Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, March 18, 2011

Maisha yana kila aina ya mitihani!


‘Jamani nilikuwa nimewaita kwa mambo ya kutafuta maisha, najua nyie ndio washauri wangu wakuu, nakumbuka hata ndoa yangu isingekuwa nyie ningelikuwa bado sijaoa. Sasa wakati naandaa muhtasari wa kuwekeza jana, ili kama inawezekana tusaidiane, nikakumbana na kisanga nyeti. Naombeni muniwe radhi, labda mtaniona nimebadilika, lakini sijabadilika na bado msimamo wangu muujuavyo ni uleule, ila niwekwa njia panda..


Tukaangaliana na rafiki yangu, halafu tukamgeukia jamaa yetu ambaye sasa hivi ni mkurugenzi wa kampuni yake binafsi. Rafiki yangu huyu tulisoma naye namjua sana, ni kati ya wale watu waliolelewa na wazazi ambao niseme walijua nini maana ya kulea. Tangu akiwa shuleni, alikuwa hana makuu, hana tabia za uhuni, yeye alikuwa ni mtu wa kusoma na kufuata taratibu zote za shule. Baada ya shule tukatawanyika kwenye vyuo mbalimbali.

Yeye alipomaliza chuo akaajiriwa kwenye kampuni yetu ya Umeme, alifanya kazi hapo miaka miwili baadaye nilipokutana naye akasema imeitishwa dharura ya kupunguzwa wafanyakazi, na yule anayetaka kujitolea aandikishe jina, na kipaumbele cha malipo mazuri kitakuwa kwa wale watakaojitolea, na yeye kaamua kujitolea, anataka kujiajiri, kwani kazi ya kuajiriwa haina maslahi kwake. Tulimshauri kuwa bado mapema na yeye alikuwa mmoja wa watu waliofanya vizuri sana shuleni, na hata kazini itakuwa hivyohivyo, lakini hakutusikiliza.

Na kweli akajiajiri kwa hela ile ile aliyolipwa iitwayo `mafao’ na mwanzoni alihangaika sana, lakini baadaye tukashangaa mwenzetu kainukia na hata kuanzisha kampuni yake ambayo ni moja ya kampuni zinazofanya vizuri sana. Na ukimuona leo huwezi kujua ni mkurugenzi fulani, ambaye ana wafanyakazi karibu ishirini na watano wa vitengo tofauti tofautii, kwani hajikwezi, hana makuu, nan i mtu wa watu..na kwakweli huwa anawalipa vizuri tu wafanyakazi wake.

‘Ndugu zanguni, kila kunapokucha nakutana na mitihani, lakini huu wa sasa umenishitua sana. Kama mjuavyo kazi yangu ina vitengo vingi, na hivi karibuni nilianzisha kitengo ambacho watendaji wake ni wanawake, na wanawake hawo sifa yao kubwa wanatakiwa wawe warembo, waaminifu na wabunifu. Nimefanikiwa kwa hilo, niliwapata mabinti watano wanaoijuahiyo kazi. Na mmojawapo ambaye mpaka niliamua baadaye nimsomeshe na kumpa usimamizi wa idara hiyo, ndiye ninayataka kumuongelea hapa.

Katika mikataba ya ajira niliyoiweka ni kuwa mfanyakazi anatakiwa awe mwaminifu, asiwe na tabia chafu ambazo zitaingiza kashifa katika kampuni, ikiwemo uhuni,ulevi, ngono, nk. Na hili nimekuwa kila kikao nawakemea sana. Na kweli wote wana lifuata hilo, kwani nimeshatoa onyo kivitendo, kila anayejishuhusisha ta tabia chafu namfukuaza kazi, sina machezo.

Huyu binti ambaye nimemwamini sana ni mke wa mtu, na ainavyoonekana waliona wakiwa wadogo sana, kwani hata sasa hivi ukimuona huamini kuwa ni mke wa mtu aliyedumu kwenye ndoa miaka mitano, …inatimia miaka mitano sasa, hawajabahatika kupata mtoto….’ Alipofika hapo akanywa maji na kufikiri kidogo.

Huyu binti ni mchapa kazi kweli na ni mtu wa imani za dini, huwezi kumuona kasimama kwenye majungu au kuteta teta watu. Nimemwamini kupita kiasi, na mara nyingi nakuwa karibu naye katika kujua maendeelo ya kitengo chao na hata kazi nyingine. Lakini niligundua kuwa ana matatizo, na sio rahisi kugundua haraka, ila kwa vile nami napenda sana kujua matatizo ya wafanyakazi wangu, na nimesomea kidogo kujua hisia na mabadiliko ya watu, niligundua mapema kuwa huyubinti ana tatizo ambalo hapendi watu walijue, anajitahidi sana kulificha.

