mtu hapa ambaye anawindwa na watu wasiojulikana …ukichanganya na hili, na hilo la kundi unalolitaja nisilokuwa na …sijui una maana kundi gani, naona hapa hakuna usalama kabisa, nitamshauri asimlete hapa kabisa…’ akasema Docta.
‘Mhhh, kweli mshauri hivyo, namjua huyo dakitari nataka nionane naye, ikiwezekana leo…’ akasema Inspecta.
‘Kweli alikuwa akisema kuwa umepotea kimiujiza na alikuwa anakuhitaji sana, hakuniambia kwasababu gani, lakini ….yes, nimekumbuka, alisema inahusiana na huyo mgonjwa na hawo maadui wake…’ akasema Docta.
‘Ngoja nikaonane naye, naona wakati wa kufufuka umefika, au sio, nashukuru sana kwa msaada wako, najua utakuwa umelipwa haki yako..’ akasema Inspecta, na kabla hajainuka kwenye kiti mlango ukagongwa, na wote wakashituka na kuangalia kuelekea kule mlangoni. Docta akawa anajiuliza huyo ni nani amekuja wakati kuna tangazo kuwa huduma zimesitishhwa kwa muda, na hakuwa na miadi na mtu yoyote! Na wakati anajiuliza haya hata Inspecta  naye akawa anajiuliza kulikoni wakati docta alishamwambia kuwa hatagemei mtu yoyote,  ndio maana hakuvaa vitu vya kumficha sura yake ikabidi akae kimashaka kwani vifaa vya kujibadili sura alikuwa navyo, lakini alikuwa kaviweka mfukoni. Na hata anavyojibadili huyo docta hajui , hakupenda ajue kabisa mbinu zake.
 Docta akainuka pale alipokuwa kakaa na kuelekea mlangoni, nia ni kumzuia huyo aliyekuja asiingie kabisa humo ndani, akaufungua mlango kimashaka, halafu alipomuona huyo aliyegonga akataka kuufunga huo mlango, lakini akaona sio jambo jema, akatoka kwa nje na kuurudishia ule mlango kwa nyuma yake, Inspecta pale alipokaa akahisi kabisa kuwa huyo aliyekuja hakutakiwa amuone huyo aliyegonga, akasikiliza kwa makini wanaongea nini.
‘Docta, sisi tunakuheshimu sana, kwani wewe ni mtu wa watu, lakini nahisi unatuficha kitu, tulikuja siku moja hapa tukakuulizia kuwa uliwahi kumuona Inspecta, kwani kapotea kimiujiza ukasema hujawahi, lakini kutokana na uchunguzi wetu tumegundua kuwa yupo hapa…tunaomba ushirikiano wako, ujue yule ni mtu wa serikalini, tukiamua kisheria utafungiwa leseni na hata…sijui utakwenda dunia gani, tunakuuliza kwa mara ya mwisho je Inspecta yumo humu au hayupo…’akauliza huyo mtu na Inspecta akaijua hiyo sauti kuwa ni msaidizi wake ambaye katika watu asiowaamini , huyo ni namba moja, hakutaka kabisa aonane na huyo mtu hadi akamilishe uchunguzi wake.
‘Kwanini niwafiche…, najua kabisa kuwa nyie ni watu wa usalama, na huyo mtu mliyemtaja ni mtu wa serikali, na kupotea kwake ni pigo kwa taifa…halafu mimii nimfiche ili iweje…?’ akasema docta.
‘Ili iweje?..., kwani wanaofanya hivyo wanafanya ili iweje, usitupotezee muda, sisi tupo kazini kama ulivyo wewe, naomba uturuhusu kukagua humu hospitalini mwako, hiki hapa kibali cha kufanya upekuzi..’ Mlio wa karatasi ulisikika kuonyesha kuwa walikuwa wakionyesha karatasi. Na huyo docta alipoonyeshwa akawa kashikwa na kigugumizi, na kabla hajasema kitu akasukumwa pembeni .
 Alikuwa kasimama mlangoni ili kumzuia huyo msaidizi wa Inspecta asifikirie kuingia hapo, na kutafuta uongo wa kumuondoa hapo, lakini akajikuta akisukuwa pembeni na huyo jamaa akafungua mlango wa ofisi yake akachungulia kwa ndani kwa muda halafu akaurudishia ule mlango na kumwambia Docta
`Wewe ingia humo ndani kwako kaa kimya, tutakuja muda si mrefu, tunakagaua kila kona, … tukimpata umepona lakini tusipompata utatuambia umemficha wapi…’akasema huyo Msaidizi wa Inspecta na  kumwacha Docta mdomo wazi, akijiuliza Inspecta kajificha wapi humo ndani, kwani palivyo, hakuna sehemu kabisa ya kujificha.
 Aliwaangalia wale maaskari wakiondoka kukagua sehemu nyingine, akahisi walishaeleekezwa wapi Inspecta anakaa, kwani mawazo yao yalikuwa hukoo huko. Alipohakikisha hawapo upeo wa macho yake , akaingia ofisini mwake na ghafla kwenye meza yake kwa chini aliibuka mzee akiwa na ndevu nyeupe, hakuweza kumtambua kabisa katokea wapi huyo mzee, cha jabu yule mzee alikuwa hajavaa viatu, akaangalia pembeni mwa kabati, ambapo Inspecta anahifadhi ndala zake, akaziendea na kuzivaa, na bila kusema neno naye alifungua mlango na kupotelea nje….
 Haikuchukua muda wale maaskari wakarudi.
……Mambo hayooo..je mnaionaje sehemu hii,inahitaji nyongeza? Naombeni ushauri wenu, ili sehemu ijayo ikamilike, kwani tunaendea sehemu ambayo…ni nyeti…!

Ni mimi: emu-three

3 comments :

samira said...

m3 mambo mazuri mimi nimependa hili kundi haramu nahisi watajulikana soon kama inspecta atafanya kazi yake

Anonymous said...

Sehemu hii imetulia sana. Naona sasa kazi inaanza kwa Ispecta. Kwani ameshawajua wasaliti wake na kundi hilo haramu.

Mambo mazuri sasa.

Usicheleweshe kutupa uhondo huu.

BN

Faith S Hilary said...

Mmmh M3...hii sehemu mi naona iko sawa hasa pale kwenye "kukata palipo patamu" na kusubiri uhondo...mi nasubiri hiyo sehemu..."nyeti" (he said it, don't get me wrong hehehe)