Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, August 24, 2016

Tenda wema uende zako

‘Leo nimepata Bahati kubwa kweli’ jamaa mmoja alikuwa akimhadithia mwenzake kijiweni kwa zile walizoziita habari za leoleo.

‘Bahati gani hiyo hebu nipe za `live’ mwenzake akamsogelea huku akishika shikio kuonyesha kuwa sikio liko wazi kumsikiliza

‘Nimepanda daladala la kwanza, konda hakunidai nauli, la pili hakunigusa kabisa, na ajabu abiria mmoja niliyekaa naye kwenye gari la kwanza alipoteremka akawa amedondosha mkono, elifu kumi kavu kabisa, nikaisweka mahala pake! Siunajua tena bongo, bajeti ikawa imekubali’ aliinua juu mkono kwa kujipongeza.

‘Rafiki yangu hapana, mimi mimi sikuungi mkono kwa hilo, ni kwanini hukumrejeshea huyu abiria aliyedondosha pesa yake..au ungempa konda ili aitangaze hapo ungekuwa umetenda uadilifu. Nasema hivyo kwasababu, abiria mwenzako ni sawa na wewe ipo siku na wewe utadondosha na kama ungefanya usamaria mwema kwake na wewe ungefanyiwa hivyohivyo…’ akasema mwenzake

‘Wewe , sirudii ujinga huo tena, niliwahi kukuhadithia kisa kilichonipata huko kijijini. Siku moja nilikuwa nalimia bustani zangu, ilikuwa karibu na barabara. Mara likapita gari la mhindi mmoja, ilikuwa siku ya mvua, kwahiyo magari mengi yalikuwa yakikwama kwama....

Basi siku hiyo mara likapita gari la mhindi lilikuwa landrover, unajua tena magari ya aina hiyo hayakwami kwami kwenye matope, Lilipofika pale nilipo, likawa kama linataka kudondoka, na ajabu kukadondoka bahasha kubwa toka ndani, ya hiyo gari..sijui ilidondakaje. Nikaisogelea na kuikagua, na ndani kuliswekwa mabulungutu ya manoti. Fikiria maisha yangu yote sijawahi kuona pesa za kiasi kikubwa hivyo, hasa kwa maisha yetu kule kijijini.

Nilifikiri kwa muda nikasema, Hapana huu sio uungwana, mimi nimelelewa vyema na wazazi wangu... nikaamua kuwakimbilia ili niwaopatie pesa yao.

Na kwasababu kulikuwa na utelezi, na barabara ilikuwa mbovu, ilikuwa ni rahisi kulifikia lile gari kwa kupitia njia za mkato. Nikalikuta limesimama. Wenyewe walikuwa wakibishana kuwa ile bahasha wameisahau huko walipotoka kwahiyo ni vyema warudi.

Mara pale mimi nikatokea, nikiwa na ile bahasha mkononi,
'Samahani wandugu wakati mnapita pale kwenye shamba langu mlidondosha hii bahasha...'nikawaambia

Jamaa walinitolea macho ya mshangao.

Yule Mhindi aliniangalia kwa muda, halafu kwa mshangao akanizaba kibao. Kibao cha haja, hadi vidole vikaonekana shavuni kwangu. Na baadaye akatoa bulungutu moja kati ya yale mabulungutu yaliyokuwemo humo ndani na kunipatia, halafu akaniambia

‘Weye afrika gani, ..., utakufa masikini…’ Akacheka sana na wenzake wakaungana naye kwenye kucheka, na bila kusema zaidi  wakaingia kwenye gari lao na kuondoka...

'Niliiumia sana moyo wangu, nilitamani niwakimbilie niwatukane, lakini lile bulungutu nililopewa lilimaliza yote. Nikapiga mahesabu kuwa pale hazipungui milioni kadhaa. Na kweli ilikuwa milioni tano. Hivi fikiria pesa yote hiyo enzi hizo milioni tano ilikuwa pesa nyingi sana kwangu, Pesa hiyo niliweza kujenga banda langu na kufungua duka, na hapo dukani nikaandika `tenda wema uende zako..’

'Na tangu siku hiyo, sifanyi makosa hayo tena..nikiokota ni bahati yangu.....'

Mimi sikupenda kuendelea kuwasikiliza, kwani hitimisho lake sikulipenda, na huo usemi unaashiria enzi nyingine ya ajabu, enzi iliyotabiriwa , enzi ya kukaribia mwisho wa dunia, enzi hii uaminifu hautakuwepo tena, enzi ya watu kunyang'anyana,  mdogo hamuheshimi mkubwa, matusi ni lugha ya kawaida, matendo yasiyofaa kuenea....

Je hii hali hatuioni..? Ndio hii hali iliyopo sasa, mwenye nacho hamjali asiyekuwa nacho na asiyekuwa nacho anatafuta kupata kwa njia yoyote ile, hata ile isiyo ya halali..Angalia sasa hivi ukidondasha kitu kwa bahati mbaya akiokota mwenzako ni chake, sio chako tena...mtu huyo , hawezi kukushitua na kukuambia samahani umedondosha kitu chako..., hasa pesa.

 Enzi hii ya ajabu imefikia hatua watu wanaogopana , kama ni usiku unaombea mungu usikutane na mwanadamu mwenzake , ni heri ukutane na mnyama, maana mnyama anaweza akakuogopa akakumbia lakini sio binadamu mwenzako, ....huyo binadamu mwenzako anaweza akawa ni jambazi, ambaye hatosheki na kukuibia tu,...anaishia na kukuua, ili usije kumtaja..hivi sasa huruma, upendo na kuaminiana imekuwa ni misemo tu,..na huenda ikawa misemo adimu.

Tumuombe mungu atuepushia na hii hali, kwani kutokana na kazi zetu kuna watu wanarudi usiku au tunatoka majumbani asubuhi sana, je tutaishije, tutawahije kwenye sehemu zetu za kutafuta riziki. Na tatizo hili linazidi kwasababu watu hawazithamini tena dini, watu hawamjui mungu.... Dini zimekuwa ni sehemu tu ya kukamilisha maisha yetu, ..kufunga ndoa, nk

Tujiulize ni kwanini hii hali inazidi...na tufanye nini....

Ni mimi: emu-three

2 comments :

Anonymous said...

Huyo alionyesha ukoloni wake tu, mtu na akili zake hawezi kufanya hilo, na asili ya uafrika ni kusaidiana, kwahiyo wewe uliyezababwa kibao usiige mambo yao, ujima na ujamaa umetujengea ushirikiano

EDNA said...

Hahaa mie pamenifurahisha hapo Mhindi alipomzaba vibao....you made my day.