Siku moja nilimgundua akiwa peke yake akilia, iliniuma sana, kwasababu ni mtu ninayempenda kwa tabia zake na uchapaki kazi wake. Sikuweza kuvumilia nikamuita ofisini, na nilitumia hekima kutafuta nini tatizo alilo nalo. Pamoja na kujuana na kuwa karibu naye sana, bado ananiogopa kama bosi wake, na anaijua kuwa sina mchezo na kazi.

‘Bosi kwa leo sina mudi wa kukuambia chochote, ila nimewaza sana, na hutaamini tatizo nililo nalo limefikia hatua …bosi samahani sana, nitakuja kukuambia siku nyingine, ila vyovyote iwavyo naomba liwe moyoni mwako, na maamuzi yako ukitoa iwe siri yako, hata kama utaamua kunifukuza kazi, basi usije ukasema lolote…lakini siwezi kukuambia kwa leo kuwa ni tatizo gani, ila linahusiana na ndoa yangu..’ akaniambia na alipotaja ndoa yake nikashituka, sipendi kuingilia ndoa za watu, …ila kama inakwamisha utendaji wa kazi huwa natoa ushauri…ushauri nasaha au sio.

Basi sikutaka kumwingilia sana kiundani, ila nilimuomba sana asiwe analia-lia na kama anahitaji likizo nitampa ili aweze kuyashughulia majukumu yake ya ndoa, lakini akasema hilo tatizo halihitaji likizo, ni swala nyeti sana, utatuzi wake hautakiwi uzidi mwaka. Basi tukaachana naye ikapita miezi miwili. Ndio jana akaja wakati natayarisha mambo yangu ili nipate ushauri kwenu. Sasa yale mambo tutayaongea siku nyingine, nataka mnishauri kwa hili, ninalotaka kuwaambia sasa.

Nikiwa ofisini asubuhi sana, kama kawaida yangu, huyu binti, au mke wa mtu akaingia ofisini kwangu, alikuwa katika uso wa huzuni sana, nikajua ni yale yale mambo yake. Nikamuomba atulie na aniamini mimi, kuwa nipo tayari kumsaidia kwa lolote lile…nilipotamka hivyo sikuwa na maana mbaya, nilikuwa nimelenga `kimaslahi zaidi’ ila yeye aliposikia hilo neno kwa lolote lile akaniangalia machoni halafu akainama chini na kusema;

‘Bosi unamaanisha kweli kwa lolote lile, …maana usije ukanifukuza kazi, bosi kama nilivyokueleza, hili sio swala la mchezo, na vyovyote itakavyokuwa naomba iwe siri yako…’ akasema na kuniangalia machoni kuhakikisha kauli ninayotoa inatoka moyoni.

‘Bosi mimi na mume wangu tumeishi katika ndoa miaka mitano sasa, hatujabahatiska kupata mtoto, na katika kuhangaika sana, vipimo, ibada na kila kitu tumekwama, hatukufanikiwa jambo lolote. Tukaamua kumuona dakiatari bingwa, bingwa zaidi kwani tumeshapitia madakitari bingwa kabla, ila huyu anaaminika sana kwa mambo hayo, bingwa wa mambo ya uzazi , ….’ Akainama kwa huzuni, na machozi yakamtoka.

`Bosi nashindwa kukuambia kwani licha kuwa tunapendana sana na mume wangu, lakini jamii inayotuzunguka imekuwa ni mwiba wa ndoa yetu, na amefikia hatua wanafamilia waliamua niachike eti kwasababau sizai, walisahau kuwa ndoa ni kitu kingine na watoto ni kitu kingine, tumepima hatuna matatizo, …lakini docta alisema kuna nafasi kubwa kuwa tatizo lipo kwa mume wangu, kuwa kuna uhaba wa mbegu, ….na kitu kama hicho, huenda tukawa tunapishana ki nguvu kitu kingine alisema..sielewei sana mambo hayo, lakini nilivyochunguza zaidi kuwa kama mume wangu akipata mke mwingine anaweza kuzaa, …! Lakini imani yetu hairuhusus wake wawili!

Mume wangu tunapendana sana, akaniambia kitu kilichonishitua sana aliniambia kwa vile wanajamii wanachotaka ni mtoto, basi tufanye njia nyingine ya kupata mtoto…nilitaka kuzimia, kwani mume wangu unavyoniona mimi ni nusu, ni mtu wa dini, ile imani kali, sikutegemea maneno kama hayo yatoke mdomoni kwake. Alisema haraka kuwa ‘tafuta chapa yangu, lakini asiwe ndugu yangu, kwasababu uki-adapt mtoto ni yale yale, na ukimpata anayefanana na mimi tunaweza tukapata mtoto,..adapt na hilo ni yale yale tu, ila nisijue, ila …siri yangu na yako na huyo mtu, na ikiwezekana hata huyo mtu asijue nini unachotaka…sitaka kusema zaidi, kwasababu nakupenda, na sitaki tuachane, ila kinachoendelea kwenye familia yetu kinaweza kikavunja ndoa yetu.., nakuachia wewe utajua mwenyewe nini cha kufanya,ila mwaka ukiisha nitajua mimi nini la kufanya…’

Bosi wewe na mume wangu mnafanana kama mapacha..’akaniambia na kuniangalia machoni, halafau akaona aibu. Mimi mwenyewe aliposema hilo neno la kufanana kama mapacha, nikajua kuna balaa linakuja, nikatafuta njia za kumtoa nje lakini akasema lazima animbie kila kitu ili nikiamua niamue kikamilifu, kumfukuza kazi au kumsaidia…kwasababu baada ya kauli hii sidhani kuwa utaniamini tena, na hata mimi sitaweza kukuangalia machoni tena.

‘Bosi tunataka mtoto, ili ndoa yetu iwepo, ili niwe na raha, na mue wangu…naomba msaada wako…’ akapiga magoti mbele yangu. Unajua nilitamani nimfukuze, lakini hekima ikanilinda, nikamuonea Huruma yule binti. Nilimuuliza swali moja kubwa sana;

‘Je wewe unamwamini mungu? Na unajua kuwa mitihani kama hiyo ipo , hebu kumbuka kisa cha nabii Ibrahimu waliishi mapaka uzeeni bila mtoto, lakini yote yalikuwa majaribu ya Mungu, walizaa uzeeni..sasa wewe umwaminifu hilo unalotaka kufanya ni kinyume cha dini, ni kinyume cha ndoa , na huna uhakika kuwa litakusaidia…inuka sinipigia magoti, nakushauri nenda kafunge sana, muombe mungu wako atakusaidieni…’ nikatoka pale kwenye kiti nikafungua mlango ili aondoke, lakini akabaki akiwa kasimama.

‘Basi bosi , nakutakia kazi njema, kwasababu nakumbuka ulianza kusema kuwa utanisaidia kwa lolote lile, pili nilikuwambia nina mawili kunikubalia ombi langu au kunifukuza kazi, …na kwa hali niliyoo nayo naona heri …, kwani nimefunga, nimefanya kila liwezekanalo sijafanikiwa, lakini siwezi kujizalilisha tena kwa mtu mwingine, …huwezi jua nini ninachokipata ndani ya familia yangu hasa ya ndugu na familia za mume wangu…sina raha, lakini siwezi kabisa kuzalilika tena, …na nampenda sana mume wangu,kama utalisikia lolote limetokea usishangae ni heri uamuzi nitakaochukua kuliko kuonekana kioja ndani ya jamii isiyoeleweka, …maisha hayana maana kwangu..kwaheri bosi!

Sasa ndugu zanguni sijui nini kinaendelea kwa huyo binti, na aliondoka akwia katik ahali mbaya sana, ya kimawazo na kujiona kazalilika, na mawazo yangu yananipeleka mbali kuwa anaweza..anaweza…’ akatulia kufikiri na rafiki yangu akamalizia;

‘Kujiua labda….’ Akasema rafiki yangu

‘Haswa, kwani alipotoka pale alipitia mezani kwake akachukua kila kitu chake , na hakuaga mtu’ akasema jamaa yetu huyu. Na asubuhi ya leo kwa wasiwasi nikaona nipitie kwao, uue mue wake kasafiri, na sijui alisafiri kwasababu ya kumpa nafasi hiyo au la…nikaona nipitie kumwambia arudi kazini na mimi nitamkutanisha na mke wangu, kwani mke wangu anajua sana kumweka sawa mtu ki-mani, lakini sijamwambia mke wangu lolote.

Basi nikapitia nyumbani kwake, nilipofika, ilikuwa subuhi, sana na yeye huwa anawahi sana kazini, nikagonga mlango kimiya, nikajaribu kutafuta majirani kujua kuwa hayupo, lakini ilikuwa asubuhi sana, basi nikaamua kuufungu mlango, na nilishangaa upo wazi haujafungwa na fungua, nikaingia mle ndani, nikaita ..Rose, Rose, kimya…nikaona kuna jambo limetokea, kwani mle ndani kuna oneyesha dalili kabisa kuwa kuna mtu, au alikuwepo mtu…nikaamua kufungua mlango ambao nahisi ni wa chumba chao,…balaa…nilijikuta nakosa la kufanya nikataka kukimbia nikashindwa…

Simu ya jamaa ikaita na akaisikiliza ,akasema anaitwa haraka ofisini, kuna askari wanamsubiri…akaondoka!

Nisiwachoshe, hiki ni kisa kifupi,…hakihitaji kusubiri, nilitaka nikiendeleze kivyangu, lakini nikaona kwa vile kinagusa hisia za watu niwasikilize nyie mtasemaje, kwani tukio kama hili ni mara ya pili kulipata, je nyie kama nyie mngemshaurije huyu mtu, Na sijui kimetokea niniukumbuke huyo binti keshaondoka, na hatujui nini kinachoendelea huko!

Huu ni mkasa wa Juma


Ni mimi: emu-three

6 comments :

Yasinta Ngonyani said...

Hapa kuna mtego hapa. Kwanza kwa nini familia ya mume iingilie maisha ya kijana wao ? na kwa nini kila wakati inapotokea tatizo kama hili la kukosa mtoto basi ni tatizo la mke...Nionavyo mimi hapo amemtega tu kama kweli ana imani? kama anampenda kwa dhati? Na yeye Rose kwa vile anampenda sana mume wake na amemchochea sana kuwa hakuna shida ukimpata anayefanana nami itakuwa safi ila usipofanya baada ya mwaka basi mimi nitajua nifanyeje. Basi hapo kamtisha kwa hiyo yupo tayari kufanya lolote lile ila mradi tu mume asioe mke mwingine. Ushauri wangu mimi nisingefanya kama mume wangu atakavyo. Duh hapa inatakiwa ushauri wa busara ...naona kama kichwa changu kinazunguruka....ngoja niachie kwanza hapa

John Maembe. said...

Hapo kuna hali tofautitofauti sana kweli ukiona m2 anamacho mekundu sio anumwa bali ni matatizo yamemuelemea.
Mi naona huyo mdada baada ya hayo matatizo yamemsababishia msongo wa mawazo(STRESS) ambao mwisho wake ni mbaya siku zote na dawa ya hilo tatizo ni Kupata m2 aliyeenda shule katika maswala ya Ushauri nasaha kama Boss anavyotaka kufanyia na sio hawa walalahoi wa mitaani.
Sina lazaidi nasubiri hiyo nione mwisho uutakuwaje kwani huyo mume wake haijulikani huko alikokwenda kaenda kufanyaje na akirudi itakuwaje.
Kila la Kheri M-3.

Simon Kitururu said...

Hili nalo ni ndude la kitu!

Ngojea ninlikalie vizuri kiwazo!

Koero Mkundi said...

Kila mtu na lake moyoni.....

Faith S Hilary said...

Haya ndio mambo ya "eating your own words" maana ukisema hivi basi mtu anachukulia vingine kabisa. Ndio kasema "chochote" lakini hufikirii kwanza...ok kachukua miezi miwili kabla ya kusema habari yote lakini mmh! Na hii issue za watoto na ndoa...matatizo kweli. Angeendelea tu kumuomba Mungu na kulinda ndoa, watu wanakaa zaidi ya miaka 10 bila watoto na wengine pia wanapata...haya tuone asije akawa amechukua uamuzi mbaya baadae...

emuthree said...

Waungwana, wajumbe, majirani, wakuu, wapendwa, hata mimi mumeniacha njia panda, lakini sio mbaya, maana nilihitai sana mawazo (hasa hayo ya kila mtu lake moyoni)ili nikikutana na jamaa yetu niweze kumpa `ya moyoni' kama ingelikuwa wewe ungelichukua uamuzi gani, lakini sio mbaya, nikikutatana naye tunajua jinsi ya kumshauri, kwani hatujajua nini kimemsibu huyo mwanamke, na ukumbuke ni mke wa mtu!
Nitafuatilia na nitawapa nini kilitokea na hataimaye yake ilikuwa vipi!